SABABU ZA UKAWA KUMPOKEA LOWASSA HIZI HAPA


Baada ya miaka 38 ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), kada wake maarufu,
Waziri Mkuu mstaafu, Edward Lowassa amejitoa na kujiunga na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA). 

Kwa kujiunga na Chadema katika sherehe iliyofanyika kwenye hoteli maarufu Kunduchi, Dar es Salaam, Lowassa anajisafishia njia ya kuteuliwa kugombea urais kupitia Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) ambao juzi ulimwalika kujiunga nao. 
Waziri Mkuu huyo aliyejiuzulu mwaka 2008 kutokana na kashfa ya Richmond, alithibitisha kuwa Safari ya Matumaini aliyoiasisi ndani ya CCM inaendelea, akimaanisha nia yake ya kutaka kuwa Rais wa Tanzania.
“Kama Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alivyosema, CCM siyo baba yangu wala mama na kwamba kama Watanzania hawapati mabadiliko ndani ya CCM watayatafuta nje ya CCM. Sasa tuyatafute mabadiliko hayo nje ya CCM,” alisema Lowassa. 
“Hivyo basi, baada ya kutafakari kwa kina nimeamua kuwa kuanzia leo ninaondoka CCM na kuitikia wito wa Ukawa kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kuungana nao katika kuleta mabadiliko ya kweli ya nchi yetu,” alisema mbunge huyo wa Monduli mkoani Arusha tangu mwaka 1995.
Akieleza sababu za kutoka CCM ambako aliwania urais mwaka huu na kutemwa
katika vikao vya uteuzi, Lowassa alisema anaamini hakutendewa haki katika mchakato mzima wa kupendekeza majina na kuteua mgombea wa Urais kupitia chama hicho tawala. 
Alisema mchakato huo uligubikwa na mizengwe, ukiukwaji wa maadili, uvunjaji
wa Katiba na taratibu za uchaguzi za CCM, na dhahiri, alidai uchaguzi ulisimamiwa
kwa upendeleo na chuki dhidi yake.
“Kwa mantiki hiyo, nitakuwa mnafiki kama nitaendelea kujidanganya mimi mwenyewe na umma wa Watanzania kwa kusema kuwa bado nina imani na CCM au kuwa CCM ni chama kitakachowaletea ukombozi wa kweli wa kiuchumi, kisiasa na kijamii. 
“CCM niliyoiona Dodoma siyo tena kile chama nilichokulia na kilichonipa malezi na maadili ya siasa yaliyojengwa kwenye misingi ya haki, usawa na uadilifu,” alisema Lowassa na kuongeza kuwa kama Mtanzania aliye na uchungu na nchi yake, “nasema imetosha na sasa basi!”
Akielezea kuhusu kuendelea kwa falsafa yake aliyoitumia CCM kuomba urais, Lowassa aliyefuatana na mkewe Regina na familia yake, alisema: “Safari ya Matumaini inaendelea kupitia Ukawa, lakini haitafanikiwa iwapo sote hatutajiandikisha kupiga kura. Natoa wito kwa wakazi wa Dar es Salaam kutumia fursa iliyopo kujiandikisha kwa wingi. Naiomba Tume ya Uchaguzi iongeze siku za muda wa kujiandikisha kama ilivyofanya Njombe.”
Akizungumzia kuondoka kwake CCM aliyojiunga nayo ilipoasisiwa mwaka 1977, Lowassa alisema hakufanya uamuzi huo kwa pupa, lakini unafika wakati wa kuchukua maamuzi hata kama ni magumu kwa kuamini fika kuwa ni kwa maslahi ya Taifa. 
Chadema, CUF, NLD na NCCR-Mageuzi kwa mwaliko wao na imani yao na kuthamini mchango anaouweza kutoa kufanikisha azma ya kuleta mabadiliko na maendeleo. 
Lowassa aliyevalia shati la maji bahari na suruali ya ‘dark blue’ na viatu nyeusi, aliwasili kwenye ukumbi wa mkutano saa 10.19 akifuatana na viongozi wa Ukawa. 
Alizungumza kwa dakika 15 kuanzia saa 10.29 na ilipofika saa 10.51 alikabidhiwa kadi ya Chadema na Mwenyekiti wa Taifa wa chama hicho, Freeman Mbowe, akitanguliwa na mkewe Regina. Mbali ya hao wawili, familia yake ambayo inahusisha watoto watano, pia imeelezwa kujiunga na Chadema pamoja na wafuasi wake kadhaa akiwamo Naibu Waziri wa zamani, Goodluck ole Medeye ambaye alisema leo atazungumzia hatima yake kisiasa. 
Akijibu maswali ya waandishi wa habari, Lowassa alisisitiza hahusiki na kashfa ya Richmond na kwamba amechoshwa na tuhuma hizo. 
“Nimechoka na suala hili, nimesema kama kuna mtu ana ushahidi aende mahakamani. Kama huna ushahidi, please, shut up and keep quiet (kama huna ushahidi nyamaza),” alisema Lowassa na kuongeza kuwa hatalipa kisasi na kuwa wanaosema atalipa kisasi wanaogopa kwani wamefanya dhambi gani. 
Kwa upande wao, Mwenyekiti wa NLD Taifa, Dk Emmanuel Makaidi alimkaribisha kwa moyo mkunjufu Lowassa katika Ukawa na asahau mambo ya CCM. Naye Makamu Mwenyekiti wa CUF Zanzibar, Dk Juma Duni Haji alisema Lowassa ni jembe kwasababu wameongeza nguvu ya Ukawa ulioasisiwa wakati wa Bunge la Katiba mwaka jana. 
Mwenyekiti wa Taifa wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia alisema Lowassa ni jasiri na kwamba Ukawa haitamwaga damu katika kuingia madarakani. 
Mbowe ambaye alikuwa mwenyeji wa Lowassa jana, alikiri kuwa mchakato wa
kumwingiza mwanasiasa huyo ndani ya Chadema haukuwa rahisi. 
Alisema kulikuwa na hofu kubwa ndani ya chama chake na kudai kuwa baadhi ya viongozi wa CCM walimpigia simu wakitaka asimpokee mwanasiasa huyo. 
Akitetea tuhuma zinazoelekezwa dhidi ya Lowassa, Mbowe alisema hawawezi kuishi kwa mambo ya zamani na yasiyo na ushahidi, na chama hicho hakiwezi kuwa chama cha kuhukumu watu. 
Alisema wamekubali kumchukua Lowassa kwa sababu ya rekodi yake ya utendaji na kwamba atakuwa na haki zote sawa na mwanachama mwanzilishi wa Chadema. 
Lowassa aliyezaliwa Agosti 26, 1953, sasa anajiandaa kupeperusha bendera ya Ukawa katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 25, baada ya vyama hivyo vinne kufanya uteuzi wao wa ndani, lakini Chadema ikimsimamisha yeye na vyama vingine vitamuunga mkono. Kwa mujibu wa wakuu hao wa Ukawa, mgombea wao atapatikana mapema mwezi ujao kabla ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi kufanya uteuzi wa wagombea Agosti 21, mwaka huu. 
Licha ya kuwapo kwa viongozi wengi wa kitaifa wa Ukawa, kiongozi wa juu
aliyekosekana jana alikuwa Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willbrod Slaa. 
Naibu Katibu Mkuu wa Chadema Zanzibar, Salum Mwalimu alipoulizwa kuhusu kukosekana kwa Slaa, alisema ni vyema akatafutwa mwenyewe. “Lakini kuna jambo gani kubwa kwani hata viongozi wengine hawapo kama John Mnyika,” alieleza Salum, hata baada ya kueleza kuwapo kwa viongozi wengine wa juu, bado alisema hakuna tatizo lolote.
Mkutano huo ulihudhuriwa na wabunge kadhaa wa Chadema na wafuasi wao.

No comments: