Rais Jakaya Kikwete amezungumzia hali ya usalama wa
nchi, ikiwemo uvamizi wa vituo vya Polisi, uporaji wa silaha
ulioambatana na vifo vya askari na kusema matukio hayo, baadhi yake yana dalili
za ugaidi.
Akizungumzia hali ya usalama nchini jana katika hotuba
yake ya mwisho wa Februari, Rais Kikwete pia amekuja juu kuhusu mauaji
kwa watu wenye albinism na kusema vitendo hivyo vinafedhehesha, kudhalilisha
taifa na havivumiliki.
“Kwa jumla hali
ya usalama ni nzuri, hata hivyo kuna matukio ya kiusalama ambayo ningependa
kuyazungumzia. La kwanza ni mashambulizi yenye sifa za ujambazi na
mwelekeo wa kigaidi. Na, la pili ni la mauaji ya watu wenye ulemavu wa
ngozi,” alisema Kikwete.
Akizungumzia mauaji ya albino yaliyoanza kuibuka tena
mwaka jana na mwaka huu, baada ya hali kuwa tulivu mwaka 2011, Rais Kikwete
amekubali kukutana na viongozi na wanachama wa Chama cha Watu Wenye Ulemavu wa
Ngozi, kwa lengo la kuwasikiliza na kuangalia jinsi ya kumaliza mauaji ya watu
hao, yanayofanywa kwa imani ya ushirikina.
“Naungana na
Chama cha Albino Tanzania kulaani ukatili huu na kutaka watu wote
wanaojihusisha na ukatili huu wasakwe, wakamatwe, wafikishwe mahakamani na
kupewa adhabu kali inayowastahili wanapopatikana na hatia,” alisema Rais Kikwete.
“Nimekubali wiki
ijayo kukutana na baadhi ya viongozi na wanachama wa Chama cha Watu Wenye
Ulemavu wa Ngozi, kuwasikiliza maoni yao na kuangalia jinsi ya kumaliza
tatizo hili. Kwa kweli, mauaji ya albino ni jambo linalofedhehesha na
kudhalilisha taifa letu, ni vitendo visivyovumilika…hatuna budi sote
kushikamana na kuhakikisha tunapambana nao kisawasawa na kuwashinda, tusikubali
kamwe waturudishe kule kubaya tulikokuwa zamani, alisisitiza Rais Kikwete.
Rais Kikwete aliongeza “Nimesikitika na mauaji ya
ndugu zetu albino. Ni vitendo vya kinyama ambavyo havitegemewi kufanywa au
kutokea katika jamii yeyote. Naamini ushirikiano wa karibu kati ya
serikali na jamii utatuwezesha kutokomeza mauaji ya ndugu zetu wenye ulemavu wa
ngozi na kuliondolea taifa letu aibu hii”.
Alisisitiza, watu wenye ulemavu wa ngozi ni
wanadamu kama walivyo wasio na ulemavu huo na wana haki sawa ya kuishi na
kupata hifadhi ya maisha yao, kama walivyo wanadamu wengine.
Alitaka jamii kushikamana kuhakikisha mapambano dhidi ya
wahalifu hao yanafanywa na kuwakamata, wafikishwe kwenye vyombo vya sheria,
haki itendeke.
“Niwahakikishie
ndugu zangu albino wakati wote serikali inalipa uzito mkubwa suala la kudhibiti
na kukomesha mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi , watuhumiwa kadhaa wa
mauaji hayo wako waliokwishahukumiwa na wengine bado wanaendelea kusakwa,”
alisema Rais Kikwete.
Aliongeza serikali itatumia mbinu na maarifa
iliyotumia kukabili wimbi kubwa la mauaji hayo miaka ya nyuma. Aliomba wananchi
kutoa ushirikiano wa kuwafichua watu wanaofanya vitendo vya mauaji na kukata
viungo vya watu wenye ulemavu wa ngozi.
“Kutokomeza
kabisa matukio ya mauaji na ukataji wa viungo vya watu wenye ulemavu wa ngozi
ni jambo linalowezekana, kikubwa ni watu kuacha imani za ushirikina, eti kiungo
cha albino kinaweza kukusaidia, ni imani potofu kabisa, uvuvi, uchimbaji
madini, biashara ni vichocheo vya uovu huu,” alisema Rais Kikwete.
