Mbunge wa Kigoma
Kaskazini, Kabwe Zitto (Chadema) jana aliteta faragha na Spika wa Bunge, Anne
Makinda kushauriana naye kama ajiondoe
kwenye ubunge baada ya chama chake kutangaza kumvua uanachama.
Lakini pia mbunge huyo jana hiyo jioni
alipanga kuonana na spika wa zamani Samuel Sitta kuzungumza naye kuhusu suala
hilo, ambalo habari za uhakika zinaeleza kuwa amedhamiria kuliaga Bunge hata
kabla ya chama chake kuwasilisha barua ya kumvua uanachama kwa spika.
Akizungumza na gazeti hili jana, Zitto ambaye
hakukubali au kukanusha habari hizo, alisema kwamba atatangaza kujiondoa kwenye
ubunge ama la, mara atakaposhauriana na spika Makinda pamoja na Sitta.
Zitto, ambaye jana habari zilitapakaa kuwa
ataliaga Bunge, aliliambia gazeti hili kuwa habari hizo zinaweza kuwa na ukweli,
lakini hatima yake itajulikana mara atakapokutana na viongozi hao ambao alisema
katika kipindi chake cha ubunge cha miaka 10 walimlea bungeni.
Zitto alisema, “Kama hizo fununu zipo
zitajulikana hivi karibuni, lakini kwanza ni lazima nishauriane na Makinda na
Sitta, hawa wamenilea katika maisha yangu ya ubunge wakiwa viongozi wangu,
hivyo siwezi kufanya jambo lolote linalogusa ubunge bila wao kushauriana nao.
“Hivi nakwenda kwa spika nyumbani kwake kwa
sababu nina miadi naye na baadaye nitakwenda kuongea na Sitta…baada ya hapo
nitakwambia kitakachofuata,” alisema Zitto.
Zitto ambaye alifika bungeni jana, alishiriki
kikao cha kwa kuuliza swali la nyongeza
na baadaye alishiriki kuchangia kwenye
muswada wa sheria ya kuratibu ajira za wageni nchini.
“Jamani mimi bado ni mbunge si mmeniona
nimeshiriki kikao cha leo, hayo mengine yatajulikana baadaye,” alisema Zitto.
Ubunge wa Zitto utakoma pale chama chake cha
Chadema kitakapoandika barua kwa Tume ya Taifa ya Uchaguzi ambayo pia
itamwandikia barua spika kumjulisha kuwa jimbo hilo liko wazi.
Hata hivyo, chama chake licha ya Mwanasheria
wake Tundu Lisu kutangaza kuwa Zitto sio mwanachama wa chama hicho, kinaonekana
kusita kuandika barua hiyo kwa maelezo kuwa kamati kuu ya chama hicho ndio
yenye jukumu la kufanya hivyo.
Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa
amenukuliwa na baadhi ya vyombo vya habari akieleza kuwa barua hiyo sio
kipaumbele cha chama kwa sasa, bali wanashughulikia mambo mazito ya kitaifa.
No comments:
Post a Comment