WASICHANA WADOGO WANAOBEBA MIMBA WAONGEZEKA


Msichana mmoja kati ya wanne wenye umri wa  miaka 15 hadi 19 ni mjamzito au ana mtoto, imeelezwa.

Idadi hii inawakilisha maisha halisi na kuonesha kwamba kama jitihada za makusudi hazitachukuliwa wasichana wataendelea kukosa haki zao za msingi na kuzidi kuwa wategemezi.
Hayo yalisema na mke wa Rais Mama Salma Kikwete wakati akifungua mkutano wa
kimataifa wa utafiti katika ukunga ulioandaliwa na LUGINA Afrika Midwives Research Network (LAMRN) uliofanyika katika Hoteli ya Kunduchi jijini Dar es Salaam.
Mama Kikwete ambaye ni Mwenyekiti wa Taasisi ya Wanawake na Maendeleo (WAMA) alisema vifo vya akinamama wajawazito na watoto  wenye umri wa chini ya miaka mitano ni tatizo katika nchi zote zilizopo Kusini mwa Bara la Afrika hata hivyo jitihada mbalimbali zinafanyika ili kuhakikisha tatizo hilo linapungua au kumalizika kabisa.
“Naamini utafiti uliofanywa na LAMRN kwa kipindi cha miaka miwili, utasaidia kuongeza utendaji kazi wa wakunga na kupunguza vifo vya akinamama wajawazito na watoto katika bara letu la Afrika,” alisema.
Kuhusu mimba za utotoni Mwenyekiti huyo wa WAMA alisema tafiti zilizofanyika zinaonesha wasichana  wanaanza kufanya mapenzi mapema zaidi wakiwa na umri mdogo ukilinganisha na wavulana jambo linalopelekea kupata mimba za utotoni na hivyo kukosa elimu kwa kukatisha masomo yao.
Mama Kikwete alisema: “Takwimu za Ulimwengu zinaonesha zaidi ya wasichana milioni 58 wameolewa kabla ya kufikisha umri wa miaka 18  kati ya hao milioni 15 wana umri wa miaka 10 hadi 14”.
Nchini Tanzania asilimia 13 ya wasichana wanaanza kufanya mapenzi wakiwa na umri wa miaka 15 na kwa upande wa wavulana  kwa umri huo huo ni asilimia saba".
Akizungumza kwa niaba ya Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Seif Rashid, Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Paul Makonda alisema  kaulimbiu ya mkutano huo ambayo ni 'utendaji wa kazi kwa kutumia ushahidi wa utafiti, utaimarisha afya ya mama na watoto wachanga' imekuja wakati muafaka wa kuweka suala la afya ya mama na mtoto kwanza hii ni moja ya mipango ya Shirika la Afya Ulimwenguni (WHO) kwa mwaka  2010-2015 katika bara la Afrika.

No comments: