BASI LA OSAKA LAGONGA LORI LIKIWA NA ABIRIA 57 DODOMA

Abiria 57 wa basi la Osaka lililokuwa linatoka Bukoba kwenda Dar es  Salaam wamenusurika kifo baada ya basi hilo kugonga tela la lori lililokuwa limeegeshwa kutokana na kuwa bovu na kutumbukia mtaroni.

Ajali hiyo iliyotokea katika barabara kuu Dodoma/Morogoro eneo la Chuo cha Biashara (CBE) Kata ya Makole Manispaa ya Dodoma kwenye makutano ya barabara maarufu kama kona ya Dodoma Inn, majira yanayokaribia saa sita usiku.
Imeelezwa kuwa dereva wa basi hilo lenye namba za usajili T. 197 BUS Scania, Said Chaupendo Mshana (33) aligonga tela hilo lenye namba za usajili T. 533 BNM la gari lenye namba za usajili T. 426 BMJ Scania lililokuwa likiendeshwa na Idd Juma (41) lililokuwa limeharibika, kabla hajatumbukia mtaroni na kujeruhi abiria mmoja.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, David Misime alisema kwamba basi hilo la Osaka baada ya kushusha abiria stendi kuu ya mabasi Dodoma liliondoka likiwa katika mwendokasi na kushindwa kusimama pamoja na kusimamishwa na askari wa usalama barabarani waliokuwa kwenye eneo ambalo lori limeharibika.
“Kutokana na mwendokasi, aliligonga  tela kisha kutumbukia mtaroni pembeni mwa barabara katika uzio wa Chuo cha Biashara (CBE) na kusababisha majeruhi kwa abiria mmoja aliyefahamika kwa jina la Justa Trazias mwenye miaka 19,  mkazi wa Ubungo River side Dare es Salaam ambaye amelazwa katika hospitali ya rufaa Dodoma kwa matibabu na hali yake inaendelea vizuri,” alisema Kamanda Misime.
Kamanda Misime alisema uchunguzi wa awali unaonesha kwamba chanzo cha ajali hiyo ni uzembe wa dereva, mwendokasi na kukataa kutii amri ya askari aliposimamishwa kisha kushindwa kulimudu gari na kusababisha ajali hiyo.
Kamanda huyo ametoa mwito kwa madereva kuwa na udereva wa kujihami na wenye kuchukua tahadhari na kufuata sheria kwa kutokiuka agizo la mabasi kutotembea baada ya saa sita usiku.
“Kwa  muda huo alitakiwa walale stendi ya mabasi Dodoma na ndiyo maana aliposimamishwa na askari alikataa kusimama na matokeo yake akasababisha ajali hii,” alisema Kamanda Misime.

No comments: