Watendaji wa Halmashauri waliokaa kwenye vituo
vya kazi kwa zaidi ya miaka 10, wataanza kuhamishwa wakati wowote kuanzia sasa
kuleta ufanisi katika utendaji na kukomesha
kufanya kazi kwa mazoea.
Waziri Mkuu, Mizengo Pinda (pichani) ameagiza ofisi za
mikoa ziainishe majina ya watendaji husika, utaratibu wa kuwahamisha ufanyike
kunusuru utendaji wa kazi kwenye maeneo walikokaa muda mrefu.
Alitoa agizo hilo juzi wilayani Mufindi katika
mkoa wa Iringa. Alisema serikali imebaini watendaji wanaokaa kwenye vituo vya
kazi kwa miaka 10 na zaidi kwenye
halmashauri, wanakuwa kikwazo cha utendaji kazi wenye ufanisi kutokana na
kufanya kazi kwa mazoea badala ya kitaalamu.
Alisema, “Niliwahi kwenda kutembelea
halmashauri fulani nikamkuta mzee mmoja amekaa hovyo kwa kujiachia achia tu na
kusahau kuwa ni mtendaji wa serikali. Ilibidi nimuulize, mzee nawe umo, akasema
, ndio mheshimiwa. Nikashangaa, hata huyu! Kwa jinsi hivi alivyo atafanya kazi
vizuri kweli?”
“…Nilipomwuliza nilipata majibu
yaliyodhihirisha kuwa alikuwa alivyo na kutenda kazi kwa mtindo aliokuwa
akiufuata kwa sababu ya mazoea yaliyotokana na kuwepo kwenye halmashauri husika
kwa zaidi ya miaka 10, hii haikubaliki kwa watendaji wa halmashauri”.
Pinda alisisitiza, kuwepo kituoni kwa muda
mrefu kwa watendaji katika halmashauri ni miongoni mwa udhaifu unaotoa mwanya
wa wizi wa fedha za halmashauri kwa sababu wanakuwa wakifahamu mbinu za kuiba
na jinsi ya kukwepa kujulikana uhusika.
“Huu ni ukweli na ushahidi tumeuona katika
maeneo ambako watumishi walikuwa wakiiba fedha. Kuwapangua kulisaidia sana
kunusuru fedha zisiibwe katika baadhi ya halmashauri zilizokuwa na matatizo ya
kifedha kutokana na wizi wakati wa kukusanya kodi na ushuru mbalimbali,”
alisema Waziri Mkuu.
Katika mkutano huo, alimtaka Mkuu wa Mkoa wa
Iringa, Amina Masenza kuandaa orodha ya watumishi wa mkoa huo waliokaa kwenye
nafasi za ajira kwa zaidi ya miaka 10 na kumpelekea wafanyiwe utaratibu wa kuhamishiwa vituo
vingine.
“Tafuta wote waliokaa zaidi ya miaka 10. Ni
lazima tuwabadilishe... niletee orodha mapema iwezekanavyo,” alisema Waziri
Mkuu.
Alisema nia ya mchakato huo ni kuongeza
ufanisi kwani watumishi wakikaa sehemu moja kwa muda mrefu, wanakuwa butu kwa
kukosa ubunifu kwenye kazi zao, wanaota mizizi na kugeuka kuwa chanzo cha
matatizo katika baadhi ya maeneo.
Wakati huo huo, ameagiza uwekwe uwiano wa
idadi ya walimu katika shule zote za sekondari, kulingana na mahitaji kwa
kuhamisha walimu wa ziada kutoka katika maeneo walipo sasa, kwenda kwenye
maeneo yenye upungufu.
Alisema, “Kuna maeneo nimeona walimu wanakula
bwerere tu kwa sababu wako wengi sana. Hawa inabidi wapunguzwe na kupelekwa
kwenye shule zisizo na walimu, shushu hiyo haihitajiki kwa sababu kuna wengine wanakosa wa
kuwafundisha ilhali wamelundikana eneo moja”.
Jumapili wakati akizungumza na wakazi wa kata
ya Ipogolo, nje kidogo ya mji wa Iringa, Pinda alimtaka Mkurugenzi wa Manispaa
ya Iringa, Ahmed Sawa kukaa pamoja na
Ofisa Elimu wake wapunguze walimu 230 waliozidi mahitaji kwenye manispaa hiyo,
badala yake wawapangie kwenda vijijini.
“Manispaa inahitaji walimu 534 lakini waliopo
ni 764. Hapa kuna ziada ya walimu 230 tena kwenye shule za msingi... Mkurugenzi
kaa na Ofisa Elimu wako muwaondoe walimu waliozidi na kuwapangia waende
vijijini ambako kuna mahitaji zaidi,” alisema.
“Kwa
upande wa shule binafsi nako pia tatizo ni lile lile. Walimu wamezidi. Mahitaji
ni walimu 75 waliopo ni walimu 142 ... wanaozidi ni walimu 67,” alisema Waziri
Mkuu.
Aliendelea kusema, “Sina tatizo na walimu wa
shule binafsi kwa sababu wao wana mfumo wao wa ajira lakini hawa wa shule za
Serikali ni lazima muwaondoe tena haraka sana. Waondoeni waende vijijini kwenye
mahitaji makubwa sababu ualimu ni ualimu tu, siyo lazima mtu awe mjini ndiyo
afundishe vizuri.”
No comments:
Post a Comment