Mke na Mume wanaotuhumiwa kumuoza binti wa miaka 10 jana
walifikishwa katika Mahakama ya Wilaya ya Dodoma Mjini huku Mahakama ikifunga
dhamana yao hadi kesi hiyo itakapomalizika.
Washtakiwa hao wanakabiliwa na shtaka la kumuozesha
mtoto mwenye umri wa miaka 10 ambaye ni binti yao kwa mahari ya Sh 100,000 na
mbuzi 12.
Mbele ya Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Wilaya Dodoma Mjini
, Mwajuma Lukindo Mwendesha Mashitaka wa Serikali, Lina Magoma, alidai
washtakiwa Stephano Nyambuya (65) na mkewe Juliana Gidion (30) ambao ni wakazi
wa kijiji cha Lionii wilayani Bahi mkoani Dodoma walitenda kosa la kumuozesha
mtoto aliye chini ya miaka 15.
Mwendesha mashitaka huyo alisema watuhumiwa hao
walitenda kosa hilo kinyume cha kifungu cha sheria namba 138 (2)
cha kanuni ya adhabu kilichofanyiwa marejeo mwaka 2002.
Magoma alisema wazazi na walezi hao waliamua kumuozesha
mtoto aliye chini ya umri huo kwa Joshua Mnamba mwenye umri wa miaka (25),
ambapo wote kwa pamoja walikana shitaka lao.
Hakimu Mkazi Lukindo alisema washitakiwa hao
wanatakiwa kuwa rumande kutokana na kosa walilotenda kutokuwa na dhamana.
Alisema sheria ya makosa ya jinai inazuia dhamana kwa watu wenye makosa kama
hayo, hivyo washitawa watabaki rumande mpaka kesi yao itakapokwisha.
Mnamba ambaye alimuoa binti huyo alifikishwa mahakamani
hapo Februari 24, mwaka huu na yuko rumande. Kesi hiyo imepangwa kutajwa tena
Machi 16, mwaka huu.
Mshtakiwa huyo alishtakiwa kwa kosa la kubaka.
Kwa sasa mtoto huyo aliyeozwa amepata hifadhi kwa Mkuu
wa Wilaya ya Dodoma Mjini Betty Mkwasa. Kukamatwa kwa mtuhumiwa huyo
kulifuatiwa taarifa zilizotolewa na majirani kwa Serikali ya Kijiji na hatimaye
Polisi na watuhumiwa kufanikiwa kukamatwa.
No comments:
Post a Comment