Mshituko wa matukio ya mfululizo ya
ajali, umeendelea kugubika nchi, baada ya watu 20 kupoteza maisha katika ajali
ya basi dogo aina ya Toyota Hiace, iliyotokea jana wilayani Rungwe mkoani
Mbeya.
Ajali hiyo ambayo taarifa na picha
zake zilisambaa kwa kasi katika mitandao ya kijamii, imesababisha taharuki
kutokana na ukaribu wake na matukio mengine ya ajali yaliyotokea wiki hii.
Tangu Jumapili iliyopita mpaka
jana, siku zisizozidi sita kumetokea ajali kubwa tatu zilizohusisha mabasi ya
abiria na kuteketeza maisha ya watu 40.
Mbali na ajali hizo, wiki hii
Kamanda wa Jeshi la Polisi Kikosi cha Usalama Barabarani, Mohamed Mpinga alitoa
takwimu zilizosababisha huzuni kwa Watanzania, kwamba kati ya Januari mosi na Aprili
12 sawa na siku 102, watu 969 walipoteza maisha katika ajali za barabarani.
Jumatano wiki hii, basi la Air
Jordan lililokuwa likitokea mkoani Mwanza kwenda Arusha, lilipata ajali na
kusababisha kifo cha mtu mmoja na majeruhi 20.
Ajali hiyo ilitokea wakati
Watanzania wakiwa na kumbukumbu ya ajali iliyotokea Jumapili ya wiki jana,
ambapo watu 19 waliteketea kwa moto, baada ya basi la Kampuni ya Nganga Express
na lori aina ya Fuso kugongana uso kwa uso na kuwaka moto katika eneo la Iyovi,
Milima ya Udzungwa, mkoani Morogoro.
Akizungumza na mwandishi jana,
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mbeya, Mohamed Msangi, alisema ajali hiyo mpya
imetokea katika eneo la Ilongo ambalo limebatizwa jina la Uwanja wa Ndege
karibu na Kiwira, ambapo watu 18 walipoteza maisha papo hapo.
“Watu wanne waliojeruhiwa, mmoja
alikuwa katika hali mbaya na kwa bahati mbaya alifia njiani wakati akipelekwa
Hospitali ya Wilaya ya Rungwe kwa matibabu,” alisema Kamanda Msangi.
Kamanda Msangi alisema chanzo cha
ajali hiyo ni mwendo kasi na dereva kutokuwa makini katika uendeshaji wake.
Taarifa zilizotufikia baadae,
zilieleza kuwa abiria mwingine aliyekuwa akipatiwa matibabu, alifariki akiwa
hospitalini.
Mashuhuda wa ajali hiyo
waliozungumza na gazeti hili, pia walidai kuwa chanzo cha ajali ni mwendokasi
uliosababisha dereva ashindwe kumudu gari hilo katika mteremko wenye kona,
akajikuta gari likimshinda na kutumbukia katika Mto Kiwira.
Kwa mujibu wa madai ya mashuhuda
hao, kuna uwezekano dereva huyo alikuwa akikimbizwa na baadhi ya madereva wa mabasi
aina ya Toyota Coaster, yanayofanya safari zake kati ya Mbeya, Tukuyu na Kyela.
Inadaiwa kuwa madereva wa mabasi
hayo aina ya Toyota Coaster, hawakutaka
mabasi madogo aina ya Toyota Hiace kubeba abiria kutokana na wao kuwa kwenye
mgomo.
Kwa mujibu wa mashuhuda hao, askari
wa Jeshi la Polisi walifika mapema eneo la tukio na kusaidiana na wananchi
kuokoa majeruhi na miili ya marehemu.
No comments:
Post a Comment