BASI LAPINDUKA HIFADHI YA MIKUMI NA KUUA

Watu saba ambao wote ni wanaume wamekufa papo hapo na wengine 17 kujeruhiwa baada ya basi walilokuwa wakisafiria kutoka Dar es Salaam kwenda mjini Ifakara, wilayani Kilombero mkoani Morogoro kupinduka ndani ya hifadhi ya Taifa ya Mikumi katika  barabara kuu ya Morogoro – Iringa.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Morogoro, Leonard Paulo, alithibitisha jana kutokea kwa ajali hiyo majira ya saa sita mchana maeneo ya hifadhi ya Taifa ya Mikumi, wilayani Kilosa kwenye barabara kuu ya Morogoro- Iringa  wakati basi hilo likitaka kulipita lori lililokuwa mbele yake na kukosa mwelekeo.
Kwa mujibu wa Kamanda Paulo, basi hilo lenye namba za usajili T 637 CDC aina ya Tata, mali ya Kampuni ya Msanga Line Express lililokuwa likiendeshwa na Saleh Rajabu (42), likitokea Dar es Salaam kwenda Ifakara, wilayani Kilombero, mkoani Morogoro.
Akielezea chanzo cha ajali hiyo, alisema wakati mvua inanyesha gari hilo lililazimisha kulipita lori lililokuwa mbele yake lililokuwa likielekea Iringa, ndipo gari hilo likakosa mwelekeo, kupinduka na kusababisha vifo vya watu saba na kujeruhi wengine 17 waliokimbizwa Hospitali ya Mtakatifu Kizito, Mikumi huku miili ikihifadhiwa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro.
Hii itakuwa ni ajali ya pili kutokea ndani ya hifadhi ya Taifa ya Mikumi, ambapo Machi 17, mwaka huu, watu wawili walifariki dunia papo hapo na wengine 18 kujeruhiwa baada ya kutokea ajali ya barabarani baina ya basi la FM Safari na Mitsubishi Fuso katika barabara kuu ya Morogoro – Iringa.

No comments: