MR BEAN ALAMBA BINGO, ALIPWA NA BIMA FIDIA YA KIHISTORIA UINGEREZA...

KUSHOTO: Polisi wakishughulikia kuliondoa gari la Mr Bean eneo la ajali. KULIA: Rowan Atkinson maarufu kama Mr Bean.
Mwigizaji Rowan Atkinson maarufu kama 'Mr Bean' amefanikiwa kulipwa Pauni za Uingereza 910,000 na bima kama fidia ya matengenezo ya gari lake aina ya McLaren F1 supercar baada ya kupata ajali - hii ikiwa ni fidia kubwa zaidi kuwahi kutolewa nchini Uingereza.
Bean alipata ajali hiyo baada ya kushindwa kulimudu gari hilo lenye mwendokasi wa hadi maili 240 kwa saa, linalokadiriwa kuwa na thamani ya Pauni za Uingereza milioni 3, Agosti 2011.
Baada ya kuserereka barabarani karibu na Peterborough, gari hilo likajibamiza kwenye mti na kuwaka moto.
Lakini wakati nyota huyo mwenye miaka 58 akinusurika kifo kwenye ajali hiyo mbaya akiwa kavunjika bega, gari lake - moja kati ya aina 64 tu duniani - liliharibika vibaya.
Sehemu yote ya nyuma ya gari hilo iliharibika kabisa wakati injini ya lita 6.1 iliishia kutupwa umbali wa yadi 20.
Kampuni ya bima ya Atkinson ilitumia karibu miezi minane kushughulikia madai hayo, kabla ya kukubali kulipa kiwango hicho kikubwa zaidi cha fidia.
Sasa, baada ya zaidi ya mwaka wa marekebisho ya wataalamu kwenye karakana ya McLaren huko Woking, Surrey, gari hilo limerejea likiwa safi kama jipya.
Hatahivyo, Atkinson, ambaye aliripotiwa kuwa na utajiri wa Pauni za Uingereza milioni 71, hakutoka salama. Kwa mujibu wa wataalamu, michango ya bima ya gari la nyota huyo itapanda hadi kufikia Pauni 60,000 kwa mwaka kufuatia ajali hiyo iliyosababisha uharibifu mkubwa.
Ben Stagg, meneja anayehudumia wateja wakubwa katika kampuni ya bima ya RK Harrison, alisema: "Inagharimu kati ya Pauni 10 - 15,000 kwa mwaka kuiwekea bima McLaren F1 nje ya barabara katika gereji.
"Kama unataka kuiendesha - na inaonesha Atkinson aliiendesha sana - michango ya bima inapanda hadi kati ya Pauni za Uingereza 20 - 40,000 kwa mwaka sababu ya ongezeko la hatari za barabarani.
"Sasa amepata ajali, kampuni ya bima ya Atkinson inaweza kuongeza michango kwa asilimia nyingine 50."
Akicheza kama Mr Bean, Atkinson amekuwa akitumia gari aina ya Mini. Katika maisha halisi, anatumia gari lake aina ya McLaren kwa kusafirika kati ya nyumbani kwake Northamptonshire na anakofanyia majukumu yake ya uigizaji mjini London, pia kwa kwenda mapumzikoni na familia yake.
Atkinson alitumia Pauni za Uingereza 634,500 kwa ajili ya gari lake la kimichezo mwaka 1997, lakini ameshuhudia thamani yake ikiporomoka katika miaka ya hivi karibuni.
Mwaka jana, aina moja iliuzwa kwa Pauni za Uingereza milioni 3.4. Hadi wakati ikipata ajali, gari hilo lilikuwa limetembea maili 38,000. Atkinson alisema kurerejea kuendesha gari tena baada ya miezi 16 ilikuwa kama 'kuvaa sweta ulilolizoea'. Aliongeza: "Imekuwa sehemu ya maisha yangu. Natarajia kufikisha maili 100,000."
Ajali hiyo ilikuwa ya pili kwa Atkinson kwenye gari hilo. Mwaka 1999, alijibamiza nyuma ya gari aina ya Rover Metro.
Fidia ya Pauni za Uingereza 910,000 ni mara tatu zaidi ya rekodi ya malipo iliyokuwepo awali kwa ajili ya matengenezo. Mwaka 2010, Aviva alilipwa Pauni za Uingereza 300,000 kutengenezea gari lake aina ya Paganini Zonda.

No comments: