MAMA WA MTOTO ALBINO ASIMULIA JINSI ALIVYOJERUHIWA


Mama wa mtoto mwenye ulemavu wa ngozi, Yojana Bahati (1), Ester Thomas aliyelazwa katika hospitali ya Bugando akipatiwa matibabu baada ya kujeruhiwa, ameelezea jinsi alivyovamiwa na watu wasiojulikana.
Akizungumza na mwandishi, Ester (30) alisema alijeruhiwa juzi nyakati za usiku na watu wasiojulikana mkoani Geita baada ya kumvamia nyumbani kwao na kumpora mtoto wake mwenye ulemavu wa ngozi.
Akizungumza kwa shida hospitalini hapo, Ester alisema alivamiwa akiwa amelala na mtoto wake huyo ambapo walimkatakata kwa mapanga sehemu mbalimbali za mwili na kisha kutokomea kusikojulikana. 
Naye Mkuu wa kitengo cha dharura hospitalini hapo, Dk  Derick David alisema mgonjwa huyo alipokewa juzi saa nane mchana akitokea mkoani Geita.
Daktari alisema mgonjwa huyo ambaye hali yake sio ya kuridhisha, alijeruhiwa sehemu mbalimbali za mwili kutokana na kukatwa panga kwenye paji la uso pamoja na kukata sehemu ya mfupa wa pua.
"Tunamshukuru Mungu mgonjwa huyu anaendelea vizuri baada ya kufanyiwa upasuaji kwani kwa sasa hali yake ni tofauti na alivyopokewa," alisema. 
Alisema mama huyo anaendelea na matibabu ya majeraha na pia atapatiwa na huduma ya kisaikolojia kutokana na maumivu makali aliyonayo ya kuporwa kwa mtoto wake.

No comments: