Mahakama ya
Hakimu Mkazi Dodoma Mjini jana ilimwachia kwa dhamana Mwenyekiti wa Jumuiya ya
Wafanyabiashara nchini, Johnson Minja (34), huku taarifa kutoka mikoa
mbalimbali zikisema wafanyabiashara nao wamelegeza mgomo wao na kufungua
maduka.
Minja
(pichani) alifutiwa dhamana kwa kile kilichodaiwa kuendelea kuhamasisha wafanyabiashara
wasilipe kodi kwa serikali wakati akiwa nje kwa dhamana.
Kuachiwa kwa
mtuhumiwa huyo kulizusha shangwe kwa mamia ya wafanyabiashara kutoka
mikoa mbalimbali nchini ambao walifurika mahakamani hapo kusikiliza kesi ya
kiongozi wao huku ulinzi ukiwa umeimarishwa .
Kutokana na
mwenyekiti huyo kuachiwa idadi kubwa ya wafanyabiashara ambao walizuiwa kwenye
lango kuu la kuingia mahakamani walitawanywa na polisi huku wengine wakikataa
kuondoka mpaka wamuone Minja huku wakili upande wa utetezi Godfrey Wasonga
akiwatangazia mara kwa mara wananchi hao kuondoka eneo la mahakama kwani
mwenyekiti huyo hatazungumza chochote na wafanyabiashara.
Uamuzi wa
kumuachia kwa dhamana Minja ulitolewa na Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya,
Rhoda Ngimilanga baada ya kusikiliza hoja za upande wa mashtaka na upande wa
utetezi.
Wakili wa
Serikali, Rose Shio alisema mara ya mwisho mshtakiwa alifutiwa dhamana kwa
sababu ya kukiuka masharti aliyowekewa na mahakama Januari 28, mwaka huu,
wakati alipofikishwa mahakamani kwa mara ya kwanza na kushtakiwa kwa mashtaka
ya kuwashawishi wafanyabiashara kugomea kutumia mashine za EFDs na wasilipe
kodi kwa serikali.
Alidai
wanakubali dhamana ni haki ya mshtakiwa lakini inatakiwa kwenda pamoja na
masharti kwani kulikuwa na taarifa kwenye hoteli aliyofikia aliitisha mkutano
na ajenda zilizokuwa zikijadiliwa ni mgomo wa matumizi wa mashine za EFD’s.
“Ilikuwa ni
sahihi kwa Minja kufutiwa dhamana” alidai wakili wa serikali
Akijibu hoja
hiyo, Wakili upande wa utetezi, Godfrey Wasonga alisema anapinga hoja za wakili
wa serikali kwani dhamana ni haki ya mshtakiwa kikatiba kwani inatoa haki ya
mtu kupata dhamana ni marufuku kwa mtu
aliyeshtakiwa kwa kosa kuendelea kumuweka rumande Minja ni kama tayari
ameshatiwa hatiani wakati mahakama bado haijaamua kama ana hatia au la.
“Tukimwachia
Minja aendelee kukaa Isanga tutakuwa tumevuruga katiba ambayo ni sheria mama
kwani hajawahi kuvunja masharti ya dhamana” alisema
Alidai Minja
hakuwahi kufanya mkutano na mahakama isiendelee kusikiliza umbea kutoka kwa
wakili wa serikali, kwani kama aliitisha mkutano angekamatwa na kufikishwa
kunakohusika na si mahakama kuamini maelezo ya upande wa mashtaka ambayo hayana
ushahidi wowote.
Akitoa uamuzi
wa mahakama, hakimu Ngimilanga alisema amesikiliza maelezo ya pande zote mbili
na kitu kikubwa upande wa mashtaka unadai mshtakiwa alivunja masharti ya
dhamana kwa kufanya mkutano na kusababisha kuvunjika kwa amani.
Kutokana na
hilo hakimu Ngimilanga alisema mshitakiwa atakuwa nje kwa dhamana hadi
Aprili 9, mwaka huu kesi yake itakapoanza kusikilizwa maelezo ya awali.
Jijini Dar es Salaam, hali katika maduka ya Kariakoo yalirejea
katika hali ya kawaida, kwani yalifunguliwa nyakati za mchana baada ya mahakama
kumwachia kwa dhamana Minja. Hali kama hiyo iliripotiwa kutokea katika mikoa
mbalimbali nchini.
No comments:
Post a Comment