Wakati serikali ikianza kutafuta suluhisho la kudumu la matatizo wafanyabiashara ndogo,
mama lishe kuhusu upatikanaji wa maeneo, imebainika kuwapo mchezo ‘mchafu’ wa
wafanyabiashara wakubwa kutumia mgongo wa wamachinga, kusambaza na kuuza bidhaa zao maeneo yasiyoruhusiwa.
Katika Manispaa ya Kinondoni, Dar es Salaam, imebainika yako maghala 12 ya bidhaa za
chakula eneo la Ubungo, ambako wafanyabiashara ndogo wamekuwa wakigawiwa bidhaa
kuziuza maeneo yasiyoruhusiwa na kisha jioni hupeleka hesabu kwa matajiri kwa
ujira mdogo.
Msemaji wa Manispaa ya Kinondoni, Sebastian Mhowera alisema wamebaini
tatizo hilo na wanapaswa kulizingatia wakati wa kutekeleza mpango wa serikali
kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), wa
kusaidia wamachinga kufanya biashara zao kwa amani kwenye maeneo
yanayoruhusiwa.
Aidha, katika kutekeleza azma hiyo ya Tamisemi, Manipsaa ya Ilala imeainisha maeneo kadhaa, ikiwemo Viwanja
vya Jangwani ambako itajengwa
miundombinu kama vile vyoo, taa na kuwekewa ulinzi, litumike kwa ajili ya soko la kila siku.
Hatua hizo za halmashauri za jijini Dar es Salaam, ni utekelezaji kwa vitendo mpango aliosema
Waziri Mkuu, Mizengo Pinda katika
mkutano wa 18 wa Bunge ulioahirishwa hivi karibuni.
Pinda alisema kimeundwa kikosi
cha kiofisi kitakachohusisha wajasiriamali hao kwa lengo la kukubaliana kuhusu
maeneo na muda muafaka wa kuendesha shughuli zao. Wameanzia jiji la Dar es
Salaam kabla ya kwenda miji na majiji mengine.
Msemaji wa Manispaa ya Kinondoni, Mhowera alisema, “tumebaini wengi wa
wanaofanya biashara maeneo yasiyoruhusiwa siyo wamachinga, bali ni vibaraka wa
wafanyabiashara wakubwa wenye maduka na maghala makubwa.”
“Mfano pale Ubungo, tumebaini kuna maghala 12, ya wafanyabiashara
wanaotoa bidhaa za mazao ya chakula mikoani na wanawaajiri watu ambao kila siku
huenda kwenye maghala hayo kuchukua bidhaa na kuzipanga barabarani na jioni
hurudisha hesabu kwa ujira mdogo, sasa hao ni machinga kweli?” alisema Mhowera.
Alisema iko haja ya kuchukua hatua kudhibiti wafanyabiashara
wakubwa wanaofanya mbinu chafu ionekane
ni machinga na hivyo kukwepa kuuza
kwenye masoko kisheria.
Alisema wanafahamu yaliko maghala hayo. Alisema katika utekelezaji wa
azma ya kusaidia wafanyabiashara ndogo, watahakikisha watu hao wanatenganishwa,
kwani wanatumia mgongo wa wamachinga kuongeza tatizo la watu kufanya biashara
kwenye maeneo yasiyoruhusiwa kwa manufaa yao.
Ofisa huyo wa manispaa alisema walifanya utafiti kwenye maeneo yote,
ambayo watu hufanya biashara barabarani na kubaini wapo wafanyabiashara wasio
rasmi zaidi ya 3,400 .
Utafiti ulibaini wengi wao walipewa maeneo kwenye vizimba katika masoko
mbalimbali yanayokubalika kisheria
kufanyia biashara ingawa baadhi yao, wanaendelea kufanya biashara maeneo.
