MIPANGO YA DK MWAKYEMBE YAGONGA UKUTA...

Dk Harrison Mwakyembe.
Utekelezaji wa mipango ya Wizara ya Uchukuzi, inayosimamiwa na Dk Harrison Mwakyembe, kwa mwaka huu wa fedha uliobakiza miezi mitatu kwisha, ni wazi umekwama.
Wakati amebakiza muda huo mfupi kutimiza malengo aliyoahidi bungeni, na kuidhinishiwa bajeti ya Sh bilioni 317.7, mpaka sasa Dk Mwakyembe amepewa asilimia 25 tu ya fedha alizoidhinishiwa.
Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Miundombinu, Peter Serukamba, akizungumza jana kuhusu bajeti ya wizara hiyo kwa mwaka ujao wa fedha, aliiagiza Serikali ikamilishe asilimia 75 ya fedha iliyobaki kwa wizara hiyo, ili ikamishe shughuli zake.
Katika bajeti ya mwaka huu wa fedha unaoisha, kati ya Sh bilioni 317.7 zilizoombwa, Sh bilioni 64.9 zilipangwa kutumika kwa ajili ya matumizi ya kawaida na Sh bilioni 252.7, kwa ajili ya matumizi ya miradi ya maendeleo.
Baadhi ya mipango ya Wizara ya Uchukuzi ni pamoja na ukarabati wa mabehewa 31, kujenga upya injini nane za treni, kufanya malipo ya awali ya ununuzi wa injini za treni mpya 13, kufanya malipo ya awali ya ununuzi wa mabehewa mapya ya abiria 22.
Pia kukarabati mabehewa mabovu ya mizigo 125, kufanya malipo ya awali ya ununuzi wa mabehewa mapya ya mizigo 274, kufanya malipo ya awali ya ununuzi wa mabehewa mapya ya breki 34 na ukarabati wa karakana za Tabora na Dar es Salaam.
Katika sekta ya anga, walipanga kukamilisha ukarabati wa Kiwanja cha Ndege cha Bukoba, Kiwanja cha Ndege cha Kigoma, Kiwanja cha Ndege cha Tabora na Kiwanja cha Ndege cha Arusha.
"Fedha hizo zikitolewa kwa wakati zitaiwezesha TRL kutekeleza mipango yake kwa wakati uliopangwa ili kuiwezesha kutoa huduma inayotarajiwa," alisema Mwakyembe wakati akiwasilisha bajeti mwaka jana.
"Kuchelewa kutolewa kwa fedha hizi kumechangia kwa kiasi kikubwa kukwamisha miradi mingi ikiwemo matengenezo ya reli ya kati," alisema Serukamba.
Hata hivyo, pamoja na changamoto hiyo ya kuchelewa kutolewa kwa fedha hizo, Serukamba alitaja maeneo mengine yaliyofanyiwa kazi na bajeti ya mwaka jana, ambayo bado miradi yake itaendelea kwa mwaka wa fedha ujao, kuwa ni gati sita za Ziwa Victoria, Nyasa na Tanganyika, utengenezaji wa meli katika maziwa hayo sambamba na kulipia ushuru ili zianze kufanya kazi.

No comments: