WALIOFAULU LA SABA WATAKIWA KURIPOTI KABLA YA MACHI 28


Serikali imeagiza wakuu wote wa mikoa, kuweka mikakati ya kuhakikisha watoto wote waliofaulu mitihani ya darasa la saba, wanajiunga na shule za sekondari katika kipindi hiki kabla ya Machi 28 mwaka huu, vinginevyo watakaokwamisha watoto hao watachukuliwa hatua kali.

Agizo hilo limetolewa na Naibu Waziri Ofisi ya Waziri MkuuTawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) anayeshughulikia Elimu, Kasimu Majaliwa katika kikao cha Kamati ya Ushauri ya Mkoa wa Tabora (RCC), kilichoketi katika ukumbi wa Mtemi Isike Mwanakiyungi mjini hapa juzi.
Alisema kila mkoa unatakiwa kujiwekea mkakati wa kuhakikisha watoto wote, waliochaguliwa kujiunga kidato cha kwanza katika shule mbalimbali za sekondari wanaripoti ili wasipoteze fursa hii muhimu waliyopata kwa kisingizio cha namna yoyote ile iwe wazazi au vinginevyo.
‘Ili zoezi hili liende vizuri na watoto wote waripoti kwa asilimia 100, suala la usimamizi  ni la muhimu sana na kila halmashauri inapaswa kutekeleza wajibu wake ipasavyo, vinginevyo mtakuwa mnakwamisha malengo ya serikali ya kufanikisha mpango wa matokeo makubwa sasa’, aliongeza.
Aliagiza wakuu wa mikoa, wakuu wa wilaya  na wakurugenzi wa halmashauri zote, kuhakikisha kila mzazi au mlezi atakayehusika kwa namna moja au nyingine kukwamisha au kuzuia mtoto wake kujiunga shule ya sekondari, anachukuliwa hatua kali mara moja ikiwemo kufikishwa katika vyombo vya sheria.

No comments: