MAANDALIZI HAFIFU CHANZO CHA UDANGANYIFU WA MITIHANI


Maandalizi hafifu ya watahiniwa wa mitihani kwa ngazi zote ndio chanzo kikubwa cha kuwapo udanganyifu katika mitihani ya mwisho.

Hayo yamebainishwa na Mkuu wa Idara ya Fedha na Utawala wa Baraza la Mitihani ya Tanzania (Necta), Daniel Mafie aliyekuwa akizungumzia mafanikio ya baraza hilo kwa niaba ya Katibu Mtendaji.
Alisema pamoja na kupungua kwa watahiniwa wanaofanya udanganyifu kwenye mitihani, lakini maandalizi hafifu ya wanafunzi wanachangia tatizo hilo.
“Unakuta mtahiniwa hajajiandaa vizuri na hapo hapo anataka kuwa na matokeo mazuri, hilo ndilo linalowafanya kuingia katika udanganyifu. Jamii inatakiwa kujua njia pekee ya kufanya vizuri katika mitihani ya mwisho ni kuwa na maandalizi mazuri,” alisema.
Alisema, Baraza lake kwa kushirikiana na Kamati za Uendeshaji wa Mitihani katika ngazi za Mikoa na Wilaya  na wasimamizi wameweza kudhibiti tatizo la wizi wa mitihani  kwa kiasi kikubwa.
Alitolea mfano mtihani wa kumaliza elimu ya msingi, udanganyifu umepungua kutoka watahiniwa 9,736 wa mwaka 2011 hadi mtahiniwa mmoja mwaka 2014, wakati Kidato cha Nne ni watahiniwa 3,303 kwa mwaka 2011 hadi watahiniwa 184 kwa mwaka 2014.
Katika matokeo ya mwaka 2014 yaliyotangazwa hivi karibuni kati ya watahiniwa 184 ambao matokeo yao yalifutwa kwa udanyanyifu, watahiniwa 128 walikuwa ni watahiniwa wa kujitegemea katika vituo viwili na watahiniwa 56 wakiwa ni watahiniwa wa shule.
Kwa upande wa Kidato cha Sita udanyanyifu umepungua kutoka watahiniwa 11 kwa mwaka 2011 hadi watahiniwa watatu mwaka 2014.

No comments: