DCI MANUMBA SASA APUMULIA MASHINE HOSPITALINI...

Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai nchini (DCI), Robert Manumba.
Hali ya afya ya Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai nchini (DCI), Robert Manumba ambaye hivi sasa anapumua kwa msaada wa mashine, bado inahitaji uangalizi wa karibu wa madaktari na wauguzi.
Mkurugenzi wa Tiba wa Hospitali ya Aga Khan, Dar es Salaam, Jaffer Dharsee alithibitisha hayo jana katika taarifa yake iliyoelezea hali ya Manumba anayeendelea kupatiwa matibabu katika hospitali hiyo.
“Uongozi wa hospitali ya Aga Khan unapenda kuujulisha umma, kwamba DCI Manumba bado yuko hospitali anaendelea na matibabu. Hali ya afya yake bado inahitaji uangalizi wa karibu wa madaktari na wauguzi,” alisema.
Katika hatua nyingine, ndugu, jamaa, marafiki na maofisa wa ngazi mbalimbali wa Polisi waliendelea kufika hospitalini hapo kumjulia hali Manumba ambaye amelazwa katika chumba cha wagonjwa wanaohitaji uangalizi maalumu (ICU).
DCI Manumba aliugua ghafla na kulazwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) Januari 14, kabla ya kuhamishiwa Aga Khan kwa ajili ya uchunguzi zaidi na kulazwa ICU.

No comments: