Chama cha Kutetea Abiria Tanzania
(CHAKUA) kimewaomba Waziri wa Uchukuzi,
Samuel Sita kuingilia kati na kuagiza
Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (SUMATRA), isikilize
kilio cha wananchi kuhusu kupunguzwa kwa
nauli.
Hayo yalisemwa jana na mwenyekiti wa chama hicho, Hassan Mchanjama wakati
akizungumza na waandishi wa habari jiji Dar es Salaam.
Alisema wamefikia uamuzi huo baada ya Ewura
kushusha bei ya mafuta, hivyo ni vyema na abiria nao wakanufaika kutokana na
mafuta kushuka tangu mwaka jana Desemba, kwani inaonekana wanaonufaika ni
wamiliki wa vyombo vya usafiri.
Aliongeza kuwa imekua ikishuhudiwa mara kwa
mara mafuta yakipanda kidogo, nauli nazo zinapanda haraka, lakini mafuta
yakishuka Sumatra hawataki kuitisha mkutano
na wadau ili kujadili kushusha nauli .
“Sisi Chakua tumechukua hatua ya kwanza
kuwaandikia barua, lakini Sumatra ipo kimya tukaandika tena Februari 5, lakini
bado wamekaa kimya,” alisema Mchanjama.
Alisema Chakua inataka nauli zote zipungue kwa
asilimia 25, kwa mfano nauli za daladala chini ya kilometa 10 nauli ya sasa ni
Sh 400 hivyo ipungue hadi Sh 300 na mikoani nauli ipungue kwa asilimia 25.
Alisema nauli ikipungua itasaidia kupunguza
bei za bidhaa nyingine ikiwemo vyakula, kwani mfumko wa bei unachangiwa na
gharama za usafirishaji.
Katibu wa Barabara wa chama hicho, Gervas
Rutaguzinda aliitaka serikali kujenga vibanda vya kupumzikia abiria katika
Kituo Kikuu cha Mabasi Ubungo, kwani kila abiria anayeingia katika
kituo hicho analipa Sh 200. Alisema pesa zinazokusanywa kila siku na kituo
hicho ni nyingi, lakini kwamba hakuna vibanda muda mrefu.
“Abiria wananyimwa haki wanakaa kwenye jua
kali na mvua hakuna pa kusimama wakati wanalipa kiingilio ni jambo la aibu na
lazima watakuwa wanajiuliza ni wapi fedha hizo zinapelekwa wakati hakuna
maendeleo yoyote,” alisema Rutaguzinda.
No comments:
Post a Comment