HATIMA YA CHENGE NA WENZAKE MIKONONI MWA RAIS


Hatima ya tuhuma za Mbunge wa Bariadi Magharibi, Andrew Chenge na wenzake kuhusu fedha walizopata kutoka iliyokuwa akaunti ya Tegeta Escrow, iliyokuwa Benki Kuu (BoT), itapelekwa kwa Rais Jakaya Kikwete.

Ofisa Sheria Mkuu wa Sekretarieti ya Maadili, Filotheus Manula, ameliambia mwandishi kuwa, baada ya Baraza la Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kukusanya tuhuma pamoja na utetezi wa pande zote mbili, limeandika ripoti na utetezi na kuuwasilisha kwa Rais ambaye ndiye mwenye maamuzi ya kutoa hukumu.
 Alisema wao wamemaliza vikao vyao na kinachoendelea ni kuandaa ripoti ambayo baraza hilo litaeleza kwa nini liliamua kumpeleka mshitakiwa ndani ya baraza na mapendekezo ya hatua za kuchukuliwa pamoja na utetezi wa watuhumiwa hao.
“Baada ya kupeleka majumuisho yetu, uamuzi wa hukumu uko kwa Rais kwani baraza halina uwezo wa kutoa hukumu na ndiyo inavyofanyika kwa miaka yote,” alisema.
Chenge alipanda katika kizimba cha Baraza la Maadili, kujibu mashitaka ya kutumia madaraka yake vibaya alipokuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali na kushauri Serikali iingie mkataba wa miaka 20 na kampuni ya IPTL.
Aidha, anadaiwa baada ya kustaafu wadhifa huo wa uanasheria wa Serikali Desemba 24, mwaka 2005, mwaka 2006 aliingia mkataba wa kuwa mshauri mwelekezi wa kampuni wa VIP Engineering and Marketing Limited iliyokuwa na hisa za asilimia 30 kwenye kampuni ya IPTL na kujipatia Sh bilioni 1.6.
Baada ya kusomewa mashitaka hayo, mbunge huyo alikataa kesi hiyo kusikilizwa na kuwasilisha pingamizi la kutaka suala hilo kutoendelea kusikilizwa kwa kuwa tayari kuna kesi ya msingi Mahakama Kuu inayoendelea kusikilizwa.
Naye  Profesa Anna Tibaijuka, aliitwa katika Baraza la Maadili kwa viongozi wa umma  kujibu tuhuma za kukiuka maadili ya uongozi na kujipatia Sh bilioni 1.6 ambazo aligawiwa kutoka katika fedha za akaunti ya Tegeta Escrow.
Hata hivyo, Profesa Tibaijuka alikana mashitaka hayo, na kusisitiza kuwa hakukiuka maadili hayo ya viongozi wa umma, kwa kuwa fedha hizo hakuziomba kwa maslahi yake binafsi, bali kwa ajili ya kuendeleza na kuboresha taasisi yake inayotoa huduma ya elimu kwa watoto wa kike wasio na uwezo lakini wenye vipaji.
Mbunge wa Sengerema, William Ngeleja, alikiri mbele ya Baraza la Maadili ya Viongozi wa Umma kwamba, aliomba na   Sh milioni 40.4, kutoka kwa James Rugemalira kwa kujitetea, alifanya hivyo kama ilivyo kawaida pia kwa wabunge wengine.
Ngeleja alidai mbele ya baraza hilo kwamba, msaada huo aliopewa na Rugemalira, hauna tofauti na mingine aliyowahi kupokea kutoka kwa wafanyabiashara wakubwa kama vile Reginald Mengi, Said Salim Bakhresa na Yusuf Manji.
Wengine ambao taarifa zao zitapelekwa kwa Kikwete, ni Mnikulu Shaban Gurumo, Mkurugenzi wa Sheria wa Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Rugonzibwa Mujunangoma, Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Ufilisi na Udhamini (RITA), Philip  Saliboko, Naibu Kamishna Upelelezi na Kodi Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Loicy Appollo.
 Pia yumo Mkurugenzi  Mdhibiti  Uchumi Mamlaka ya Usafiri wa Anga, Dk Benedict Diu  na Meya wa Halmashauri ya Manispaa ya Tabora, Gulam Remtullah.

No comments: