Hatimaye Askofu wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Josephat
Gwajima (45), amepanda katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, akikabiliwa na
mashitaka mawili, ikiwemo la kutumia lugha ya matusi dhidi ya Askofu Mkuu wa
Jimbo Kuu la Dar es Salaam la Kanisa Katoliki, Mwadhama Polycarp Kardinali
Pengo.
Mbali na Gwajima, washitakiwa wengine ni Askofu msaidizi wa
Kanisa hilo, Yekonia Behagaze (39), Geofrey Mzava (31) ambaye hakuwepo
mahakamani hapo na George Milulu (43) mkazi wa Kimara Baruti.
Kesi hiyo ambayo ilianza kutajwa saa 9:30 alasiri hadi saa
11 jioni, ilisikilizwa mbele ya Hakimu Wilfred Dyansobera, ambapo mawakili wa
Serikali; Wakili Mwandamizi Joseph Maugo, akisaidiwa na Shadrack Kimaro na
Tumaini Kweka, walisoma mashitaka dhidi
ya washitakiwa.
Katika mashitaka ya kwanza yanayomkabili Gwajima,
Wakili Kweka alidai kuwa katika siku
isiyofahamika kati ya Machi 16 na 25 mwaka huu, maeneo ya Tanganyika Packers,
kiongozi huyo alitumia lugha ya matusi dhidi ya Kardinali Pengo, akieleza kuwa
ni mtoto, hana akili katika namna ambayo angeweza kusababisha uvunjifu wa
amani.
Mshitakiwa alikana shitaka hilo ambapo suala la dhamana kwa
mshitakiwa lilileta mabishano ya kisheria kati ya Wakili wa Serikali Maugo na
Wakili wa Gwajima, Peter Kibatala ambapo
upande wa mashitaka ulitaka mshitakiwa awe na wadhamini watakaopatikana wakati
mshitakiwa asipokuwepo.
Hata hivyo, Kibatala alidai kuwa mteja wake kwa kuzingatia
cheo alicho nacho ni mwaminifu na aliiomba mahakama hiyo, ajidhamini mwenyewe
kutokana na muda ambao walipelekwa mahakamani hapo.
Kupitia mabishano hayo, Hakimu Dyansobera alikubaliana na
ombi hilo na kumtaka Gwajima asaini hati ya Sh milioni moja.
Akisoma mashitaka ya pili, Wakili Kimaro alidai kuwa Gwajima
anakabiliwa na mashitaka ya kushindwa kuhifadhi silaha, ambayo ni kinyume na
Sheria ya Silaha za Moto.
Alidai kuwa kati ya Machi 27 na 29 mwaka huu, maeneo ya
Hospitali ya TMJ iliyopo Mikocheni A wilayani Kinondoni, akiwa amepewa leseni
ya silaha hiyo yenye namba za usajili CAT 5802 na risasi tatu za bastola na
risasi 17 za bunduki, aliziacha kwa watu wasio husika bila ya ruhusa.
Kimaro alidai katika siku hiyo washitakiwa Behagaze, Milulu
na Mzava walikutwa na bastola bila ya ruhusa na kinyume na taratibu katika
Hospitali ya TMJ iliyopo Mikocheni A, Kinondoni.
Mshitakiwa wa tatu alidaiwa kuwa siku hiyo hiyo katika
Hospitali ya TMJ, alikutwa na risasi tatu za bastola na 17 za bunduki (shotgun)
bila ya kuwa na ruhusa. Mshitakiwa wa nne hakusomewa mashitaka kwa kuwa
hakuwepo mahakamani hapo.
Washitakiwa wote walikana mashitaka na kwamba upande wa
mashitaka ulidai kuwa upelelezi wa shauri hilo bado unaendelea.
Wakili Kibatala aliomba dhamana kwa washitakiwa hao kwamba
wajidhamini wenyewe, lakini Hakimu Dyansobera aliwataka kila mmoja awe na
mdhamini mmoja atakayetambulika na Mahakama, atakayesaini dhamana ya Sh milioni
moja, ambapo washitakiwa wote walitimiza masharti.
Akizungumza nje ya mahakama, Kibatala alidai kuwa mteja wake
alitakiwa kujisalimisha Machi 27 mwaka huu na
alifanya hivyo, lakini mahojiano hayo hayakukamilika, kutokana na
matatizo ya kiafya aliyoyapata.
Pia, alidai kuwa mara ya pili aliamriwa apeleke nyaraka 10
za umiliki wa mali zake, ikiwemo helikopta, nyumba na kanisa, ambapo aliamua
kuandika barua kuomba vifungu vya sheria, ambavyo alidai kuwa mpaka leo
hajapata.
‘’Leo asubuhi nilipigiwa simu na Gwajima akinieleza kuwa
amezingirwa na Polisi walioongozwa na Mkuu wa Upelelezi Mkoa wa Kinondoni.
Nilipofika nilifanya mazungumzo na Polisi, nikawaambia hakuna sababu ya kuja
wengi hivyo, mteja wangu atakuja mwenyewe,’’ alidai.
Baadhi wa waumini waliokuwepo katika viwanja vya mahakama
hiyo, walikuwa wakishangilia na kupiga kelele baada ya ‘baba’ yao huyo wa
kiroho kuachiwa kwa dhamana.
Gwajima aliondoka mahakamani hapo saa 12:00 jioni kwenye
gari namba T 631 AHD aina ya Land Cruiser, huku ikifuatiwa na msafara wa magari
ya waumini wake waliokuwa wamepakatana katika magari hayo.
Awali, nyumba ya Gwajima
ilizingirwa na Polisi kwa zaidi ya saa saba kuanzia saa 12 alfajiri ya jana
hadi saa sita mchana, kwa madai ya kutaka kumkamata, kutokana na kutotokea
Polisi kama alivyotakiwa hapo juzi.
Polisi wakiwa na magari ya aina
tofauti, walionekana kuzingira nyumba ya askofu huyo iliyopo maeneo ya Tegeta
Salasala katika Kata ya Wazo eneo la Kilimahewa, huku nyumba ya mchungaji huyo
ikiwa imefungwa geti.
Eneo hilo pia lilizungukwa na
wafuasi wa askofu huyo karibu 200, waliokuwa wakisubiri kujua hatma ya kiongozi
wao huku wakisali.
Kati ya magari ya Polisi
yaliyoonekana katika eneo hilo, kulikuwa na Land Rover Defender zenye namba za
usajili T 337AKU na T 475 BNM na mengine aina ya Toyota Land Cruiser yenye
namba za usajili PT 1686 na PT 2665 yakiwa na maandishi ya Polisi.
Wakizungumza na mwandishi,
baadhi ya waumini wa kanisa hilo walidai wamekuwa na utaratibu wa maombi ya
asubuhi siku za Jumatano na Ijumaa, lakini jana walifika kanisani kama kawaida, lakini hawakumkuta askofu na
hakukuwa na taarifa.
Mchungaji Miriam Eliah alisema
waliamua kwenda nyumbani kwake majira hayo ya saa 12 asubuhi, wakakuta mlango
umefungwa jambo ambalo si kawaida na walipogonga hawakufunguliwa, lakini
walisikia sauti za watoto ndani.
Alisema baadaye waliona gari la
Polisi likifika katika maeneo hayo na kushusha polisi na ya pili ikafika na
kushusha polisi kisha zikaondoka na baadaye nyingine iliyokuwa na Polisi
ikafika maeneo hayo na kubaki karibu na geti la askofu huyo.
Mpaka mchana bado magari ya
Polisi yalikuwa yakiendelea kuzunguka karibu na nyumba hiyo, huku baadhi ya
viongozi wa kanisa hilo wakiwa katika makundi na vikao wakijadili.
Mwenyekiti wa serikali ya Mtaa
wa Wazo anapoishi Gwajima, Richard Njeru, alisema alipata taarifa ya askari
kuja kumkamata askofu huyo na aliwaona wakifika saa 12 asubuhi kwa sababu
hakufika juzi Polisi kama alivyotakiwa.
Ilipofika majira ya saa sita
mchana, magari ya Polisi yaliyokuwepo takriban sita yalianza kuondoka moja moja
na gari la mwisho lililondoka muda mfupi baada ya Wakili Kibatala kuwasili saa
6:30 akiwa na teksi.
Wakili huyo alifika katika eneo
hilo na kusalimia Polisi kisha kuonana na uongozi wa kanisa hilo waliokuwa
wakijadili jambo na baadaye gari la Polisi lililokuwa na polisi wanane
liliondoka katika eneo hilo.
Mara baada ya polisi wote
kuondoka, waumini wa askofu huyo walisogea katika geti la nyumba ya Gwajima na
kuanza kushangilia na kutamka kwa sauti kubwa kuwa ‘majeshi ya bwana ni hatari
sana’.
Akizungumza kuhusu kuondoka kwa
Polisi hao, Mwenyekiti wa Baraza la
Makanisa ya Kipentekoste Tanzania (CPCT) Wilaya ya Kinondoni na Mchungaji wa
Kanisa la EAGT, Emmanuel Mwasota, alisema uongozi wa Polisi umewataka askari
waliokuwa maeneo hayo kuondoka na kutaka Askofu Gwajima kwenda mwenyewe katika
Kituo cha Polisi cha Kati.
Alisema tatizo lililokuwepo ni
mawasiliano, kwani uongozi wa jeshi hilo juzi waliwataka wasiende jana kama
ilivyokuwa imetakiwa, kwa kuwa walikuwa wameshajitayarisha kwa kila kitu.
“Tunashangaa leo wamekuja
kuzingira nyumba lakini hakuna tatizo kwani baada ya muda askofu atatoka na
tutaenda naye polisi kama walivyotuagiza,”alisema
Ilipofika saa 7:32 Kibatala
akiongozana na wachungaji wengine wa Kipentekoste akiwemo Katibu Mkuu wa Baraza
la Makanisa ya Kipentekoste Tanzania (CPCT), Askofu David Mwasota, na
aliyekuwa Mbunge wa Bunge Maalum la Katiba, Amon Mpanju, waliingia ndani
ya nyumba ya Gwajima.
Baada ya kuingia ndani, nje ya
nyumba hiyo magari manne yaliingia katika eneo hilo ambapo alishuka Mtume
Onesto Ndegi wa Kanisa la Living Water Center na Mchungaji Vernon Fernandes wa
huduma ya Agape na wengineo.
Ilipofika saa 7:27 geti la
nyumba ya Askofu Gwajima lilifunguliwa na kutoka gari jeusi lenye namba za
usajili T 159, DDH likiendeshwa na mchungaji Hu na pembeni yake amekaa wakili
Kibatala.
Pia, katika gari hilo alipanda
Askofu Gwajima pamoja na Mpanju na kushangiliwa na waumini wa kanisa hilo na
baadaye Wakili Kibatala alizungumza na waandishi wa habari.
“Tunaenda Polisi kuitikia mwito
wa kisheria, kwani hatukuwa na taarifa zozote za kisheria za Polisi kuzingira
eneo hili na kwa nini walikuja kumkamata, baada ya kufika huko ndiyo tutaelezwa
yote,” alisema.
No comments:
Post a Comment