OMBI LA MARANDA WA EPA KUSIKILIZWA FEBRUARI 18


Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imepanga Februari 18, mwaka huu kusikiliza ombi la kwenda kutibiwa nchini India, lililowasilishwa na mshitakiwa wa kesi ya wizi wa Sh milioni 207 katika Benki Kuu (BoT) kupitia Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA) Rajab Maranda.

Kesi hiyo ilitajwa kwa ajili ya kusikiliza ombi hilo lakini Hakimu Mkazi Frank Moshi, aliahirisha kwa kuwa jopo la mahakimu wanaosikiliza kesi hiyo halikukamilika.
Awali Wakili wa Serikali, Shadrack Kimaro alidai kesi imetajwa kwa ajili ya kusikiliza ombi la Maranda (pichani) lakini aliomba Mahakama ipange tarehe nyingine ya kutajwa kwa kuwa jopo linalosikiliza kesi halikufika.
Aidha upande wa utetezi uliomba Mahakama itoe kibali kwa mshitakiwa Farijala Hussein kupewa kibali cha kusafiri. Hakimu Moshi alisema hawezi kutoa kibali hicho na kuwashauri wawasilishe ombi hilo mbele ya jopo la mahakimu linalosikiliza kesi hiyo.
Washitakiwa wengine katika kesi hiyo ni Imani Mwakosya, Esther Komu na Bosco Kimela. Wanakabiliwa na mashitaka ya kuwasilisha nyaraka za uongo, kughushi, kuiba Sh milioni 207 kutoka BoT na kusababisha hasara ya fedha hizo.
Inadaiwa kuwa washitakiwa walighushi nyaraka, ambazo ni pamoja na hati za makubaliano ya kuhamishiwa deni kutoka Kampuni ya General Marketing ya India kwenda Kampuni ya Rashaz (T) ya Tanzania, ambazo walizitumia na kuiba fedha hizo.

No comments: