Mahojiano baina ya Jeshi la Polisi na Askofu
Mkuu wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Josephat Gwajima yaliyokuwa yanatarajiwa
kuendelea jana, ikiwa ni siku mbili baada ya kuachiwa kwa dhamana na jeshi
hilo, jana yalikwama kuendelea kutokana na kile kilichoelezwa kutoimarika kwa
afya ya askofu huyo, na sasa yatafanyika Alhamisi ijayo.
Gwajima alidaiwa kuzimia wakati akihojiwa na
makachero wa Polisi waliokuwa wanamhoji, alipojisalimisha alasiri ya Ijumaa
iliyopita baada ya kutakiwa kufanya hivyo, kutokana na kufunguliwa jalada la
malalamiko ya kumkashifu Askofu Mkuu wa Kanisa Katoliki Jimbo Kuu la Dar es
Salaam, Mwadhama Kardinali Polycarp Pengo.
Kutokana na hali hiyo iliyotokea majira ya saa
tatu usiku wakati akiendelea na mahojiano yaliyoanzia alasiri, alikimbizwa
Hospitali ya TMJ, Mikocheni akiwa chini ya ulinzi wa Polisi hadi aliporuhusiwa
kutoka Jumanne wiki hii na baadaye kuachiwa kwa dhamana.
Mwanasheria wa Askofu Gwajima, John Mallya
alithibitisha kuahirishwa kwa mahojiano kati ya mteja wake na Polisi, akisema
mapema jana asubuhi aliripoti Kikuo Kikuu cha Polisi Dar es Salaam kama
alivyotakiwa kuripoti kituoni hapo kwa ajili ya mahojiano.
Hata hivyo, alisema hakuweza kuhojiwa kutokana
na kile kinachoelezwa kuwa afya ya mteja wake haijaimarika vizuri na hivyo
wamepangiwa kurudi tena kituoni hapo Aprili 9 mwaka huu, yaani Alhamisi ijayo
kwa ajili ya mahojiano.
“Mteja wangu alifika kituoni leo (jana)
asubuhi kwa ajili ya mahojiano na pia kuripoti kama ilivyoagizwa siku
alipopatiwa dhamana, hata hivyo afya yake bado haijaimarika na hivyo
imewalazimu polisi wampatie muda zaidi hadi Aprili 9 atakaporudi tena kwa ajili
ya mahojiano,” alisema Mallya.
Hata hivyo, Mallya alisema hali ya afya ya
Gwajima imeanza kuimarika na kadri siku zinavyozidi kwenda, atakuwa na nguvu na
ataendelea na kazi zake kama kawaida.
Mtumishi huyo alipatiwa dhamana katika Kituo
cha Polisi Oysterbay na kutakiwa kuripoti Kituo Kikuu cha Kati kwa ajili ya
mahojiano zaidi na kusubiri uchunguzi wa kesi yake ukamilike.
Akiwa hospitalini TMJ, wafuasi wake 15
wakiwemo wachungaji sita, mhadhiri mmoja wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM)
na mwanafunzi wa udaktari katika Chuo Kikuu cha Kimataifa cha Matibabu na
Teknolojia (IMTU) walikamatwa na Jeshi la Polisi kwa kile kilichoelezwa kula
njama za kutaka kumtorosha askofu huyo bilionea anayemiliki utitiri wa magari
likiwemo aina ya Hummer lenye thamani ya zaidi ya Sh milioni 250, nyumba ya
ghorofa ya kifahari, helikopta na kadhalika.
Kukamatwa kwa wafuasi hao ambao nao wamefunguliwa
mashitaka, kulithibitishwa na Kamishna wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es
Salaam, Suleiman Kova.
Katika taarifa yake, alisema watu hao
wanatuhumiwa kwa makosa ya kula njama pamoja na kujaribu kumtorosha Askofu
Gwajima aliyekuwa amelazwa katika Hospitali ya TMJ kwa matibabu.
Alisema siku ya tukio (usiku wa kuamkia
Jumapili iliyopita), saa tisa na nusu usiku, watu 15 walifika hospitalini hapo
kwa lengo la kumuona mgonjwa huyo.
“Askari ambao wapo katika lindo hilo
waliwatilia mashaka watu hao hivyo waliwakatalia kuingia. Na hapo walijaribu
kutumia nguvu, lakini walikamatwa,” alisema.
Kova alisema baada ya kuwapekua, watu hao
walikutwa na bengi lenye bastola aina ya BERRETA yenye namba CAT5802 ikiwa na
risasi tatu, risasi 17 za Short gun na vitabu viwili vya hundi.
Alisema begi hilo pia lilikuwa na hati ya
kusafiria yenye jina la Gwajima Joseph Mathias yenye namba AB 544809, kitabu
cha hundi cha Benki ya Equity, nyaraka mbalimbali za kampuni ya PUMA, chaja ya
simu na tablets, suti mbili na nguo za ndani.
Aliwataja waliokamatwa ni Chitama Mwakibambo
(32), fundi seremala mkazi wa Gongo la Mboto, mchungaji Edwin Audex (24) mkazi
wa Kawe Maringo, Adam Mwaselele(29), mhandisi na mkazi wa Kawe Maringo,
Frederick Fusi (25) mkazi wa Mbezi Beach.
Wengine mwanafunzi wa chuo cha IMTU, Frank
Minja (24) mkazi wa Mbezi Beach, Emmanuel Ngwela (28) mkazi wa Keko Juu ambaye
ni mlinzi shirikishi, Geofrey William (30), Mhadhiri UDSM mkazi wa Survey Chuo
Kikuu, Mchungaji Mathew Nyangusi (62) mkazi wa Mtoni Kijichi, Mchungaji Boniface
Nyakyoma (30) mkazi wa Kitunda.
Pia wametajwa Geofrey Andrew (31), dereva
mkazi wa Kimara Baruti, Mchungaji David Mgongolo (24) mkazi wa Ubungo Makoka,
Mfanyabiashara George Msava (45) mkazi wa Ilala Boma, Mchungaji Nicholaus
Patrick (60) mkazi wa Mbagala Mission, George Kiwia (37) ambaye ni dalali wa
magari na mkazi wa Tandale Uzuri na Mchungaji Yekonia Bihagaze (39) mkazi wa
Kimara Stop Over.
Kova alisema upelelezi wa shauri hilo
unaendelea kwa madhumuni ya kubaini sababu za njama hizo sambamba na kujua
mbinu zote zilizotumika kutaka kufanikisha jaribio la kumtorosha Askofu
Gwajima.
No comments:
Post a Comment