Vijana
waliohitimu mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa (JKT), wanatarajia kufanya
maandamano ya siku tatu mfululizo usiku na mchana jijini Dar es Salaam kuanzia
Jumatatu ijayo, kushinikiza kuonana na Rais Jakaya Kikwete kumweleza matatizo
ya ajira wanayokabiliana nayo.
Wahitimu
hao jana walifanya mkutano katika eneo la Msimbazi Centre, Dar es Salaam na
Mwenyekiti wa Vijana waliohitimu mafunzo ya JKT, George Mgoba alisema kwa muda
mrefu wamekuwa wakiomba kukutana na Rais
ili wamueleze matatizo wanayokumbana nayo, lakini wamekuwa wakipewa ahadi za
uongo na Katibu Mkuu wa Rais.
“Tumeomba
mara nyingi kukutana na Rais na tumekuwa tukiandika barua, lakini hatujibiwi chochote.
Tunajua hizi ni njama tu za watu wachache wanaozuia tusionane na Rais,” alidai
Mgoba.
Alidai
kuwa wameandika barua nyingine na hivi karibuni
Katibu wa Rais aliwapigia simu kuwa wafike Februari 10 ili waonane na
Rais na walipofika, hawakufanikiwa kumuona
Katibu huyo.
Akizungumzia sababu za kutaka kuonana na Rais, alidai ni
kutaka kujua hatma yao ya kutopatiwa ajira kutokana na mafunzo ya kijeshi
waliyoyapata. “Sisi tumepatiwa mafunzo ya kijeshi na sasa tupo uraiani kwa
ajili gani? Hawa wote unaowaona ni askari tayari ” alidai.
Mkutano
wao uliwakutanisha pamoja ili kuweka mikakati yao ikiwa ni pamoja na kufanya
maandamano ifikapo Jumatatu kama serikali haijajibu, kama itawaajiri au hapana.
Walidai endapo jibu halitapatikana, basi watafanya maandamano ya siku tatu
mfululizo hadi ombi lao la kumwona Rais lifanikiwe.
Makamu
Mwenyekiti, Paral Kiwango, alisema jambo hilo linaonekana kuwa na upendeleo
mkubwa, kwani wenzao wa upande wa Zanzibar wote waliomaliza mafunzo ya JKT,
wanapatiwa ajira. Alihoji iweje vijana
wa Bara wametelekezwa?
“Wenzetu
wa upande wa Zanzibar wakimaliza mafunzo wote wanaajiriwa, lakini sisi Tanzania
Bara hakuna anayetujali na kututhamini,” alidai Kiwango.
Kwa
upande wake, Katibu wao Liwus Emmaneul amesema kuna fursa nyingi za ajira hapa
nchini kama vile TANAPA na sehemu zingine, ambazo wao wanaweza kufanya kazi;
lakini wanaoajiriwa kule ni watu wengine wasiokuwa hata na ujuzi, huku wao
wakitelekezwa na wakiomba ajira kule hawathaminiwi, kama watu wenye maadili na
mafunzo.
Kamanda
wa Polisi wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova alipotafutwa ili
atoe ufafanuzi juu ya maandamano hayo, simu yake ya mkononi iliita bila majibu.
No comments:
Post a Comment