Wakati wadau wa usafiri nchini wakipendekeza kushuka
kwa nauli za daladala na mabasi yaendayo mikoani, wamiliki wa mabasi wametishia
kufuta utaratibu wa kutowatoza nauli askari na kuongeza kuwa, hata nauli
pungufu za wanafunzi sasa zitakuwa historia.
Wadau
wamependekeza kupunguzwa kwa nauli za mabasi yaendayo mikoani kwa viwango vya
kati ya asilimia 15 na 25 huku wakitaka nauli za daladala zipungue kutoka Sh
400 hadi Sh 300 kwa njia ya umbali wa kilometa 10.
Hayo
yaliibuka jana wakati wa mkutano wa
wadau kukusanya maoni kuhusu mapitio ya viwango vya nauli za mabasi ya mikoani
na daladala kupungua kutokana na kushuka kwa bei ya mafuta ulioandaliwa na
Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (SUMATRA).
Katibu
Mkuu wa Baraza la Watumiaji wa Huduma za Usafiri wa Nchi Kavu na Majini
(SUMATRA-CCC), Oscar Kikoyo alisema sababu ya kutaka nauli kupungua licha ya
kushuka kwa bei ya mafuta, pia wamiliki wa mabasi Julai mwaka 2014 walisamehewa ushuru wa
forodha kwa asilimia 10 hadi 25 ya mabasi mapya yanayoingizwa nchini.
Alisema
mafuta yanachangia katika uzalishaji wa
huduma kwa asilimia 20 hadi 30 na si jambo jipya katika kuomba kushusha nauli,
kwani mwaka 2009 nauli ilishuka ambapo
kwa nauli za kwenda mikoani wanataka ipungue kwa km moja kuwa Sh 28.05 badala ya sh 36.89.
Alitoa
mfano wa nauli wanazotaka kwa mabasi ya kawaida kuwa Moshi na Arusha (Sh 17,000
badala ya Sh 22,700), Mwanza (Sh 32,369 badala ya Sh 42,000), Mbeya (Sh 23,365)
badala ya sh 30,700), Bukoba (Sh 40,756 badala ya Sh 55,000) na Dodoma (Sh
12,678 badala ya Sh 16,700).
Katika
usafiri wa daladala wamesema wanataka iwe Sh 300 kwa kilometa kuwa Sh 31.39 kwa
usafiri wa kilometa 10 badala ya Sh 400 na kilometa 15 iwe Sh 450 na maeneo
mengine kupungua kwa Sh 100.
Kikoyo
alisema pia wanaandaa ombi kupitia kanuni na sheria kwa wamiliki wanaotoza
nauli kinyume inavyotakiwa walipishwe faini ya Sh milioni moja badala ya Sh
200,000 za sasa ili wayaone maumivu ya adhabu hiyo kubwa.
Naye
Mwenyekiti wa Umoja wa Wamiliki wa Mabasi ya Daladala (DARCOBOA), Sabri Mabruk
alisema wao wako tayari kupunguza nauli kwa asilimia mbili hata kesho kama
walivyofanya Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) na siyo asilimia 25
wanayotaka.
Alisema
tatizo kubwa katika ukokotoaji wa hesabu ni suala la ujazo wa abiria ambapo mwaka
2012 walipotakiwa kuunda kikosi kazi kwa ajili ya kushughulikia suala hilo
ambapo Sumatra wanadai ni asilimia 100, lakini ukweli ni asilimia 80.
“Ni
kweli unaweza kuona mabasi yamejaa, lakini wapo wanafunzi wanaolipa nusu nauli
(Sh 200) na askari ambao hawalipi kabisa sasa ni vema kuangalia suala hilo,
kwani hata nyakati za mchana mabasi huwa yanaota jua tu, hakuna abiria,”
alisema
Mabruk
alisema ni vema kabla ya nauli mpya kutangazwa kuangalia upya, kwani nafuu ya
kupungua bei ya mafuta ni Sh 12,000 ambayo inaishia kwa wafanyakazi hata
wamiliki hawaipati.
“Iwapo
mtaamua kushusha nauli tutafuta `ofa’ ya serikali ya kubeba askari bure pamoja
na kubeba abiria kwa nusu ya nauli inayotakiwa kisheria na hatutaenda kwenye
baraza au mahakamani,“ alisema.
Alisisitiza
kuwa ikiwa watatakiwa kwenda mahakamani au kwenye baraza watasimamisha magari
yao kufanya kazi, kwani hatua hizo zitakuwa kufidia nauli itakayoshushwa.
Naye
Katibu Mkuu wa Chama cha Wamiliki wa Mabasi ya Nchini (TABOA), Enea Mrutu alisema hawaoni sababu ya msingi kushusha
nauli kulingana na mahesabu na mafuta pekee si kigezo cha kushusha au kupanda nauli na kulalamikia
masuala hayo kuingiliwa na siasa.
Alishangaa
kwa nini suala la kushuka mafuta liwe kwa daladala pekee na siyo vyakula,
magazeti na mengineyo kushuka bei huku akisisitiza kuwa changamoto kubwa ni
suala la ujazo wa abiria linaloleta utata.
Huku
Katibu wa Chama cha Kutetea Abiria, Thomas Haule alisema wanaunga mkono maombi
ya Sumatra CCC katika kupunguza nauli, kwani katika punguzo wamiliki hao
wanapata faida kubwa huku akiitaka Sumatra pia kuangalia nauli za abiria
wanaoshuka katikati ya safari, kwani hazizingatiwi.
Pia
alitaka kuwe na mfumo maalumu katika kuongeza na kupunguza nauli pindi ikitokea
suala kama la kushuka au kupanda bei ya mafuta kuliko kupoteza rasilimali kukaa
na kujadili kila wakati.
No comments:
Post a Comment