Wajawazito
wakazi wa kata za Sululu na Matawale
katika Halmashauri ya Mji wa Masasi
mkoani Mtwara, wamekuwa wanajifungua kwa kutumia vibatari muda wa usiku zaidi ya miaka mitano sasa.
Diwani wa
Kata ya Sululu, Peter Mrope alisema hayo alipokuwa akizungumza na
mwandishi wa habari hizi.
Alisema
kuwa hali ya zahanati sio nzuri na zaidi ya miaka mitano wakazi wake na kata ya
jirani ya Matawale, wanapougua au kujifungua wakati wa usiku, wauguzi na
madaktari wanatumia vibatari ili wapate kumhudumia mgonjwa aliyefika muda huo.
Alisema zahanati hiyo iliyopo kijiji cha Makalani, haina huduma za umeme au nishati ya
jua, kiasi huduma za afya kuzorota.
Mrope alisema baadhi ya wauguzi na
watumishi hawaipendi zahanati hiyo,
kutokana miundombinu yake sio rafiki kwa watumishi.
Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji wa Masasi,
Andrew Mtumisha alikiri kuwapo tatizo la ukosefu wa huduma ya umeme,
linalosababisha wajawazito na wagonjwa wa magonjwa mbalimbali kutibiwa kwa
kutumia vibatari katika zahanati ya Sululu.
Alisema tatizo hilo ni la muda mrefu. Alisema
hakuna miundombinu ya umeme tangu
zahanati ikiwa katika Halmashauri ya wilaya ya Masasi mkoani Mtwara.
Alisema
baada ya kugawa maeneo ya mipaka
na utawala kati ya Halmashauri ya Mji na
Halmashauri ya wilaya, kata ya Sululu ilipangwa kuwa ya Halmashauri ya Mji wa
Masasi mwaka 2012.
Alisema kipindi hicho, Mfuko wa Jimbo ambao uko
chini ya Mbunge wa jimbo ulishaanza, lakini zahanati hiyo haijapata nishati ya
jua ili kuondoa tatizo la wagonjwa
kujifungua kwa kutumia vibatari.
Alisema ofisi ya Mbunge na Uongozi wa Mfuko wa
Jimbo, unapaswa kukagua maendeleo ya zahanati hiyo na kuweza kubaini tatizo hilo.
Alisema kikao cha Baraza la Madiwani cha Januari
30, mwaka huu kiliagiza Ofisi ya Mkurugenzi kununua na kuweka umeme wa jua kwa muda wa mwezi mmoja.
Mkurugenzi wa
Mji wa Masasi, Fortunatus Kaguro alikiri kupewa maazimio ya kwenye kikao
cha Baraza la Madiwani kununua nishati ya jua.
No comments:
Post a Comment