Moto
mkubwa uliozuka na kuteketeza sehemu ya bweni la wanawake katika Hosteli za
Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) zilizopo Mabibo jijini Dar es Salaam,
uliibua taharuki kwa wanachuo na wananchi waishio jirani na eneo hilo.
Katika
tukio hilo, mbali ya moto kuunguza mali za wanafunzi, wawili kati ya wanafunzi
wa kike walikimbizwa hospitali baada ya kuumia katika purukushani za kujiokoa
ambapo mmoja alijirusha kutoka ghorofa ya pili ulipoanzia moto huo na mwingine
aliumia kwenye mkanyagano wakati wa kujiokoa.
Kwa
mujibu wa Makamu Mkuu wa chuo hicho kikongwe na chenye heshima ya miaka mingi
barani Afrika, Profesa Rwekaza Mukandala alisema hakuna mwanafunzi aliyepoteza
maisha kutokana na mkasa wa moto huo ulioanza majira ya saa 3 asubuhi katika
ghorofa ya tatu katika jengo la Block B, isipokuwa wanafunzi wawili walioumia
baada ya kuruka.
“Tunashukuru
Mungu hakuna aliyepoteza maisha ingawa kuna wanafunzi wawili wamejeruhiwa
na tumewakimbiza hospitali. Ila mali nyingi za wanafunzi zimeharibika vibaya.
“Moto
umetokea na tunahisi kuwa ni hitilafu ya umeme, lakini tunasubiri taarifa ya
wataalamu kutupa chanzo cha moto.”
Aliongeza
kuwa, ghorofa ya tatu ambayo ndiyo iliyowaka moto imeharibika vibaya na kuwa
uongozi wake umewatoa wanafunzi wote katika jengo hilo kwa sababu za kiusalama.
“Shida
kubwa tunayoshughulika nayo ni kuhakikisha tunawapatia malazi wanafunzi wote
waliokuwa kwenye jengo liliokumbwa na moto. Hawatakaa mpaka hapo wataalamu
watakapotuambia kama jengo hilo ni salama kwa kuishi watu.
Jengo
hilo lenye ghorofa tatu lina vyumba 153 ambapo kila chumba wanaishi kati ya
wanafunzi wanne hadi nane.
Alisema
pia uongozi wa chuo chake utafanya ukarabati katika mabweni yaliyoko ghorofa ya
kwanza na ya pili, ambayo pamoja na kuwa hayakukumbwa na moto, milango ya
vyumba ilivyunjwa ili kuondoa vitu vilivyokuwapo.
“Tutawasaidia
wanafunzi wote, hawa ni wanetu, hata wale wenye shida binafsi tutawasaidia, kwani
kila kitu chao kimepotea ikiwa ni pamoja na vifaa, vitabu na fedha,” alisema na
kuongeza kuwa, ninaamini hitilafu ya umeme uliokatika usiku wa kuamkia siku ya
jana na kurudi ghafla baadaye.
Hata
hivyo, pamoja na athari ya moto, baadhi ya wanafunzi wamejikuta wakipoteza
vifaa vyao kama kompyuta mpakato, fedha na hata simu baada ya kuibiwa na watu
walioingia katika vyumba kwa kile kilichoonekana kama kwenda kutoa msaada
katika janga la moto.
Katika
eneo la tukio, wanafunzi hao wakionekana kupatwa na mshtuko, walielekeza lawama
zao kwa Kikosi cha Jeshi la Zimamoto na Uokoaji kwa kuchelewa kufika eneo la
tukio licha ya kudaiwa kuarifiwa mapema.
Kutokana
na hali hiyo, wanafunzi, wa kike na kiume katika hosteli hizo zenye uwezo wa
kuchukua zaidi ya wanafunzi 4,000 kwa wakati mmoja, walishirikiana kuuzima moto
na kuokoa mali.
Hata
gari la Zimamoto lilipowasili, tayari shughuli ya kuokoa mali na kuudhibiti
moto ilikuwa imefanikiwa, ndipo askari wa kikosi hicho wakajikuta katika wakati
mgumu kutokana na wanafunzi wenye hasira kuanza kuwazomea na kuwarushia mawe
wakiwataka waondoke kabisa eneo hilo.
Waziri
Mkuu wa Serikali ya Wanafunzi wa chuo hicho, Gibson George alisema chanzo
hakijajulikana, lakini moto huo ulisambaa maeneo mbalimbali ya jengo hilo
haraka.
"Watu
wa zimamoto tumewapigia simu mapema sana ila wamechelewa kufika hadi muda
huu (saa 4:30) ndio wamefika, tumejaribu kuuzima moto na umepungua kidogo japo
bado unaendelea kwa baadhi ya vyumba," alisema.
Hakuna
kiongozi wa Jeshi la Polisi mkoa wa Kinondoni aliyepatikana kuzungumzia tukio
hilo, kwani hata Kamanda wake, Camillius Wambura alipotafutwa mara kadhaa kwa
njia ya simu, hakupatikana.
No comments:
Post a Comment