Mahakama ya
Hakimu Mkazi Mkoa wa Morogoro, imekubali ombi la upande wa mashitaka, katika
kesi ya kula njama na kufanya ukatili dhidi ya mtoto Nasra Mvungi (4), kutaka
washitakiwa wahojiwe upya Polisi, ili mashitaka yanayowakabili yabadilishwe
baada ya kifo cha muathirika.
Mwendesha
Mashitaka na Wakili wa Serikali, Sundy Hyera, kwa kushirikiana na jopo la
mawakili wenzake akiwemo Mwendesha Mashitaka wa Polisi, Anganile Msiani,
aliwasilisha ombi hilo jana Mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mkoa wa Morogoro,
Mary Moyo.
Awali
washitakiwa hao, baba mzazi Nasra, Rashid Mvungi (47), mkazi wa Lukobe na mtumishi
wa Halmashauri ya Wilaya ya Morogoro na wanandoa Mariam Said (38) na mumewe
Mtonga Omar (30), wakazi wa Mtaa wa
Azimio, Kata ya Kiwanja cha Ndege, Manispaa ya Morogoro, walifikishwa
mahakamani hapo jana kujibu mashitaka yanayowakabili.
Wakili Hyera alidai
muathirika Nasra alifariki dunia Juni mosi mwaka huu, kwa hiyo ipo haja ya
kusikiliza ombi hilo, ili mahojiano hayo yafanyike upya na kuwezesha mabadiliko
ya mashitaka kwa washitakiwa wote watatu.
Pia aliomba
mahakama ipange tarehe nyingine ya karibu kwa mwezi huu, ili kesi hiyo
ifikishwe mahakamani hapo kutaja baada ya kufanyika mahojiano mapya na
washitakiwa Polisi.
Baada ya hoja
hizo, Hakimu Moyo aliridhia ombi hilo na kutoa ruhusa washitakiwa wote watatu
wafikishwe Polisi kuhojiwa na kuandikisha maelezo mengine, kwa kuwa
mtoto Nasra ameshafariki.
Hakimu huyo
aliiahirisha kesi hiyo hadi Juni 12, mwaka huu itakapofikishwa mahakamani hapo
kutajwa tena, pia aliamuru washitakiwa
waliopo rumade, waendelee kubakia rumande.
Awali wakazi wa
Manispaa ya Morogoro walifurika kwenye
viwanja vya mahakama hiyo, kusikiliza kesi inayowakabili washitakiwa hao.
Wananchi wa rika
mbalimbali walianza kumiminika mahakamani hapo kuanzia saa mbili asubuhi,
wakiwa na nia ya kuona hao wanaodaiwa
kumfanyia katili mtoto huyo, kwa kumfungia ndani ya boksi kwa miaka zaidi ya
mitatu.
Mshitakiwa wa
kwanza kufika mahakamani hapo saa nne asubuhi, alikuwa Mvungi ambaye yupo nje
kwa dhamana na wenzake waliletwa kwa gari la Polisi, lililokuwa pia na mahabusu wengine wanaokabiliwa na mashitaka
ya aina mbalimbali mahakamani hapo.
Washitakiwa hao
waliposhuka kwenye gari, wananchi waliokuwepo mahakamani hapo waliwazomea huku
wakitoa kauli za mashinikizo kwa mahakama, kwamba itoe adhabu kali ili iwe ni
fundisho kwa watu wengine wenye tabia kama hiyo.
Mkazi mmoja wa
mtaa wa Boma aliyekuwepo mahakamani hapo, aliamua kuangua kilio baada ya
kuwaona washitakiwa hao, huku akisema wamemkosea Mungu pamoja na kiumbe huyo
asiye na hatia hapa duniani.
Hali hiyo ya nje
ya Mahakama, ikiwemo pia heka heka za baadhi ya wananchi waliokuwa na simu
zenye
kamera kutaka kupinga picha washitakiwa, ilisababisha
mashauri mengine yasitishwe kwa muda, ili kupisha kesi hiyo kwanza.
Ndani ya chumba
cha wazi cha mahakama, kulifurika watu na kuwapa wakati ngumu askari Polisi
kuhakikisha ulinzi na amani wakati wote wa shauri hilo.
Baada ya kesi
kuahirishwa, watu hao walizingira gari dogo lililofika mahakamani hapo
kuwachukua washitakiwa na kuwapeleka Kituo Kikuu cha Polisi, ambapo waliamua
kusukuma kwa nyuma huku
wanawake wa
wanaume wakiendelea kuzomea washitakiwa hao.
No comments:
Post a Comment