“Mifano ni mingi.., kuna mama
mmoja (alimtaja jina) huyu tulimbaini na
tulikuwa naye wakati tunafanya tathimini ya wanaofanya biashara maeneo holela
na yeye tulimgawia eneo Soko la Makumbusho na pia ana eneo Soko la Shekilango, ila bado yuko
barabarani pale Ubungo, ndio anajiita Mwenyekiti wa wafanyabiashara maeneo
yasiyoruhusiwa.
“Na sasa anataka apewe tena eneo tulilotenga la soko pale Kituo cha
Mabasi cha Mawasiliano, sasa utasema na huyo naye ni eneo kakosa”, alisema
Mhowera.
Mkurugenzi wa Manispaa ya Ilala, Isaya Mngulumi alisema kwa upande wao
wameanza utekelezaji kwa kutenga maeneo kwa kuzingatia upatikanaji wa wateja,
ulinzi, miundombinu na usalama.
Alisema viwanja vya Jangwani kwa
upande wa mmoja wa karibu na Klabu ya Yanga, vitatumika kwa soko la kila siku
na litajengewa miundombinu muhimu kama vile taa, vyoo na kuwekewa ulinzi.
Alisema pia siku zijazo, eneo hilo litajengwa maegesho ya magari ambayo
wamiliki watapata fursa ya kununua bidhaa kabla ya kuondoka na magari yao.
“Kwa siku za usoni eneo la Jangwani litajengwa maegesho ya magari
binafsi kwani hayataruhusiwa kuingia katikati ya mjini, na hiyo ni fursa kwa
wafanyabiashara katika soko hilo kupata wateja,” alisema Mngulumi.
Alitaja maeneo mengine yaliyotengwa ni Chanika, Pugu, Kigogo Fresh,
Mchikichini, Machinga Complex na Jangwani.
Alisema wanaendelea kufanya utafiti
wa maeneo mengine kuhakikisha wafanyabiashara wanaondoka kwenye maeneo
hatarishi na kufanya biashara kwenye maeneo yanayoruhusiwa.
Alisema pia Manispaa inaimarisha Vyama vya Akiba na Mikopo (Saccos),
viwe na mitaji mikubwa ya kukopesha wamachinga, waondokane na kunufaisha wenye maduka ya bidhaa za jumla
ambazo huuza kwa ujira mdogo.
“Hatutaki tena machinga wafanye
biashara kwa mali kauli ambayo mwisho wa siku anayefaidika ni mwenye mali na
siyo machinga, tunataka wawezeshwe wawe na mitaji na wanunue wenyewe bidhaa zao
na kuziuza kwa faida,” alisema Mngulumi.
Kwa upande wa Manispaa ya Temeke, msemaji wake, Joyce Msumba alisema
wametenga masoko kila kata na pia eneo la Zakhiem limetengwa kwa ajili ya
wafanyabiashara.
Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za
Mitaa(Tamisemi), Jumanne Sagini alisema kila halmashauri ilipewa mwongozo wa
kutenga maeneo kwa ajili ya wafanyabiashara ndogo na vijana.
“Tulitoa miongozi kwa halmashauri
zetu zote nchini kutenga maeneo ya vijana na wafanyabiashara ndogo na wengi
wametekeleza, ila wale waliotengwa kwenye maeneo hatarishi tumeyakataa kwani
siyo salama, na utekelezaji wake tumewaambia uanze mara moja,” alisema Sagini.
Alisema Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwekezaji na Uwezeshaji),
Christopher Chiza, ameshaanza kuchukua
hatua kwa kuzungumza na wafanyabiashara ndogo kuangalia namna ya kuwasaidia.
Alisema serikali kwa kuona umuhimu, mfano kwenye kituo kipya cha mabasi
madogo jijini Dar es Salaam cha Simu 2000 maarufu kama Mawasiliano, kumejengwa
pia soko kwa ajili ya wafanyabiashara ndogo.
Akizungumzia masoko ya Jumapili, Sagini alisema yanafanyiwa utafiti yatakapotengwa yawe na
miundombinu. Hata hivyo alisema masoko hayo hayatakuwa kila sehemu isipokuwa ni
baada ya kupata tathmini nzuri ya maeneo.
No comments:
Post a Comment