Waziri Mkuu
Mizengo Pinda, amesema Serikali imepanga kuajiri walimu zaidi ya 35,000 kwa
ajili ya shule za sekondari, ili kukabiliana na tatizo la uhaba wa walimu
nchini.
Alitoa kauli
hiyo jioni wakati akizungumza na mamia ya wakazi wa kata ya Kiwere, baada ya
kukagua ujenzi wa maabara na kuzindua nyumba nne za walimu kwenye Shule ya
Sekondari ya Kiwere, tarafa ya Kalenga, wilayani Iringa.
Waziri Mkuu
alisema walimu hao watagawanywa kwenye shule kulingana na mahitaji
yaliyokwishawasilishwa na watakapopata
mgawo wao, hawana budi kuangalia kwanza shule zenye miundombinu iliyokamilika
kama ilivyo kwa shule hiyo.
Akifafanua
kuhusu kasi ya ujenzi wa maabara, Waziri Mkuu alisema: “Mkoa mzima wa Iringa
unahitaji maabara 318 na zilizo tayari mpaka sasa ni 108.
“Lakini kuna
nyingine 141 ambazo zimekwishaanza kujengwa na zimefikia hatua nzuri.
Nimeambiwa katika muda mfupi ujao kutakuwa na maabara 249 zilizokamilika,”
alisema.
“RC inabidi
uwasukume watu wako ili hizi 69 ambazo hazijaanza kujengwa zikamilike kabla ya
Juni mwaka huu kama ambavyo Rais Jakaya Kikwete alivyoelekeza. Alisema
hataongeza tena muda wa ujenzi,” aliongeza.
Alisema elimu
ni sekta ya msingi ambayo Serikali imeamua kuipa umuhimu wa kipekee na kuiweka
katika moja ya maeneo sita muhimu ya kipaumbele chini ya Mpango wa Matokeo
Makubwa ya Haraka (BRN).
Waziri Mkuu
aliwataka wanafunzi wa shule hiyo wasome kwa bidii na wawe wasikivu, ili
wafanye vizuri zaidi kwenye masomo yao.
Mapema, akitoa
taarifa mbele ya Waziri Mkuu, Ofisa Elimu wa Wilaya ya Iringa, Leonard Msigwa,
alisema ujenzi wa nyumba hizo nne zenye pande mbili, umegharimu Sh milioni
323.2.
Alisema nyumba
hizo zenye vyumba vitatu vya kulala, sebule na jiko, zina uwezo wa kubeba
familia nane.
Msigwa alisema
ujenzi wa nyumba hizo ulifanywa na shirika la Deswos la Ujerumani kwa
kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Iringa pamoja na wananchi.
Pia walisaidiwa
kujengewa tangi la maji na mabweni mawili yenye uwezo wa kuchukua wanafunzi 112
kila moja kwa ajili ya wasichana.
Akifafanua
kuhusu hali ya ujenzi wa maabara, Ofisa Elimu huyo alisema hadi sasa
wamekamilisha ujenzi wa vyumba viwili vya Kemia na Bayoolojia, lakini bado viko
kwenye hatua ya kupaka rangi. Aidha mfumo wa gesi na maji umekwishafungwa ndani
ya vyumba vya maabara.
“Ujenzi wa
maabara hadi sasa umekwisha gharimu Sh milioni 52.8/- na kwa Februari 2015,
tumefanikiwa kutengeneza baadhi ya samani za maabara yaani meza 24 na stuli 96
zenye thamani ya Sh milioni 8.9,” alisema.
No comments:
Post a Comment