MSHINDI WA TWEET YA MENGI ATANGAZWA


Mshindi wa Sh milioni 10 katika shindano la wazo bora la biashara linaloendeshwa na Mwenyekiti wa Makampuni ya IPP Media, Reginald Mengi kupitia kwenye mtandao wa kijamii wa twitter ametangazwa na wengine kumi wamejinyakulia kitita cha Sh milioni moja.

Fredrick Shayo,  mhitimu wa chuo kikuu na mjasiriamali anayejishughulisha na ufugaji wa kuku wa kienyeji ndiye aliyetangazwa kuwa mshindi kati ya washiriki 1,680 waliotuma maombi yao na kuingia katika kinyang'anyiro hicho cha kuwania Sh milioni 10  kama mtaji wa kuendeleza wazo bora la biashara.
Akizungumza katika hafla fupi ya kumtangaza mshindi wa shindano hilo, Dk Mengi aliwaasa vijana kutochagua kazi kwani kila kazi ina malipo.
“Vijana wengi ambao hawana kazi wanachagua kazi. Kila mtu anatakiwa afanye kazi ilimradi inampatia mshahara na baada ya hapo utakuwa na mtaji wa kujiendeleza katika shughuli nyingine na hata kufungua kampuni,” alisema  Mengi.
Alisema wapo Watanzania wanaowakatisha tamaa wengine kwa kusema Watanzania hawawezi kuwa mamilionea. Kitu ambacho si kweli kwani kuwa na mali nyingi kunatokana na juhudi ya kazi na pia ni baraka kutoka kwa Mungu.
“Mimi nawashangaa sana baadhi ya watu wanaosema hakuna mtu anaweza kuwa milionea hapa Tanzania. Kwa maana hiyo wanasubiri mamilionea kutoka nje ya nchi ili waweze kuwapigia magoti. Hii ni kuwakatisha tamaa vijana wenye ari ya kujituma na kutaka kuwa matajiri,” alisema.
Kwa upande wa mshindi wa shindano hilo Shayo alisema amefurahi sana kushinda kiasi hicho cha pesa kwani kitamsaidia kuongeza uzalishaji wa kuku wa kienyeji na kuuza katika maeneo mengi na kuwasaidia wengine kuongeza ufugaji wa kuku.
Washindi wengine walioingia kumi bora walizawadiwa kila mmoja Sh  milioni moja  kama pongezi ya kuwa wabunifu na kuwatia moyo wasikate tamaa na shughuli zao za ujasiriamali wanazozifanya.

No comments: