Serikali inatarajiwa kutoa Sh
bilioni 40 kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za walimu katika halmashauri 80
nchini, sawa na Sh Sh milioni 500 kwa kila halmashauri.
Hayo yamesemwa na Waziri wa Fedha,
Saada Salum Mkuya aliposoma Hotuba ya Serikali kwa mwaka wa fedha wa
2014/15.
Alisema hayo mjini hapa juzi, wakati
akielezea matumizi ya fedha kwa makundi maalumu, hasa kuhusu ujenzi wa nyumba
za walimu.
Waziri huyo alisema serikali
inaendelea na utaratibu wa ujenzi wa nyumba za walimu kwa awamu.
Alisema katika mwaka wa fedha
2013/14, halmashauri 40 zilipewa kila moja Sh milioni 500 ili zianze ujenzi wa
nyumba za walimu. Kiasi kama hicho, kitatolewa katika halmashauri hizo kwa
mwaka 2014/15.
“Aidha, Sh milioni 500 zitatolewa
kwa halmashauri 80 zaidi, hivyo kufanya jumla ya halmashauri 120 kunufaika na
utaratibu huo, lengo likiwa ni kuzifikia halmashauri zote mwaka 2015/16”,
alisema.
Aliwahimiza viongozi wa Serikali
katika ngazi za mikoa, wilaya na kata, kusimamia kikamilifu fedha hizo ili
zitumike kwa malengo yaliyokusudiwa.
Kuhusu malipo ya madai ya walimu,
alisema serikali inaendelea kulipa madai ya walimu yaliyohakikiwa, ambapo
katika mwaka 2014/15 kiasi cha Sh bilioni 5.6 kimelipwa.
“Aidha, kwa mwaka 2014/15 madai ya
walimu ambayo yatakuwa yamehakikiwa, yataendelea kulipwa.
Aidha, Waziri huyo alisema uwiano wa
mwalimu kwa wanafunzi katika shule ya msingi, umeimarishwa kutoka 1:47 mwaka
2012 na kufikia 1:43 mwaka 2013, ikilinganishwa na lengo la uwiano wa 1:40.
Katika elimu ya sekondari, uwiano wa mwalimu kwa mwanafunzi ulifikia lengo la
MKUKUTA II la 1:28 mwaka 2013.
No comments:
Post a Comment