JESHI LA POLISI, JWTZ WAPONGEZWA KAZI NZURI TANGA

Baadhi ya wakazi wa jijini Tanga wamepongeza hatua ya awali iliyofikiwa na Jeshi la Polisi kwa kushirikiana na JWTZ kwenye operesheni maalumu ya kusaka wahalifu pamoja na silaha waliokuwa wamejifisha katika mapango ya Majimoto yaliyopo eneo la Mzizima Amboni, nje kidogo ya mji.

Pongezi hizo zilitolewa jijini hapa jana na wakazi mbalimbali baada ya kupatikana kwa bunduki ya SMG yenye risasi 20, mhalifu pamoja na watu wengine wanaoendelea kuhojiwa kuhusiana na tukio hilo.
Walisema hatua hiyo ni mwanzo wa mafanikio ingawa wakaongeza kwamba jitihada zaidi zinapaswa kuongezwa ili kuhakikisha silaha na vitu vingine vyote vinapatikana kwa wakati kabla ya kuleta madhara kwa jamii.
Mwajuma Msagati, mkazi wa Chumbageni alisema taarifa ya jana ya Kamishna wa Operesheni na Mafunzo wa Jeshi la Polisi, Paul Chagonja alivyonukuliwa kwenye vyombo vya habari imeendelea kupunguza wasiwasi kwenye jamii.
“Unajua tetesi na taarifa zimekuwa nyingi kiasi kwamba huelewi ushike ipi au amuamini nani lakini kwa kweli taarifa kuhusu tatizo hilo ambazo zimeanza kutolewa wiki hii na Mkuu wa Mkoa wa Tanga pamoja na Jeshi la Polisi zimetupa matumaini mapya ya kuanza kuimarika kwa hali ya amani,” alisema.
Naye Peter Mgembe, mkazi wa Mafuriko Amboni alisema hali ya ulinzi na usalama iko shwari ingawa magari yenye vikosi vya askari yamekuwa yakipita pita kuelekea eneo tukio.
“Kwa kweli hata upitaji wa magari yenye askari sio ule wa kutisha kama ilivyokuwa mwishoni mwa wiki… kwa sasa wanaonekana kama wanafanya doria za kawaida …kwa hali hii tunayoiona sasa imeturejeshea tumaini la kuwepo kwa amani na tunapata ujasiri wa kuweza kuendelea na shughuli zetu za uzalishaji kama awali”, alisema.

No comments: