Mwanafunzi wa Darasa la Saba, Adam Abdul Sapi
(13) ametawazwa kuwa Chifu mpya wa Wahehe, akirithi nafasi ya baba yake,
aliyefariki na kuzikwa mkoani Iringa.
Rais
Jakaya Kikwete alishiriki maziko ya Chifu huyo wa Wahehe, Abdul Sapi
Mkwawa (66) yaliyokwenda sanjari na
hafla ya kumsimika mtoto huyo kushika wadhifa huo wa kimila.
Maziko ya kiongozi huyo aliyefariki Februari 14, mwaka huu,
yalifanyika katika kijiji cha Kalenga, nje kidogo ya mji wa Iringa ndani ya
makumbusho yaliyowekwa fuvu la babu
yake,Chifu Mkwavinyika Munyigumba Mwamuyinga Mkwawa.
Mbali na Rais Kikwete, wengine waliohudhuria
maziko hayo ambayo taratibu zake zilitumia takribani saa 2.30 kuanzia saa 7
mchana ni pamoja na Makamu Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwa upande
wa Tanzania Bara, Phillip Mangulla, wakuu wa mikoa ya Iringa na Mbeya na
viongozi mbalimbali wa serikali na vyama vya siasa.
Kabla ya kifo chake kilichosababishwa na
maradhi ya sukari na figo, Abdul Sapi Mkwawa aliyekuwa mtoto wa tatu wa Spika
wa kwanza mweusi nchini, Adam Sapi Mkwawa, alikuwa akifanyakazi katika kiwanda
cha maji Afrika cha Kidamali, Iringa.
Amewahi pia kufanyakazi katika Chama cha
Wazalishaji Tumbaku Iringa na Shirika la Elimu Supplies.
Alizaliwa Mei 4, 1949 katika kijiji cha
Kalenga na kupata elimu ya msingi katika shule za Kalenga na Tosamaganga kati
ya mwaka 1956 na 1963.
Mwaka 1964 hadi 1970 alijiunga na shule ya
sekondari Iyunga na Mkwawa, ambako alipata elimu ya kawaida na ya juu ya
sekondari kabla ya kujiunga na elimu ya juu ya biashara na utawala 1971 hadi
1973.
Mmmoja wa ndugu wa marehemu, Hussein Sapi
alisema mpaka umauti unamkuta, Abdul Sapi Mkwawa alikuwa mtwa (chifu); alisimikwa mwaka 1999 baada ya kifo cha baba
yake, Adam Sapi Mkwawa aliyefariki Juni 25, 1999.
Kabla ya maziko ya Chifu huyo, wazee wa kabila
la Wahehe walimsimika Adam ambaye ni mtoto wake wa tano kuwa chifu mpya wa
kabila hilo.
Hata hivyo, mtoto huyo anayesoma katika shule
ya msingi ya Highlands ya mjini Iringa, atalazimika kusubiri kufanya shughuli
za kichifu mpaka atakapotimiza umri wa miaka 20.
Tangazo lililotolewa mbele ya Rais na ndugu wa
karibu wa familia hiyo, Joseph Mungai, ilisema mdogo wa marehemu, Saleh
atashikilia wadhifa huo mpaka mtoto huyo atakapofikisha umri huo.
Baada ya maziko , Rais Kikwete na msafara wake
walizungumza na familia ya marehemu kijijini hapo.
No comments:
Post a Comment