MMILIKI WA L.A. LAKERS AKIMBIZWA HOSPITALI KWA KUKAUKIWA MAJI MWILINI...

Mmiliki wa timu ya mpira wa kikapu ya L.A. Lakers, Jerry Buss amekimbizwa hospitali mjini Los Angeles juzi usiku ambako alipatiwa matibabu ya ukosefu wa maji mwilini, vyanzo vya habari katika familia ya Buss vimeeleza.
Kwa mujibu wa vyanzo hivyo, Buss mwenye miaka 78 alianza kuugua akiwa nyumbani kwake majira ya saa 3:00 usiku na mtu mmoja wa ndani ya nyumba hiyo akapiga simu ya dharura. Wafanyakazi wa Kitengo cha Zimamoto cha mjini Los Angeles walifika na madaktari wakamkimbiza Jerry kwenye hospitali moja mjini humo.
Buss bado anaendelea kupatiwa matibabu, lakini mwakilishi wa Lakers amesema, "Anaendelea kupata nafuu na anatarajiwa kuruhusiwa hivi karibuni."
Mara ya mwisho kwa Buss kulazwa hospitali ilikuwa Desemba mwaka jana kutokana na kuganda kwa damu miguuni kulikosababishwa na kusafiri sana mara kwa mara.

No comments: