LOWASSA AMFAGILIA KINANA, ASEMA HAJAWAHI KUTOKEA


Aliyekuwa Waziri Mkuu  na Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa amesema Chama Cha Mapinduzi (CCM), hakijawahi kupata Katibu Mkuu hodari na mchapakazi wa mfano wa Abdulrahman Kinana, tangu kuanzishwa kwake.

Katika hatua nyingine, Kinana akiwahutubia wakazi wa mji wa Mto wa Mbu wilayani Monduli, alisisitiza kuwa uadilifu utaendelea kuwa sifa namba moja ya mgombea wa CCM kwa nafasi yoyote ya uongozi, na kwamba Watanzania wanaweza kusamehe kasoro nyingine, lakini si kwa kiongozi kuwa mlaji na mdokozi wa mali ya umma.
Aidha, Katibu Mkuu huyo wa CCM amemwomba Lowassa kusaidia kushawishi wabunge wenzake kushinikiza bungeni kubadilishwa kwa sheria zote, zinazosababisha kero kwa wananchi, zikiwemo sheria zilizorejesha kwa
mlango wa nyuma ushuru na kodi kero kwa wananchi, ambazo awali zilifutwa na Serikali.
"WanaCCM wote nyie ni mashahidi, kazi inayofanywa na Kinana na Nape (Nnauye- Mjumbe wa Halmashauri Kuu, Itikadi na Uenezi) ni kubwa na kwa kiasi kikubwa sana wamerejesha uhai wa chama chetu.
"Chini ya uongozi wa Kinana sasa CCM imekuwa moja na kwa kiasi kikubwa amerejesha imani ya wanaCCM na wananchi wa Tanzania kwa chama chao.
“Kazi anayoifanya ni kubwa na ngumu sana. Kufanya mikutano 26 mfululizo si jambo rahisi hata kidogo na nimemweleza mke wangu azungumze na mkewe, ili apunguze hizi safari," alisema Lowassa aliyekuwa akishangiliwa na umati wa wananchi.
Akizungumza na wakazi wa Jimbo la Monduli, Kinana pamoja na kusifu kile alichokiita kiwango cha juu cha utekelezaji wa Ilani ya CCM kilichofanywa na Lowassa katika jimbo hilo, alisisitiza umuhimu wa viongozi na wanachama wa CCM kuzingatia uadilifu katika utumishi wao kwa umma.
"Katika siku za hapo katikati, wananchi walianza kupoteza imani kwa chama chetu kwa vile sisi wenyewe hatukuwa sawa, tulikuwa hatutekelezi kile wananchi wanachohitaji, lakini sasa tumejipanga vizuri katika kukisimamia chama chetu ipasavyo.
"Watanzania wa sasa hawapo tayari kuona nchi yao inaongozwa kwa ujanja ujanja, au kwa watu kuwa walaji au wala rushwa. Wapo tayari kukusamehe kosa jingine lolote, lakini si kwa suala la uadilifu, wizi na udokozi wa mali ya umma au rushwa," alisema Kinana.
Kinana alitumia nafasi hiyo kumwomba Lowassa kuisaidia CCM katika kushawishi wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kufuta au kufanyia marekebisho sheria zote zisizo na manufaa kwa wananchi na hasa zile zinazosababisha kuibuka kwa kodi na ushuru kero
kwa wananchi.
"Sheria zinaundwa kwa manufaa ya wananchi na si wanyama. Kama zipo sheria zinaifanya jamii ilalamike au inawapokonya wananchi haki zao, basi sheria hiyo itakuwa haifai na ni vema ndugu yangu Lowassa ukanisaidie katika kulishawishi Bunge kuzifuta sheria za aina hii," alisema Kinana.
Akizungumza na wakazi hao wa Mto wa Mbu, Nape alisema kazi iliyofanywa na Lowassa katika kuliletea maendeleo jimbo hilo ni kubwa.
Pia, alitumia muda mrefu kusifu uadilifu, uhodari na uchapakazi wa Mbunge wa zamani wa Jimbo hilo la Monduli na Waziri Mkuu wa zamani, Edward Sokoine, kuwa akishirikiana na viongozi wengine, alijenga misingi ya kuwafanya viongozi wa umma kuwa waadilifu na jasiri katika kufikia uamuzi kwa masuala ya kitaifa.

No comments: