Chama
cha Walimu Tanzania (CWT) kinakusudia kuanzisha benki yake kwa kishindo, hivyo
kuwataka walimu na wananchi kujitokeza kununua hisa za benki ya walimu.
Uuzaji
wa hisa hizo unatarajiwa kufanyika kuanzia Machi 23 hadi Mei 4 mwaka huu baada
ya taratibu za ufunguzi wa benki hiyo kufikia hatua za mwisho.
Akizungumza
Rais CWT, Gratian Mukoba (pichani) alisema maombi ya kuuzwa kwa hisa hizo yameshakubaliwa
na Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA), hivyo waraka wa matarajio
utatolewa na kusambazwa nchi nzima mwezi huu kabla ya mauzo kuanza.
Alisema baada
ya kupata kibali hicho, benki hiyo itaanza na mtaji mkubwa unaozidi Sh
bilioni 25, kwani mtaji wa chini wa kuanzisha benki ya biashara hapa nchini
ni Sh bilioni 15.
Aliongeza
kuwa hisa hizo, zitauzwa kwa wiki sita na baada ya hapo majina ya wanahisa
yatapelekwa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) kwa ajili ya uhakiki na benki kupatiwa
leseni yake, ianze biashara na hisa zitaorodheshwa kwenye Soko la Hisa Juni
mwaka huu.
Aidha, chama hicho kimeweka kivutio kwa walimu cha
Sh 50,000 kwa kila aliye hai katika malipo yake kwa chama. Hali hiyo
itawawezesha kununua hisa 100 katika benki, ambacho ndicho kiwango cha chini,
hivyo kuwataka walimu wanunue hisa kwa wingi ili kuongeza mtaji wa benki.
Alisema
ili kuhakikisha uuzaji wa hisa unamfikia kila Mtanzania wameamua kuweka
utaratibu wa kununua kwa njia ya simu za mkononi kwa kushirikiana na kampuni ya
MaxMalipo na kwenye ofisi za madalali wa soko la hisa na matawi yote ya benki
ya CRDB nchi nzima.
Aidha,
alisema mpaka sasa walimu waliopo ni zaidi ya 200,000 na lengo lao likiwa ni watu
300,000, ambao ni walimu na wananchi wa kawaida.
Pia,
aliomba wanachama wa chama hicho na wananchi wajitayarishe ili ifikapo Machi
23, waanze kununua hisa kwa wingi ili kumiliki benki hiyo kwa faida ya nchi.
No comments:
Post a Comment