Taasisi
ya Mashehe na Wanazuoni wa Kiislamu, imewataka maaskofu nchini wawe wavumilivu,
kwani Serikali ni ya watanzania wote.
Aidha,
imewasisitiza watanzania kwa ujumla, kupata elimu ya Katiba Inayopendekezwa kwa
kuisoma kwa makini na kuielewa ili wawe na uwezo na uhuru wa kuchagua kile
wanachokiona kina manufaa kwao, bila kuwepo shinikizo la kiimani.
Hayo
yalisemwa jijini Dar es Salaam jana na Katibu Mkuu wa Taasisi hiyo, Shehe
Khamis Mataka (pichani), wakati akitoa tamko la taasisi hiyo, kufuatia tamko la TCF
kuhusu Katiba Inayopendekezwa, Mahakama ya Kadhi na Hali ya Usalama na Amani ya
Nchi.
“Tunawasihi
watanzania wote kuendelea kudumisha undugu wao kama watanzania, bila kujali
rangi, dini, kabila na itikadi za kisiasa na tumkemee yeyote yule anayetaka
kutugawa kwa kutumia misingi ya kidini, kikabila, kisiasa na kiuchumi” alisema.
Pia,
imeiomba Serikali iache kuzingatia tamko lililotolewa na Jukwaa la Wakristo Tanzania
(TCF), badala yake iendelee na mchakato wa Katiba Inayopendekezwa na Mahakama
ya Kadhi kwa kufuata misingi ya haki.
Shekhe
Mataka aliongeza “Taasisi imezipitia kwa kina nukta zote nne za Tamko hilo
pamoja na hitimisho lake na kubaini kwamba maaskofu wamejisahau kwamba wao ni
viongozi wa kiimani na kiroho, ambao wanatakiwa wawe tayari kumpokea yeyote na
kumpa neno la hekima lililojazwa faraja, bila hata ya kujali itikadi au chama
chake cha siasa. Badala yake wameamua kutoa faraja kwa waumini wao kwa
kuzingatia utashi wa kisiasa”.
“Maaskofu
wameamua kuanzisha utamaduni mpya wa kuendesha mambo ya kisiasa kwa misingi ya
kiimani na hivyo kutoa tishio la kuwagawa watanzania kwa misingi hiyo. Hivyo
baada ya Taasisi yetu kujiridhisha na yaliyomo katika Tamko hilo la Maaskofu
chini ya mwavuli wa TCF, tunashauri hatua za kuchukua,” alisema.
Alisema,
“Kwa kuwa serikali ina vyombo makini vyenye wataalamu wenye uwezo wa kufahamu
na kuelewa uvunjifu wa katiba na Umoja wa Kitaifa, tunaomba ipuuze tamko hilo
ambalo limeisikitisha taasisi yetu na kuwadhalilisha waislamu.
“Suala la Mahakama ya Kadhi ni haki ya
Waislamu na haliwahusu wala halihitaji ridhaa ya wasiokuwa Waislamu, kama
ambavyo waislamu hawajapata kuombwa ridhaa yao katika yale ambayo Serikali
imekuwa ikiwafanyia wakristo na makanisa yao,” alisema.
Shehe
Mataka alisema, “Taasisi hii inapinga kwa nguvu zote madai ya Maaskofu kuwa,
Waislamu kuwa na Mahakama ya Kadhi ni uvunjifu wa Katiba, kwani sheria za
Kiislamu ni moja ya vyanzo vya sheria ya Tanzania. Mahakama za Tanzania
zimekuwa zikitumia sheria hizo kuhukumu kesi za waislamu kuhusu ndoa, talaka,
mirathi toka mwaka 1963 na kufuatiwa na sheria ya Tamko la Sheria ya Kiislamu
ya mwaka 1964 na kuhitimishwa na Sheria ya Ndoa ya mwaka 1971”.
Alisema,
“Jambo la msingi hapa ni kuwa kesi hizo zinahukumiwa na mahakimu wasio na
elimu, wala ujuzi na sifa za kuwa Makadhi, kwa mujibu wa Sheria za Kiislamu na
ndio msingi wa Waislamu kudai uwepo wa Mahakama ya Kadhi Tanzania Bara”.
Alisema
taasisi hiyo inawakumbusha maaskofu kuzingatia kuwa madhara ya kuwagawa
watanzania kwa misingi ya kiimani, dhambi yake haitaishia kwenye kadhia ya
Mahakama ya Kadhi, wala Katiba Inayopendekezwa, bali itaendelea kukita mizizi
yake katika kila jambo linalowahusu watanzania.
Mataka
alisema, “Jukwaa linasisitiza viongozi wa dini wabaki kuwa walezi, siyo
kuwagawa watu. Mambo ya siasa tuwaachie wanasiasa, sisi tubaki na heshima yetu
ya kuwa viongozi wa dini, kwa sababu hata waumini wetu wanatuamini tunapoongea
jambo kwamba ni tamko la Kimungu na wanatakiwa kulifuata. Kwa hili, hata Askofu
Mkuu wa Kanisa Katoliki Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Mwadhama Polycarp Kardinali
Pengo ameona hili lina tatizo”.
No comments:
Post a Comment