Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imesogeza
mbele kwa muda usiojulikana shughuli ya upigaji Kura ya Maoni ya Katiba
Inayopendekezwa.
Awali, Watanzania walikuwa waipigie kura
Katiba hiyo Aprili 30, mwaka huu.
Lakini jana katika mkutano wake na waandishi
wa habari, Mwenyekiti wa NEC, Jaji mstaafu Damian Lubuva alisema hatua hiyo
imetokana na kutokamilika kwa uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura.
“Kwa vile kazi ya uboreshaji wa Daftari la
Kudumu la Mpigakura ni ya msingi kabla ya kupiga kura, na jukumu la kwanza la
Tume ni kukamilisha kazi ya kuboresha daftari. Mengine yanafuata baada ya
hapo,”alisema.
Aliongeza: “ Kwa vile zoezi la Uboreshaji wa
Daftari la Kudumu la Wapiga Kura halijakamilika, Tume haitaweza kuendelea na
zoezi la kupiga kura ya maoni kama ilivyotangazwa awali.”
Awali, ilitangazwa baada ya kukamilika
uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura kwa mfumo mpya wa BVR nchini
nzima, upigaji kura ungefanyika mwishoni mwa mwezi huu.
Tume ilianza
Kuboresha Daftari la Kudumu la Wapiga Kura kwa kutumia mfumo wa Biometrick
Voters Registration (BVR) baada ya kuzinduliwa na Waziri Mkuu Mizengo Pinda
katika Halmashauri ya Mji wa Makambako mkoani Njombe, Februari 24 mwaka huu.
Alisema muda mwafaka ukifika, Tume itatangaza
tarehe mpya ya Kupiga Kura ya Maoni baada ya kushauriana na Tume ya Uchaguzi ya
Zanzibar (ZEC).
Akizungumzia vifaa, Jaji Lubuva alisema kuwa
serikali imeshalipa dola za Marekani milioni 72 (sawa na Sh bilioni 122.4) kwa
ajili ya vifaa hivyo na kuwa vifaa 7,750 vilivyosalia, vitaletwa nchini kwa
awamu.
Katika mchakato wa kuboresha Daftari la
Kudumu la Wapiga Kura kwa mfumo mpya wa
BVR, Tume ilihitaji vifaa 8,000 na ilianza na vifaa 250
“Nikiri kulikuwepo na ucheleweshaji wa kulipia
vifaa vya kuandikisha wapiga kura, lakini sasa Serikali imelipia vyote, na
vitaletwa kutoka China kwa awamu, siku chache zijazo tutapokea vifaa 248 na
baadaye vifaa 1,600 na vitafika kwa awamu mpaka idadi itakapofikiwa,” alisema.
Alisema kutokana na kuanza kuingia kwa vifaa
hivyo, Tume imejipanga kuhakikisha inakamilisha Uboreshaji wa Daftari la Kudumu
la Wapiga Kura kwa ukamilifu ifikapo Julai mwaka huu.
Aidha, Lubuva alisema kazi ya uandikishaji
wapigakura kwa mkoa wa Njombe, unatarajia kukamilika Aprili 18 mwaka huu na
kuwa baada ya hapo Tume itakwenda Kuboresha Daftari la Kudumu la Wapiga Kura
katika mikoa ya Ruvuma, Iringa, Mtwara na Lindi.
“Kama ilivyokuwa Njombe, Tume inatarajia mikoa
inayofuata itawahamasisha wananchi kujitokeza kwa wingi katika maeneo yao na
kujiandikisha kwa tarehe zitakazotangazwa kwenye mikoa husika,”
Hata hivyo, Lubuva alisema kumekuwapo na
malalamiko kutoka kwa wadau, wanaoona kuwapo kwa foleni ndefu kuwa ni dalili ya
ubovu wa mfumo wa BVR, lakini ukweli hali hiyo ndiyo kielelezo cha kukua na
kukolea kwa demokrasia nchini.
Licha ya makundi kadhaa kujaribu kuipinga
Katiba hiyo Inayopendekezwa, wakiwemo baadhi ya viongozi wa dini na vyama vya
siasa vya upinzani, imeelezwa kuwa zaidi ya nusu ya Watanzania wataipigia Kura
ya Ndiyo Katiba Inayopendekezwa.
Aidha, imeelezwa mwito wa vyama vinavyounda
umoja wa Ukawa wa kususa kura ya maoni haujawavutia wananchi wengi, hivyo wengi
hawauungi mkono.
Hayo yamo katika taarifa ya matokeo ya utafiti
uliofanywa na Taasisi ya Twaweza kati ya Januari 27 na Februari 17 mwaka huu na
kutolewa jana kupitia muhtasari wenye jina la “Kuelekea Kura ya Maoni ya
Watanzania kuhusu Katiba Inayopendekezwa.”
Kwa mujibu wa taarifa ya utafiti huo
uliosambazwa kwa vyombo vya habari na Mshauri wa Mawasiliano wa Twaweza, Risha
Chande, muhtasari huu umetokana na takwimu za Sauti za Wananchi, utafiti wa
kwanza barani Afrika wenye uwakilishi wa kitaifa unaofanyika kwa njia ya simu
za mkononi.
Muhtasari huu unajumuisha maoni ya wananchi wa
Tanzania Bara pekee juu ya Katiba Inayopendekezwa.
“Jumla ya wahojiwa 1,399 walipigiwa simu kati
ya Januari 27 na Februari 17, 2015. Matokeo mengine yanatokana na duru la 5 la
Sauti za Wananchi (iliyowahoji watu 1,708 kati ya Julai 16 na Julai 30, 2013)
na duru la 14 la Sauti za Wananchi
(iliyowahoji watu 1,550 kati ya Februari 12 na Machi 4, 2014).
Kuhusu Ukawa kususa vikao vya Bunge la Katiba
na ushawishi wake kwa wananchi kususa kura ya maoni, utafiti huo umeonesha:
“Kati ya wananchi waliosikia minong’ono juu ya Ukawa kususa vikao vya Bunge la
Katiba, asilimia 66 wanapinga hatua hiyo. Asilimia 68 wanapinga ushawishi kwa
wananchi kususa kura ya maoni na robo tatu (asilimia 75) ya wananchi wanasema
hawatasusa kura ya maoni.”
No comments:
Post a Comment