KIWANDA CHA U-FRESH RUKSA KUZALISHA JUISI



Shirika la Viwango Tanzania (TBS) limekiruhusu kiwanda cha U-Fresh Food Limited cha Tegeta, Dar es Salaam, kiendelee kuzalisha juisi ya U-Fresh, kwa kuwa kimetimiza masharti ya viwango vya ubora vya juisi hiyo.

Mdhibiti Viwango vya Ubora wa bidhaa wa shirika hilo, Editha Protace alisema wakati wa kukifungua kiwanda hicho juzi kuwa, baada ya kukifanyia ukaguzi upya na kupima sampuli za juisi itakayoanza kuzalishwa, TBS imeridhishwa na maboresho muhimu yaliyofanyika.
"Pamoja na kuchukua vipimo muhimu na kuvifanyia uchunguzi kwenye maabara yetu ya chakula, tumeona kuna tofauti kubwa na vigezo vya viwango vya ubora katika juisi hiyo vimezingatiwa. Sasa walaji wanaweza kuanza kuitumia kwa sababu ni salama," Protace alisema.  
Akifafanua alisema, vipimo vimeonesha kuwa sukari tamu iliyokuwa ikitumiwa awali haijatumika tena.
"Cha msingi ni wanywaji kuwa makini na tarehe ya kutengenezwa kwa juisi hiyo kuepuka kupata iliyozuiwa awali, endapo kutakuwa na wafanyabiashara waliofanikiwa kuzificha hata baada ya msako".
Anasisitiza kuwa, juisi yoyote itakayoonesha imetengenezwa kabla ya Februari 16, mwaka huu, itakuwa miongoni mwa zilizozuiwa zisiuzwe awali, hivyo, atakayeinunua airejeshe kiwandani hapo au TBS kwa ajili ya ufuatiliaji zaidi.
 Meneja Masoko wa kiwanda hicho, Kephas Gembe aliwaahidi watanzania kuwa watazalisha juisi hizo kwa kuzingatia viwango vilivyopitishwa na shirika hilo, kulinda afya za walaji na mazingira.
Kwa mujibu wake, hakuna kiungo kisichofaa kitakachotumika kutengeneza juisi hiyo, hivyo wanapoinywa wawe na amani. "Tunaomba watakaoona juisi za zamani zikiendelea kuuzwa watutaarifu au kuijulisha TBS kwa hatua zaidi.
Miongoni mwa maboresho yaliyofanywa kiwandani hapo ni pamoja na kuweka mazingira ya kiwanda hicho katika hali ya usafi, kuandika maandishi katika ukuta wake kuwa ni kiwanda kinachozalisha juisi hiyo pamoja na kuweka maelezo muhimu katika vifungashio ikiwemo viungo vilivyotumika na anuani ya mzalishaji.

No comments: