Serikali ya Tanzania na Zambia zimekubali kulisuka upya
Shirika la Reli la nchi hizo (Tazara), kwa kufanya marekebisho ya kimfumo na
kiutendaji ili kutatua matatizo ya kimuundo na kimenejimenti yanayochangia
kuzorota kwa ufanisi wa shirikia hilo.
Katika hotuba yake ya mwisho wa mwezi Februari,
aliyoitoa juzi usiku, Rais Kikwete alisema hatua hiyo inatokana na mafanikio ya
ziara yake ya siku mbili aliyoifanya nchini Zambia mwezi uliopita, kwa mwaliko
wa Rais mpya wa wa nchi hiyo Egdar Lungu.
Akizungumzia usukwaji wa Tazara, Rais Kikwete alisema
wamekubaliana kuchukua hatua thabiti kutatua matatizo ya kiungozi,
kifedha na kiufundi yanayolikabili shirika hilo kwa sasa.
“Tumeelewana,
hatuna budi kufanya marekebisho ya kimfumo, kiutendaji ili kutatua matatizo ya
kimuundo na kimenejimenti yanayochangia kuzorota kwa ufanisi wa shirika hili”,
alisema Rais Kikwete.
Katika hotuba yake hiyo alisisitiza kuwa katika
mazungumzo yao na Rais wa Zambia, wameafikiana masuala yote na kukubaliana
serikali za nchi hizo kutekeleza wajibu wake kwa Tazara.
“Tumekubaliana
kila nchi itekeleze wajibu wake ipasavyo kwa Tazara, michango ya fedha itolewe
tufufue shirika hili muhimu kwa uchumi wa nchi zetu mbili”, alisema Rais
Kikwete.
Aidha, alisema wamekubaliana kuangalia uwezekano wa
kuruhusu makampuni au mashirika mengine ya reli kutumia reli hiyo kusafirisha
mizigo yao kwa kulipia ushuru wa huduma kwa shirika hilo.
“Wazo la kuruhusu
kampuni au mashirika ya reli mengine kutumia reli yetu ni wazo jema, tumeagiza
Baraza la Mawaziri kulifanyia kazi wazo hili mapema iwezekanavyo”, alisisitiza
Rais Kikwete.
Akizungumzia sekta ya Nishati, Rais alisema
wamekubaliana nchi hizo kuendelea kushirikiana na kuimarisha bomba la mafuta la
TAZAMA, ambapo pia Zambia imeelezea dhamira yake ya kujenga bomba la
kusafirisha gesi kutoka Dar es Salaam hadi Zambia.
‘Wameomba
tukubali kuwauzia gesi asilia, nimewaambia ni jambo linalowezekana,
tumekubaliana nchi zetu zilifanyie kazi ombi hilo”, alisema Rais Kikwete.
Pamoja na ombi hilo, serikali ya Zambia imeahidi
kuimarisha njia ya umeme kutoka Kasama hadi Mbala, Zambia inakoanzia njia
inayoleta umeme Sumbawanga.
Ikiwa ahadi hiyo itakamilika Rais alisema itaondoa
matatizo ya sasa ambapo umeme unaofika Sumbawanga kutoka Mbala, ni mdogo
na hauna nguvu ya kutosha kwa matumizi ya nyumbani, ofisini na viwandani.
Kuhusu kuboresha huduma kwa abiria na mizigo katika
mpaka wa Tanzania na Zambia eneo la Tunduma, Rais alisema wamekubaliana
Tanzania ikamilishe ujenzi wa jengo litakalowezesha huduma zote muhimu za
mpakani kutolewa katika jengo hilo.
Na kwamba wakati jengo hilo likisubiriwa ujenzi wake,
watatumia jengo la muda kurahisisha taratibu za usafiri wa abiria na
usafirishaji wa mizigo katika mpaka wa Tanzania na Zambia.
Pia uboreshaji wa taratibu za forodha kwa mizigo itokayo
Bandari ya Dar es Salaam kwenda Zambia na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo
(DRC), kupitia Zambia unaendelea.
No comments:
Post a Comment