Watanzania wanaoishi Afrika Kusini, wako hatarini kutokana
na vurugu zinazofanywa na wenyeji wa nchi hiyo, dhidi ya wananchi wengine wa
asili ya Afrika wanaoishi nchini humo.
Akizungumza na mwandishi jana, Msemaji wa Wizara ya Mambo ya
Nje ya Nchi, Mkumbwa Ally, alisema Mtanzania mmoja amechomewa duka lake, huku
wengine 15 wakiwa katika kambi maalumu, wakisubiri msaada wa kurejeshwa
nyumbani.
Kwa mujibu wa Mkumbwa, Ubalozi wa Tanzania unaendelea
kukusanya takwimu za Watanzania wanaoishi nchini humo na Serikali ya nchi hiyo
imeandaa kambi maalumu za kuhifadhi wageni wakiwemo Watanzania, ambao wamekuwa
wakifanyiwa fujo na watu wa nchi hiyo.
“Hao Watanzania 15 ni wale ambao wako tayari kurudi
nyumbani, sasa hivi Serikali inashughulikia utaratibu wa kuwarejesha nyumbani.
“Kuna dalili idadi ya walio tayari kurudi nyumbani
ikaongezeka maana inasemekana vurugu, mbali na kufanyika katika mji wa Durban,
sasa zinatarajiwa kuendelea katika jiji la Johannesburg,” alisema Mkumbwa.
Alisema hali hiyo inatia wasiwasi na Tanzania inatarajia
Serikali ya nchi hiyo, itachukua hatua zinazotakiwa kuhakikisha usalama kwa
Watanzania na watu wa nchi zingine, wakati Serikali ya Tanzania ikijiandaa
kuwarejesha nyumbani wote watakaokuwa tayari.
Tayari taarifa kutoka katika mitandao mbalimbali ya habari,
zimeonesha kuwa zaidi ya wageni 2,000 wenye asili ya Afrika wanaoishi nchini
humo, wamewekewa kambi katika Uwanja wa Mpira wa Rydalvale, kwa ajili ya
usalama wao.
Mmoja wa maofisa kutoka Ofisi ya Meya wa Durban, Sipho
Mthethwa, amenukuliwa akisema wageni wengi wamepoteza mali zao na wana hasira
na kazi aliyonayo ni kuwashawishi wapunguze hasira na anafanya hivyo kwa
utaratibu.
Kwa sasa wageni hao wako katika makambi ambako kumewekwa
maturubai huku wakihudumiwa na mashirika ya misaada.
Mthethwa alisema zaidi ya mabasi 24 yanatumika kusafirisha
wageni hao kwenda katika kambi hizo, lakini tatizo wengi wamekuwa wakitaka
kubeba mali zao na kukaa nazo katika makambi, huku familia zikitaka kuwa
pamoja.
Alisema hali hiyo inamuwia vigumu, kwa kuwa taratibu za
kambi za dharura, wanawake lazima wakae eneo tofauti na wanaume na mali zao
zitafuata baada ya waathirika hao kupata eneo na kutulia.
No comments:
Post a Comment