Aliomba wananchi kusaidia kutoa taarifa kuhusu
wanunuzi wa viungo hivyo na waganga wanaochochea mahitaji ya viungo vya albino.
Tukio la kwanza liliripotiwa mkoani Geita tangu Aprili
17 mwaka 2006. Watuhumiwa wa mauaji hayo waliuawa na wananchi wenye hasira.
Mwaka 2007 kulikuwa na matukio saba na mwaka 2008 matukio ya mauaji ya albino
yaliongezeka kutokana na watu 18 waliouawa.
Kikwete alisema jitihada za serikali zilifanywa kwa
kushirikiana na wananchi na hivyo mauaji yalipungua na kuwa tisa mwaka 2009.
Mwaka 2010 matukio hayo yalipungua na kuwepo na tukio moja.
Mwaka 2013 mmoja aliuawa na wengine watatu walijeruhiwa.
Mwaka 2014 waliuawa albino watatu na wawili walijeruhiwa. Januari mwaka huu,
tukio moja mkoani Geita limeripotiwa.
Matukio ya mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi
yametokea katika mikoa 10 kati ya mikoa 30 nchini. Mikoa hiyo ni
Mwanza wenye matukio 13, Kagera (sita), Tabora (matano), Geita (manne) na Mara
matukio manne.
Mikoa mingine ni Kigoma (manne), Simiyu (matatu),
Shinyanga (mawili), Arusha (moja) na Mbeya tukio moja.
Rais alisema katika kipindi cha takribani miezi 12,
kumekuwa na matukio ya watu kuvamia vituo vya Polisi, wengine kuchoma
moto na kupora silaha. “Pia kumekuwepo na matukio ya kuwashambulia Polisi
walioko kwenye doria na wengine kuporwa silaha,” alisema.
Kikwete ambaye amepongeza polisi wakishirikiana na Jeshi
la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania kwa kazi kubwa waliyofanya, amesema vyombo
vya usalama vinaendelea kufanya kazi ya uchambuzi wa kila tukio na kulipa
nafasi yake stahiki; kwa maana kama ni la ujambazi au ugaidi.
“Mafanikio tunayaona, kama nilivyoeleza na kama
tulivyosikia kule Tanga hivi karibuni, ni matunda ya ushirikiano huo.
Hata hivyo, nimewataka waendelee kuwasaka watu hawa waovu popote walipo ili
wafikishwe mahakamani na kuzirejesha mikononi mwa Polisi silaha zote
zilizoporwa,” alisema.
Rais alitaja maeneo ya matukio husika ni Newala,
Ikwiriri, Kimanzichana, Ushirombo, Songea, Pugu Machinjioni na Tanga ambako
jumla ya silaha 36 ziliporwa, askari saba walipoteza maisha na wengine kupata
majeraha.
Vituo vya Polisi vilivyovamiwa na silaha kuporwa kwenye
mabano ni Newala mkoani Mtwara (3), Ikwiriri wilayani Rufiji (7), Kimanzichana
wilayani Mkuranga ni silaha tano ambazo kati yake, mbili ni za polisi na tatu
za raia waliokwenda kuzihifadhi.
Uvamizi ulifanyika pia kwenye vituo vya Ushirombo
wilayani Bukombe (18), Pugu Machinjioni (1), Tanga (2) na Ruvuma ambako
kulikuwepo na matukio mawili ya Polisi kushambuliwa lakini silaha hazikuporwa.
Kwa mujibu wa Rais Kikwete, silaha 18 zilizoporwa
Ushirombo zimepatikana na watu 10 wanaotuhumiwa kuhusika na uhalifu huo
wamekamatwa.
Kuhusu tukio la Tanga, Kikwete alisema silaha moja kati
ya mbili zilizoporwa imepatikana na watuhumiwa saba wametiwa mbaroni,
wanne kati yao ni waliokuwa wamejificha katika mapango ya Kiomoni
wilayani Tanga.
Kwa upande wa watu wanne wanaotuhumiwa kuhusika na tukio
la Ikwiriri, walikamatwa na kwenye tukio la Newala, silaha zote tatu
zimepatikana na watu wawili wametiwa nguvuni.
“ Upelelezi
unaendelea wa kuzipata silaha zilizoporwa ambazo hazijapatikana mpaka sasa kila
moja kutoka Kimanzichana, Pugu Machinjioni na Tanga,” alisema.
Aidha, Kikwete alitoa wito kwa wananchi kushirikiana kwa
karibu na vyombo vya usalama hususani Jeshi la Polisi kupata mafanikio
zaidi dhidi ya uhalifu kwa kutoa taarifa za kuwapo vitendo viovu au nyendo za
watu waovu wanavyokusudia kufanya wahalifu au taarifa za waliokwishafanya
uhalifu.
Kikwete pia alitaka wananchi kuacha kushabikia watu
waovu, wala kueneza taarifa zao potofu kwenye mitandao ya kijamii.
“ Tutumie
mitandao ya kijamii kuponda fikra zao potofu, fikra zao hasi na vitendo vyao
viovu pamoja na kuwafichua wao na mambo yao mabaya wayafanyayo,” alisema.
Pia, Kikwete aliwapongeza wananchi waliotoa taarifa zilizowezesha
kuzuia uhalifu kufanyika au kufanikisha kuwatia mbaroni wahutumiwa
wa vitendo vya ujambazi na ugaidi.
Wakati huohuo, Rais Jakaya Kikwete ameagiza Hazina
kuhakikisha inaitengea fedha Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kwa kazi ya
kuandikisha wapiga kura kwa Mfumo wa Teknolojia ya Utambuzi wa Alama za Vidole
‘Biometric Vote Registration’ (BVR) ikamilike kama ilivyopangwa.
Aidha, ametaka watu kuwa na subira kuhusu Kura ya
Maoni, wazingatie masharti ya Sheria ya Kura ya Maoni na Kanuni zake.
Akihutubia taifa jana, Kikwete alisema Serikali itatimiza
ahadi yake kwa kufanya kila linalowezekana kuwezesha Tume kirasilimali iweze
kutimiza jukumu hilo.
Kauli ya Rais imekuja siku chache baada ya vyama
vinavyounda Ukawa hivi karibuni kukaririwa katika mkutano na waandishi wa
habari, vikisema Nec inakabiliwa na ukosefu wa fedha, utakaoifanya Tume
ishindwe kutekeleza majukumu yake ya uandikishaji wapiga kura kwa ufanisi.
Ukawa kupitia kwa Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi
(CUF), Profesa Ibrahimu Lipumba vilitaka Serikali kuelekeza nguvu na kuiongezea
fedha Nec.
Vyama hivyo vilisema uhaba huo wa fedha umefanya Tume
kuwa na upungufu wa mashine 7,750 na pia kutokuwa na watumishi wa
kutosha.
“Nimekwishawakumbusha
Hazina kuhusu umuhimu wa zoezi hili kufanikiwa kama ilivyopangwa. Nimewataka
wahakikishe wanatoa kipaumbele cha kwanza katika mgao wa fedha. Kama
haifanyiki, naomba Tume waniambie mimi mwenyewe,” alisema.
Aidha, Kikwete alisema changamoto za kiufundi
zilizojitokeza na zile zinazotokana na upya wa mfumo kwa watumiaji, zimefanyiwa
kazi na watengenezaji wa vifaa vinavyotumika katika awamu hii ya uandikishaji
nchi nzima.
Alisema, kuanza kutumika kwa teknolojia hii ni kielelezo
cha utashi wa Serikali kuwa nchi iwe na uchaguzi ulio huru, wazi na haki.
Akizungumzia kuanza kwa uboreshaji wa daftari na
uandikishaji wapiga kura ulioanzia katika mji wa Makambako, Kikwete alisema
wananchi wamejitokeza kwa wingi kuliko ilivyotarajiwa.
Alisema kati ya Februari 23 hadi 25 mwaka huu, Tume
ilitegemea kuandikisha wapiga kura 9,541 lakini kutokana na mwamko wa wananchi
wameweza kuandikisha wapiga kura 13,042.
Kikwete alisema kila kituo kilikuwa kinaandikisha kati
ya wapiga kura 80 na 150 kwa siku, huku lengo la Tume ni kuandikisha wapiga
kura 32,000 katika Halmashauri ya Makambako ambako kwa siku wanatarajia
kuandikisha watu 4,320.
