VIONGOZI WA DINI KUCHUNGUZWA MIENENDO YA UTUME WAO


Serikali imetakiwa ichunguze viongozi wa madhehebu ya dini ya Kikristo na Kiislamu nchini, ili ijiridhishe na mienendo ya utume wao wa kuhubiri injili na sala kwa wananchi.

Lengo la uchunguzi huo, limeelezwa kuwa ni kubaini viongozi wa kiroho wanaokwenda kinyume na maadili ya kazi zao, hususani wakati huu nchi inapokaribia  Uchaguzi Mkuu, ili kujenga na kuimarisha mshikamano na amani ya nchi kwa wananchi na Taifa kwa ujumla.
Rai hiyo ilitolewa juzi jijini hapa na Naibu Kadhi Mkuu Tanzania Bara, Sheke Abubakari Zuberi, wakati akizungumza kwenye kongamano la amani la ndani mkoani hapa.
Kongamano hilo, lilishirikisha maaskofu na mashehe, wakuu wa wilaya, wabunge, kamati za ulinzi na usalama na wananchi kutoka wilaya zote saba za Mkoa wa Mwanza.
“Viongozi wa dini wachunguzwe na Serikali kama zinavyofanya nchi zingine, maana wao wanaweza kuipotosha amani.
“Kama wapo wanaotuhumiwa kushiriki kwenye vitendo vya rushwa wanaweza kuiharibu amani ya nchi, kwa sababu wana hamasa kubwa na wafuasi wengi wanaoweza kuwahamasisha kuvuruga amani ya nchi tuliyo nayo,” alisema.
Aliwataka viongozi wa dini na wanasiasa, kujiepusha na vitendo vya ufisadi kwa maelezo kuwa vinawaondolea heshima yao inayotokana na maadili ya kiroho,  hasa katika kuhudumia waumini wao na kuwaongoza wananchi kwenye maeneo yao.  
Aliwataka wananchi na viongozi wa madhehebu ya dini, washirikiane pamoja kutoa taarifa za matukio yenye kuhatarisha amani mara wanapobaini viashiria vya kuhatarisha amani katika nchi, kwa kuwa maskari waliopo nchini hawawezi kulinda amani ya nchi peke yao.
Aliitaka Serikali ianzishe mtaala maalumu wa amani, utakaofundishwa katika shule za msingi na sekondari, ili kukuza na kujenga vijana maadili kwa faida ya nchi na maendeleo yao.
Aliwataka viongozi wa kisiasa, wahubiri amani bila ya kujali itikadi ya vyama vyao vya siasa na kwa kushirikiana na Serikali, washiriki kikamilifu kwenye utatuzi wa migogoro inayowakumba wananchi kwa sasa, ikiwemo ya wakulima na wafugaji.
Alilaani watu wanaoua wenzao wenye ulemavu wa ngozi kwa madai ya kujipatia utajiri na madaraka, ambapo alisema jambo hilo linalaaniwa na viongozi wote wa madhehebu ya dini.
Naye Mchungaji Dk William Kopwe, kutoka Jumuiya ya Kikristo Tanzania (CCT), alisema kuwa amani ya nchi sio kitu cha kuchezea kiholela, na kuongeza kuwa ni kitu kinachofaa kuheshimiwa na kuenziwa na watu wa makundi yote katika jamii.
“Suala la amani ya nchi liangaliwe kwa mapana yake, sio jambo rahisi la kuchezea chezea hivi, na ili ujue amani ni kitu gani, iweke katika makundi mawili, amani hasi inayotokea kunapokuwepo vurugu na mifarakano na amani chanya ambayo ni kinyume cha hayo,” alisema.
Awali wali katika hotuba ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Magesa Mulongo, iliyosomwa kwa niaba yake na Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana, Baraka Konisaga, alisema kongamano hilo la amani ni la kujenga na sio la kubomoa na Serikali inatarajia kuona upendo na mshikamano wa watu wote katika kulinda amani ya nchi 
Alisema baada ya kuhamia jijini Mwanza, alishukuru kukuta ipo Kamati ya Amani inayojishughulisha na suala zito la amani na kuitaka kamati hiyo kufika katika ofisi yake wakati wowote watapokuwa na agenda ya kujadili suala la amani.

No comments: