Hali ya Burundi imezidi kuwa tete huku makundi mawili hasimu ya wanajeshi, yamekuwa yakipigana,
kila moja likitaka kutawala jiji la Bujumbura.
Mapigano hayo ni kati ya wanajeshi wanaomtii Rais Pierre
Nkurunziza, ambao wanapambana na wanajeshi wanaompinga, ambao wanamuunga mkono
mwanajeshi aliyetangaza mapinduzi, Meja
Jenerali Godefroid Niyombare.
Ofisa Mwandamizi wa Jeshi nchini humo, alisema wanajeshi
wanaomtii Rais Nkurunziza wamefanikiwa kudhibiti na kurejesha maeneo muhimu ya
jiji hilo chini ya utawala wa Serikali, ukiwamo uwanja wa ndege.
Hata hivyo, viongozi
wa wanajeshi wanaompinga Rais huyo, wameendelea kudai kuwa wameipindua Serikali
ya nchi hiyo.
Hali ya machafuko nchini humo, ilianza baada ya kiongozi
huyo kutangaza kuwa ana nia ya kuwania tena kipindi cha tatu cha urais, jambo
ambalo wapinzani nchini humo wamedai ni kinyume cha Katiba.
Kwa mujibu wa mashuhuda nchini humo, milio ya risasi na
mabomu imekuwa ikisikika usiku kucha kuanzia juzi katika mapigano baina ya
vikosi vinavyomtii Rais na vile vinavyotaka mapinduzi, lakini hadi sasa
haijafahamika nani aliyefanikiwa kulidhibiti jiji hilo.
“Hatujaweza kulala kutokana na hofu tuliyonayo, milio ya
milipuko na risasi imekuwa ikisikika kila sehemu, watu anaogopa kwa kweli,”
mmoja wa mashuhuda aliwaambia waandishi wa habari.
Kwa mujibu wa chanzo cha habari ndani ya kikosi kinachomtii
Rais Nkurunziza, jeshi hilo limeweza kurejesha maeneo muhimu chini ya Serikali
kama vile Ikulu, Redio na Televisheni ya Taifa na uwanja wa ndege.
Mitaa ya jiji hilo imejaa askari na polisi wanaomtii Rais na
hadi majira ya jioni uwanja wa ndege, ulifunguliwa tayari kwa kutoa huduma za
usafiri.
Hata hivyo, bado mapigano yanaendelea eneo ambapo televisheni na redio za taifa
zipo, huku vikosi vinavyotaka mapinduzi vikijaribu kuingia ndani ya vituo hivyo
vya habari.
Kila kikundi kinataka kudhibiti vituo hivyo vya utangazaji
wa taifa, kwa kuwa ndio vyombo vya habari pekee vyenye uwezo wa kusikika hadi
nje ya jiji hilo la Bujumbura.
Tayari Mkuu wa Majeshi na Rais Nkurunziza wametangaza na
kudai kuwa jaribio la kupindua nchi hiyo, limeshindikana.
Hata hivyo, kauli hizo zimekuwa zikipingwa na viongozi
wanaotaka mapinduzi nchini humo, na mmoja wao alisema kuwa wamefanikiwa
kudhibiti takribani mji wote wa Bujumbura.
Msemaji wa kundi hilo la waasi, Venon Ndabaneze, alisema
askari wanaotawanywa katika jiji hilo, wote wako upande unaotaka mapinduzi na
si wanaomtii Rais Nkurunziza.
Juzi, Meja Jenerali
Godefroid Niyombare, aliyekuwa Mkuu wa Usalama, alitangaza kumpindua Rais
Nkurunziza akiwa na baadhi ya viongozi wa Serikali, hali iliyozua shangwe
kwenye mitaa mbalimbali jijini humo. Niyombare alifukuzwa kazi na Rais
Nkurunzinza Februari mwaka huu.
Majengo ya kituo cha binafsi cha Televisheni Renaisance ya
Burundi, iliyotumiwa na Meja Jenerali Niyombare, yameripotiwa kuharibiwa vibaya
usiku wa kuamkia jana.
Kwa mujibu wa Mkurugenzi wa Kituo hicho, Innocent Muhozi,
moja ya ofisi zake ilichomwa moto usiku huo na kusababisha kila kilichokuwepo
ndani kuteketea.
Jenerali Niyombare, alitoa tangazo hilo, saa chache tu baada
ya Rais huyo kupanda ndege kwenda Dar es Salaam Tanzania kuhudhuria mkutano wa
wakuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, uliojadili suala hilo la Burundi.
Hata hivyo, iliripotiwa kuwa baada ya tangazo la kupinduliwa
kwake, Nkurunziza, alirejea Burundi bila kuhudhuria mkutano huo, lakini
alipofika Bujumbura alilazimika kurejea Dar es Salaam baada ya Uwanja wa Ndege
wa Bujumbura kufungwa.
Habari zilizopatikana
kutoka BBC baadaye jana jioni zilidai
wanajeshi watano walikuwa wameuawa, silaha nzito zilikuwa zikitumika, mirindimo ya risasi ilisikika kila kona na
waandamanaji walilazimika kujifungia ndani.
Ofisa Mwandamizi wa Usalama wa Taifa kutoka Ikulu ya Dar es
Salaam, alipozungumza na AFP, alikiri kuwa Rais Nkurunziza bado yupo Tanzania,
jijini Dar es Salaam, lakini haifahamiki ni sehemu gani alipo.
Suala sehemu alipo Rais Nkurunziza baada ya kufanyika jaribio
la kumpindua nchini kwake, limeendelea
kuwa tete baada ya Tanzania kusema haijui alipo.
Hatua hiyo imetokana na tetesi kuwa Rais huyo yupo nchini
baada ya kuhudhuria mazungumzo ya kutafuta amani kwa marais wa nchi za Afrika Mashariki jijini Dar es Salaam na
baadaye kutangazwa nchi hiyo kupinduliwa na kueleza kushindwa kurejea nchini
mwake.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard
Membe alisema hayo jana alipozungumza na waandishi wa habari mara baada ya
kufungua mkutano wa Baraza la Wafanyakazi wa wizara hiyo.
Awali , alipoulizwa alipo Rais huyo, alisema hawezi kujibu swali hilo lakini
baadaye alisema hajui huku akiondoka na kucheka.
Membe alisema baada ya tamko la viongozi wa nchi za Afrika
Mashariki, kulaani jaribio la kufanya mapinduzi
katika nchi hiyo zaidi ya hayo Baraza la Mawaziri lililokutana kwa siku mbili
Jumanne na Jumatano, litakutana tena
Jumatatu wiki ijayo na kufanya tathmini ya
hali halisi ya Burundi kwa siku tatu hizi mpaka Jumatatu.
“Kwa sasa sitaweza kuzungumza jambo jingine lolote kuanzia
sasa mpaka Jumatatu jioni baada ya kikao cha baraza la mawaziri wenzangu,
ambapo tutajua mambo ya kuzungumza.”
“Naomba kuwatahadharisha Watanzania kuwa hali ni tete
Burundi lolote unalosema wewe na kudhani dogo linaweza kugharimu maisha ya
mtu naomba mnielewe na mkae mkielewa
haya mengine tutazungumza siku hiyo ya Jumatatu,” alisisitiza.
Alisema wananchi wa
Burundi wako katika matatizo na vizuri
kuvuta subira, badala ya kuendelea kuzungumza,
kwani uhai wa mtu unaweza kuwa
matatani.
Membe alipoulizwa alipo Rais wa Burundi, kwani inasemekana
alirudi nchini Tanzania baada ya ndege
yake kushindwa kutua nchini kwake , alisema yeye hajui.
Alisema hali ya Burundi ni tete na sababu hiyo, walikutana
kutafuta ufumbuzi wa kudumu na wananchi waache kufanya ghasia na badala yake
watulie na kuchagua viongozi wao kwa amani.
Alisema imeelezwa kuwa jaribio la jana la baadhi ya askari
kutaka kuipindua Burundi, lililaaniwa na viongozi wote wa Afrika. Alisema
Afrika haitaki nchi yoyote, kwa sababu zozote,
kuhalalisha kuchukua madaraka kwa njia ya mtutu wa bunduki.
Wakati hali ya utawala nchini Burundi ikiwa tete , wakimbizi
wa nchi hiyo waliopo mkoani Kigoma,
wameanza kupatwa na majanga mengine baada ya kuripotiwa watu wanne kufa kwa
ugonjwa wa kipindupindu.
Mganga Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Leonald Subi alisema mjini
Kigoma kwamba watu wawili walikufa wakiwa tayari wanaumwa ugonjwa huo na
kufariki hapa nchini. Alisema watu wawili wengine, walipatwa na ugonjwa huo wakisubiri msaada wa
kibinadamu katika kijiji cha Kagunga wilaya Kigoma, mwambao wa Kaskazini wa Ziwa Tanganyika.
Subi alisema kuwa kwa sasa hali ya upatikaji wa huduma za
kibinadamu, ikiwemo chakula, maji, mahala pa kujihifadhi na huduma ya choo ni
mbaya sana kutoka na idadi kubwa ya wakimbizi hao kuwepo kijijini hapo kwa
kipindi kifupi na hivyo kijiji hicho kuzidiwa katika kuwapatia huduma watu hao.
Alisema kuwa Serikali ya Mkoa kwa kushirikiana na mashirika
mbalimbali ya ndani na nje, wanachukua hatua kukabiliana na hali hiyo, kwani
hali hiyo isipodhibitiwa maafa ya ugonjwa wa kipindupindu na magonjwa mengine,
yanaweza kuleta madhara makubwa.
“Hali kwa sasa ni mbaya kwa sababu watu wanajisaidia ziwani,
wanajisaidia popote na maji ya ziwani ambayo wakimbizi hao wamejisaidia
wamekuwa pia wakiyatumia kwa kunywa na kupikia bila maji hayo kutibiwa kwa kuua
vijidudu,” alisema Dk Subi.
Wakati hali ikiwa hivyo,
Shirika la Msalaba Mwekundu (Red Cross)
nchini limeanza kuchukua hatua kukabiliana na wimbi kubwa la wakimbizi
waliopo kijiji cha Kagunga kwa kupeleka huduma mbalimbali za kijamii.
Mratibu wa Shirika la Red Cross mkoani Kigoma, Jane Chagie
akizungumza katika semina kuhusu maafa kwa makundi maalum yanayohusika na
masuala ya uokoaji, alisema kuwa tayari
timu ya watendaji wa Red Cross, imeshaelekea kijijini Kagunga wakiwa na mahema
kwa ajili ya wakimbizi hao kujihifadhi, dawa ya kutibu maji na watu
wanaoshughulikia uchimbaji vyoo.
Chagie alisema kuwa timu ya ushauri ya afya ya Red Cross,
Halmashauri ya wilaya na mkoa,
wameshaenda eneo la tukio kwa ajili ya kukabiliana na magonjwa ya mlipuko
wakiwa na madawa mbalimbali.
Akizungumzia suala la uchimbaji vyoo, alisema kuwa
wamekabiliwa na tatizo kubwa la mahali pa kuchimba vyoo, kutokana na sehemu
kubwa ya eneo kuwa la Milima yenye mawe huku wakimbizi wakiwa wametapakaa eneo
kubwa la kijiji.
Kijiji cha Kagunga kina wakimbizi zaidi ya 30,000 wanaoomba
hifadhi ya ukimbizi nchini kutoka
Burundi wakati kijiji hicho kikiwa na idadi ya watu 17,000. Meli ya Mv.
Liemba imeonekana kulemewa na idadi kubwa ya wakimbizi hao. Meli hiyo ina uwezo wa kubeba watu 600 kwa safari moja.
No comments:
Post a Comment