“ Naambiwa kuwa hesabu za juzi na jana wameandikisha
hadi wapiga kura 6,000 kwa siku. Kwa kasi hii na kama mambo yatakwenda
kama inavyotarajiwa, lengo litafikiwa na hata kuvukwa.”
Kikwete aliipongeza Tume kwa hatua waliyofikia katika
uandikishaji na kuwa hali hiyo inaondoa hofu iliyoanza kuingia miongoni mwa
baadhi ya watu kuwa huenda zoezi hili lisingefanikiwa.
Kabla ya uzinduzi uliofanywa mwezi uliopita na Waziri
Mkuu, Mizengo Pinda Tume ilifanya majaribio ya uandikishaji wa wapiga kura kwa
kutumia mashine za BVR katika kata 10 za halmashauri za Kinondoni, Kilombero na
Mlele kazi iliyofanyika kwa mafanikio kwa kuvuka malengo ya uandikishaji.
Kilombero walifikia asilimia 110.9 ya lengo, Mlele
asilimia 101 na Kawe ilikuwa ni asilimia 105.67.
Aidha, Kikwete ametoa wito kwa wananchi kuhakikisha
wanakwenda kujiandikisha kwa mujibu wa ratiba ya uandikishaji katika maeneo yao
kama itakavyotolewa na Tume.
“Msifanye ajizi maana hakutakuwepo na fursa nyingine ya
kujiandikisha kabla ya uchaguzi mkuu baada ya fursa hii kupita.
Kikwete aliongeza, “Naendelea kusisitiza kuwa
watakaojiandikisha wakati huu ndio watakaopiga kura ya maoni kuhusu Katiba
Inayopendekezwa na ndio watakaopiga kura katika uchaguzi mkuu, kwani
vitambulisho vya zamani havitatumika.
Kikwete pia alitumia fursa hiyo kuwaomba viongozi wa
vyama vya siasa, Serikali, dini na asasi za kiraia kuungana na Serikali na Tume
katika kuwakumbusha na kuwahamasisha wananchi wakajiandikishe.
“Naomba
tusiwachanganye wananchi kwa kutoa taarifa zisizokuwa za kweli na kuwafanya
wakaacha kujiandikisha.”
Alisema, Serikali itafanya kila linalowezekana
kuhakikisha kila atakayejitokeza anaandikishwa na kuzipatia ufumbuzi kwa wakati
changamoto zitakapojitokeza.
“ Kupiga kura
kuamua kuhusu Katiba Inayopendekezwa au kuchagua Rais, Wabunge na Madiwani ni
haki na wajibu wa kila raia. Kuipata haki hiyo na kuweza kutimiza wajibu huo
kunategemea kuwa na kitambulisho cha mpiga kura. Bila ya hivyo
haiwezekani.”
Akizungumzia Kura ya Maoni ya Katiba Inayopendekezwa,
alisema Tume pia itatoa maelekezo kuhusu kampeni ya Kura ya Maoni
wakati ukiwadia.
“Naomba watu wawe na subira na kuzingatia masharti
ya Sheria ya Kura ya Maoni na Kanuni zake. Tukifanya hivyo, zoezi hili
muhimu na la kihistoria litatekelezwa kwa usalama na utulivu. Watu
watafanya uamuzi kwa uhuru, uelewa, amani na usalama.”
Kikwete alisema utekelezaji wa mchakato huo wa
kura ya maoni, umeshaanza na unaendelea ikiwa ni pamoja kuandikisha wapiga kura
na usambazaji wa katiba hiyo.
Alisema hadi mwishoni mwa Februari, vitabu 1,558,805
vilikuwa vimechapishwa na nakala 1,341,300 kusambazwa. Nakala 1,141,300
zimesambazwa kwenye mikoa 25 ya Tanzania Bara na nakala 200,000 zimegawiwa
Zanzibar.
Alisema kwa upande wa Tanzania Bara kila kata imepewa
vitabu 300. Kwa vile kata zina wastani wa vijiji vitano hii ina maana
kwamba kila kijiji kimepata vitabu 60.
Kikwete alisema mpaka sasa asasi za kiraia 495
zimejiandikisha kwa ajili ya kutoa elimu kwa umma, asasi 420 ni za Bara na 75
za Zanzibar.
No comments:
Post a Comment