MAJALIWA YA SHEKHE PONDA JULAI, HAKIMU WAKE ANALEA


Majaliwa ya kesi inayomkabili Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu  Nchini , Shehe Ponda Issa Ponda, ambayo  ipo kwenye hatua ya utetezi itapatikana miezi mitatu ijayo.

Hiyo inatokana na hakimu anayesikiliza kesi hiyo Hakimu Mwandamizi wa Mahakama  hiyo, Mary Moyo kuanza rasmi likizo  ya uzazi ya miezi mitatu na hivyo Hakimu Mfawidhi wa wilaya ya Morogoro Maua Hamduni kuiahirisha  hadi Aprili 16, mwaka huu ambapo itatajwa tena mahakamani hapo.
Mtuhumiwa  alifikishwa mahakamani hapo pasipo mawakili wake wa utetezi , ambapo kwa jana  upande wa mashtaka uliongozwa  na Wakili wa Serikali, Sunday Hyera. 
Kabla ya kuanza kutoa maelezo ya kuahirishwa kwa kesi,  Hakimu huyo  alimuuliza Shehe Ponda juu ya kutoonekana kwa mawakili wake mahakamani hapo na endapo  anazo taarifa zao , naye  alijibu kuwa hakuwa na taarifa zao.
Kesi hiyo kwa sasa ipo katika  hatua ya upande wa mashtaka kujibu hoja zilizotolewa na upande wa utetezi baada ya kufungwa kwa ushahidi ambazo zilidai kuwa Shehe Ponda hakuwa na kesi ya kujibu.
Kutokana na hatua ilipofikiwa , Hakimu huyo, alisema  pamoja na  Hakimu Moyo anayeisikiliza kesi hiyo tangu mwanzo kuwa katika mapumziko ya likizo ya uzazi ya miezi mitatu, kisheria  haiwezekani shauri hilo ikabadilishiwa hakimu mwingine bali itaendelezwa naye baada ya kumaliza likizo ya uzazi.
Kwa mujibu wa Hakimu huyo, kwa hivi sasa kesi ya Shehe Ponda itaendelea kutajwa mahakamani hapo hadi hakimu wake atakapoanza kazi baada ya kumaliza likizo hiyo .
Kufuatia maamuzi ya hakimu huyo, Shehe Ponda alinyosha kidole mbele ya hakimu huyo na kupewa nafasi ya kuzungumza ambapo alimwambia hakimu kuwa kwa vile kesi yake itakuwa ikitajwa pekee, anaomba siku ya kufikishwa mahakamani abakie magereza ili kuondoa usumbufu.
Shehe Ponda alidai kuwa, ingekuwa ni jambo nzuri siku ya kutajwa kwa kesi yake iitwe fomu yake na kugongwa muhuri wa Mahakama , wakati akiwa gerezani .
Hata hivyo hakimu huyo alimjibu Shehe Ponda kuwa, kisheria njia hiyo hairuhusiwi , kwani kinachozingatiwa ni kwa mtuhumiwa kufikishwa mahakamani na hakimu kumwona kwa macho yake na kuiahirisha kwa msingi huo na si vinginevyo.
Hakimu huyo alimuuliza Sheikh Ponda kuwa yenye haoni kuwa ni fursa kuja uraiani kuonana  na kusalimiana na ndugu zake na kujibiwa na Sheikh Ponda kuwa, yeye amezoea kukaa gerezani hivyo haoni sababu hizo.
Tofauti na siku nyingine inaposikilizwa kesi hiyo ambapo wafuasi wake hufurika nje ya uzio wa mahakama hiyo , jana, walijitokeza wachache hawakuzidi  watu 10 ambao hawakuweza  kufanya jambo lolote  la kusoma Quraan na kufanya maombi .
Shekhe Ponda alifunguliwa kesi namba 128/2013 katika Mahakama ya Hakimu Mkazi mkoa wa Morogoro akikabiliwa na mashtaka matatu ambayo aliyatenda Augosti 10, mwaka 2013 katika eneo la Kiwanja cha Ndege Manispaa ya Morogoro na alifikishwa mahakamani hapo kwa mara ya kwanza Agosti 19 mwaka 2013.

No comments: