HUKUMU YA SHEKHE PONDA KUTOLEWA LEO...

Shekhe Ponda Issa Ponda.
Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu leo inatoa hukumu ya kesi ya uchochezi na wizi wa mali zenye thamani ya Sh milioni 59 inayomkabili Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu, Shekhe Issa Ponda na wafuasi wake 49.

Hukumu hiyo itatolewa na Hakimu Mkazi Victoria Nongwa baada ya kupitia majumuisho ya hoja na ushahidi wa  pande zote mbili uliowasilishwa kwa njia ya maandishi.
Shekhe Ponda na wenzake wanakabiliwa na mashitaka ya uchochezi, kuingia kwa nguvu na kujimilikisha isivyo halali kiwanja cha Chang’ombe Markazi kinachomilikiwa na kampuni ya Agritanza na wizi wa mali zenye thamani hiyo.
Washitakiwa hao walifikishwa mahakamani hapo Oktoba 18 mwaka jana na kukana mashitaka dhidi yao, hata hivyo Shekhe Ponda  na Swalehe Mukadam waliendelea kusota rumande baada ya Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) kuzuia dhamana yao.
Upande wa Mashitaka katika kesi hiyo uliiomba mahakama kuwaona washitakiwa hao wana kesi ya kujibu na kuwahukumu kulingana na sheria kwa kuwa wamethibitisha mashitaka dhidi yao kwa kiwango kinachotakiwa.
Machi 4 mwaka huu washitakiwa walipatikana na kesi ya kujibu na kuanza kujitetea ambapo walikuwa na mashahidi zaidi 50 wakiwemo washitakiwa wenyewe, ambao walikiri kukutwa eneo la tukio na kudai kuwa walikwenda kwa ajili ya ibada ya Itikafu ambayo hufanyika saa 9 usiku.
Wakili wa utetezi Juma Nassoro alidai kuwa polisi walifungua kesi ya jinai kwa jazba kwa kuwa walikuwa na uwezo wa kuwashawishi washitakiwa wakafungue kesi ya mgogoro wa ardhi  ambao ndiyo chanzo cha  kesi hiyo.
Washitakiwa wanadai kuwa kati ya Oktoba 12 na 16 mwaka jana katika eneo la Chang'ombe Markazi walipanga njama na kuingia isivyo halali katika kiwanja kinachomilikiwa na kampuni ya Agritanza na kuiba mali zenye thamani ya Sh milioni 59.
Katika mashitaka mengine, Shekhe Ponda na Mukadam wanadaiwa wakiwa viongozi wa jumuiya hiyo waliwashawishi wafuasi hao kutenda kosa hilo.

No comments: