JAPAN YAJITOSA TATIZO LA KUKATIKAKATIKA UMEME DAR


Tatizo la kukatika kwa umeme katika Jiji la Dar es Salaam litakwisha baada ya Serikali ya Japan kupitia Shirika lake la Maendeleo la JICA kutoa msaada wa zaidi ya  Sh  bilioni 66, kwa ajili ya ukarabati na ujenzi wa vituo vipya vya kupozea umeme jijini Dar es Salaam.

Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco), Felchesmi Mramba alisema alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari,  Makao Makuu ya Tanesco Dar es Salaam.
Mramba alisema mradi huo utakapokamilika utapunguza mzigo kwenye vituo vya Oysterbay, Mbezi Beach na Makumbusho hivyo kuondoa adha ya kukatika kwa umeme kutokana na kuzidiwa.
“Vile vile wananchi wanaoishi maeneo jirani na vituo vipya watapata umeme wa uhakika na ulio bora zaidi. Kituo cha kupozea umeme cha Ilala kitaongezewa transfoma mbili hivyo kuweza kutoa umeme mwingi zaidi kwenye maeneo ya katikati ya Jiji pamoja na Kariakoo,” alisema.
Mkurugenzi huyo alisema kuwa, Kituo cha Muhimbili kitakuwa na laini ya peke yake itakayopeleka umeme kwenye Hospitali ya Taifa Muhimbili hivyo kuwa na umeme wa uhakika.
Mramba alisema Serikali ya Tanzania kwa kushirikiana na ya Japan walikubaliana kukarabati miundombinu ya umeme kwa kupanua na kujenga vituo vipya vya kupozea umeme katika Jiji la Dar es Saalam.
Alitaja kazi zitakazofanyika katika mradi huo kuwa ni ukarabati wa kituo cha kupozea umeme cha Ilala kwa kuweka transfoma mpya mbili za ukubwa wa MVA 60,kV 132/33.
Vile vile ujenzi wa jengo jipya la ‘control’ katika kituo cha kupoozea umeme cha Ilala, uwekaji na uvutaji wa waya wa njia ya pili ya kusafirisha umeme ya msongo wa kilovoti 132 kutoka Ubungo hadi Ilala na kupanua kituo cha kupozea umeme cha Msasani 33/11kV kwa kuweka transfoma nyingine mpya ya MVA 15, Kv 33/11.

No comments: