HAYA NDIO MAJINA YA WAKUU WA WILAYA WAPYA NA WALIOTEMWA


Rais  Jakaya Kikwete amefanya mabadiliko ya wakuu wa wilaya kwa kutengua uteuzi wa wakuu wa wilaya 12, kuteua wapya 27 na wengine 64 kubadilishwa vituo vyao.

Wakuu wa wilaya 42 ndiyo pekee wameendelea kubaki katika vituo vyao vya kazi.
Mabadiliko hayo yalitangazwa mjini Dodoma jana  na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda yakizingatia nafasi za wazi 27 zilizotokana na kufariki dunia kwa wakuu wa wilaya watatu, kupandishwa cheo watano kuwa wakuu wa mikoa na kupangiwa majukumu mengine wakuu wa wilaya 7.
Mabadiliko hayo yameibua baadhi ya majina muhimu katika siasa nchini, kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka huu na wakati huo huo yamekidhi madai ya wanasiasa, waliokuwa wameshikia bango kwamba uteuzi wa baadhi ya wakuu wa wilaya utenguliwe.
Baadhi ya majina mapya ni pamoja na Paul Makonda, Frederick Mwakalebela na Mboni Mhita.

Paul Makonda
Hii ni moja ya sura mpya, zilizoibuliwa kupitia mabadiliko hayo. Makonda anakuwa Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni jijini Dar es Salaam. Makonda ni Katibu wa Chipukizi na Uhamasishaji wa Umoja wa Vijana  wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM). Ni miongoni mwa vijana maarufu katika siasa ndani ya CCM na nchini kwa ujumla.
Kijana huyu amejipambanua katika suala zima la kambi za kuwania urais, baada ya kujitokeza hadharani kuzungumzia mbio za urais, akishutumu baadhi ya watu kwamba wanavuruga chama kwa lengo la kutaka urais 2015.
Aliungwa mkono na  baadhi ya wakongwe wa chama hicho,  ambao walimsifu kwamba ni kijana jasiri  kwa kukemea vitendo vinavyofanywa na baadhi ya wanaowania nafasi hiyo na kusema kwa kufanya hivyo, chama kitaendelea kupendwa.
Aidha katika mchakato wa Katiba Mpya, Makonda ni miongoni mwa vijana waliotengeneza majina kuanzia kwenye Bunge Maalumu la Katiba hadi nje ya bunge hilo.
Alikuwa miongoni mwa wanasiasa, waliosimama kidete kupigia debe muundo wa Muungano wa Serikali mbili, uliopitishwa ndani ya Katiba Inayopendekezwa.
Katika Bunge hilo Maalumu  mjini Dodoma, Makonda alikuwa miongoni mwa wajumbe waliopanda hadharani baadhi ya vipengele vilivyowasilishwa na Tume ya  Mabadiliko ya Katiba iliyoongozwa na Jaji mstaafu Joseph Warioba.
Ni katika bunge hilo,  kwa kuzingatia msimamo wake, Makonda alijikuta akisigana na mjumbe mwingine, Ezekiel Oluoch  aliyekuwa akipinga mabadiliko ya Kanuni, yaliyotoa nafasi kwa wajumbe kupiga kura wakiwa nje ya Bunge. Kanuni hiyo, hata hivyo, ilipitishwa.
Oluoch aliwasilisha malalamiko kwa Katibu wa Bunge Maalumu la Katiba, Yahya Hamad, akisema Makonda alisema uongo juu yake kwa kusema anataka kugombea nafasi ya ubunge huku akimtaka asitumie Bunge Maalumu la Katiba kujitangaza.
Jina la Makonda liliendelea kusikika pia Novemba mwaka jana, alipotuhumiwa kuhusika katika vurugu zilizotokea jijini Dar es Salaam kwenye mdahalo ulioitishwa na Mfuko wa Mwalimu Nyerere kujadili Mchakato wa Katiba pamoja na Katiba Inayopendekezwa.
Vurugu hizo zilihusisha kundi la vijana, waliodaiwa kumzomea Jaji  Warioba, alipokuwa akiwasilisha mada katika mdahalo huo.
Hata hivyo, Makonda alikanusha kuhusika kumdhalilisha Warioba; akisema wamelenga kumchafua kisiasa. Alijitetea kwamba  ndiye alisaidiana na watu wengine, kumtoa nje ya ukumbi mzee huyo asidhuriwe na vijana, waliokuwa wakifanya vurugu, ikiwemo kurusha chupa za maji.

Frederick Mwakalebela
Mwakalebela amepangiwa wilaya ya Wanging'ombe mkoani Njombe.  Zinapotajwa siasa za mkoa wa Iringa na hata utwaaji wa Jimbo la Iringa Mjini kwa upinzani, jina la Mwakalebela linahusishwa.
Baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 uliompa ushindi Mchungaji Peter Msigwa kutoka Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) katika Jimbo la  Iringa Mjini, kulikuwa na kauli za kushutumu kitendo cha Mwakalebela kuenguliwa katika kura za maoni za CCM.
Wachambuzi wa mambo ya siasa wanaeleza kuwa kitendo cha Mwakalebela kupewa Wilaya ya Wanging'ombe  ambayo  ipo jirani na Iringa Mjini,  kutampa fursa ya kujijenga zaidi kisiasa na hivyo wakati utakapofika atatimiza tena azma yake ya kuwa mwakilishi wa Iringa Mjini.
Umaarufu wa Mwakalebela ulianzia wakati akiwa Katibu Mkuu wa lililokuwa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF). Alishikilia nafasi hiyo kuanzia mwaka 2006  hadi 2010.
Baada ya mkataba wake kumalizika, Mwakalebela alijitosa kuomba kugombea ubunge wa Iringa Mjini kupitia CCM. Hata hivyo, alienguliwa na chama  kugombea nafasi hiyo licha ya kuwa alikuwa ameshinda kwenye kura za maoni.
Badala yake,  CCM ilimteua Monica Mbega  aliyewahi kuwa Naibu Waziri wa Fedha na Mkuu wa Mkoa, kuingia kwenye kinyang'anyiro hicho. Hata hivyo, Mbega alidondoshwa na Mchungaji  Msigwa.

Waliotenguliwa
Ingawa haikuwekwa bayana sababu za baadhi kutenguliwa ukuu wa wilaya na wengine kuwekwa ‘kiporo’ kwa ajili ya kupangiwa majukumu mengine,  inadhihirisha uteuzi huu umejaribu pia kuzingatia madai na malalamiko dhidi ya baadhi ya wakuu wa wilaya.
Baadhi yao, wameponzwa na migogoro kati ya wakulima na wafugaji.  Mfano ni Martha Umbulla  aliyekuwa Wilaya ya Kiteto.
Katika mkutano wa Bunge, Mei mwaka jana, Umbulla alishikiwa bango na wabunge kadhaa waliotaka uteuzi wake wa ukuu wa wilaya utenguliwa kwa kile kilichoelezwa kuwa ndiyo chanzo cha migogoro, iliyosababisha mauaji ya wakulima kutoka wilayani Kongwa yaliyofanyika wilayani kwake, Kiteto.
Mathalani,  Mbunge wa Arusha, Godbless Lema alimshutumu Umbulla (Mbunge wa Viti Maalum) kwamba alikuwa akiwabagua wananchi.
Ingawa Umbulla  alijaribu kueleza kilichojiri, pia  Mbunge wa Kongwa, Job Ndugai ambaye ni Naibu Spika wa Bunge, alimshutumu Umbulla akisema ubaguzi wa viongozi wilayani Kiteto ndicho chanzo cha mauaji hayo.

Waliowekwa kiporo
Miongoni mwa ambao Waziri Mkuu amesema kuwa watapangiwa majukumu mengine ni Mrisho Gambo, aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Korogwe ambaye mwaka jana, alifikishwa mbele ya Baraza la Maadili ya Viongozi wa Umma jijini Dar es  Salaam, akituhumiwa  kutumia vibaya madaraka yake.
Mkurugenzi  Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Korogwe, Anna Mwalende ni miongoni mwa waliofika mbele ya Baraza kutoa ushahidi dhidi ya Gambo na kueleza namna alivyodhalilishwa na kunyanyaswa .
Mbele ya Mwenyekiti wa Baraza, Jaji mstaafu Hamisi Msumi, shahidi huyo alidai mkuu huyo wa wilaya  amekuwa na lugha chafu kwa viongozi wenzake, ana utawala wa mabavu bila kuzingatia kanuni na sheria, jambo ambalo ni kikwazo kwa maendeleo ya wilaya hiyo.
Mabadiliko yenyewe:

Walioenguliwa
Wakuu wa wilaya ambao uteuzi wao umetenguliwa na vituo vyao katika mabano ni  James Ole Millya (Longido), Elias Wawa Lali (Ngorongoro), Alfred Msovella (Kongwa), Danny Makanga (Kasulu), Fatma Kimario (Kisarawe), Elibariki Kingu (Igunga), Dk Leticia Warioba (Iringa), Evarista Kalalu (Mufindi) ,Abihudi Saideya (Momba), Martha Umbulla (Kiteto), Khalid Mandia (Babati) na Elias
Goroi (Rorya).

Wanaopangiwa majukumu mengine
Cosmas Kayombo (Simanjiro), Ngemela Lubinga, (Mlele), Juma Madaha, (Ludewa), Mercy Silla, (Mkuranga), Ahmed Kipozi (Bagamoyo), Mrisho Gambo (Korogwe) na Elinas Pallangyo (Rombo).

Wakuu wa Wilaya Wapya
Zelothe Steven aliyekuwa Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mtwara ambaye sasa ni Mkuu wa Wilaya ya (Musoma), Mboni Muhita ambaye ni Makamu Mwenyekiti wa Taifa Umoja wa Vijana wa CCM, anakuwa Mkuu wa Wilaya ya Mufindi.
Katibu wa Chipukizi na Uhamasishaji wa kitengo cha hamasa cha Umoja wa Vijana  wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM), Paul Makonda anakuwa Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni,  
Shaabani Kissu ambaye ni mtangazaji wa Shirika la Utangazaji la Taifa (TBC), anakuwa mkuu wa Wilaya ya  Kondoa.
Wengine ni Mariam Mtima (Ruangwa), Dk Jasmini Tiisike (Mpwapwa), Paloleti Mgema (Nachingwea), Fadhili Nkurlu, (Misenyi), Felix Lyaniva (Rorya), Fredrick Mwakalebela (Wanging'ombe), Fransis Mwango (Bahi), Kimiang'ombe Samwel (Kiteto).
Wengine ni Husna Msangi (Handeni), Emmanuel Uhaula (Tandahimba), Hashim Mngandilwa (Ngorongoro), Mariam Juma (Lushoto), Thea Ntara (Kyela), Ahmad Nammohe (Mbozi), Pili Moshi (Kwimba), Mahmoud Kambona (Simanjiro), Glorius Luoga (Tarime), Zainabu Telack (Sengerema), Zuhura Ally (Uyui).

Waliobadilisha vituo
Nyerembe Munasa anatoka Arumeru  kwenda Mbeya, Jordan Rugimbana kutoka Kinondoni kwenda  Morogoro, Fatma Ally kutoka Chamwino kwenda Mtwara, Lephy Gembe kutoka Dodoma Mjini kwenda Kilombero, Christopher Kangoye kutoka Mpwapwa kwenda Arusha, Omary Kwaang’ kutoka Kondoa kwenda Karatu, Francis Isack kutoka Chemba kwenda Muleba na  Betty Mkwasa kutoka Bahi kwenda Dodoma Mjini.
Wengine ni Agnes Hokororo kutoka Ruangwa kwenda Namtumbo, Regina Chonjo kutoka Nachingwea kwenda Pangani, Husna Mwilima kutoka Mbogwe kwenda Arumeru, Gerald Guninita kutoka Kilolo kwenda Kasulu, Zipporah Pangani kutoka Bukoba kwenda Igunga na Issa Njiku kutoka Misenyi kwenda Mlelea.
Richard Mbeho kutoka Biharamulo kwenda Momba, Lembris Marangushi kutoka Muleba kwenda Rombo, Ramadhani Maneno kutoka Kigoma kwenda Chemba, Venance Mwamoto kutoka Kibondo kwenda Kaliua, Gishuli Charles kutoka Buhigwe kwenda Ikungi.
Wengine ni Novatus Makunga kutoka Hai kwenda Moshi, Anatory Choya kutoka Mbulu kwenda Ludewa, Christine  Mndeme kutoka Hanang kwenda Ulanga, Jackson Musome kutoka Musoma kwenda Bukoba, John Henjewele kutoka Tarime kwenda
Kilosa, Dk Norman Sigalla kutoka Mbeya kwenda  Songea, Dk Michael Kadeghe kutoka Mbozi kwenda Mbulu, Crispin Meela kutoka Rungwe kwenda Babati, Magreth Malenga kutoka Kyela kwenda Nyasa.
Wengine ni Saidi Amanzi kutoka Morogoro kwenda Singida, Antony Mtaka utoka Mvomero kwenda Hai, Elias Tarimo kutoka Kilosa kwenda Biharamulo, Francis Miti kutoka Ulanga kwenda Hanang, Hassan Masala kutoka Kilombero kwenda Kibondo.
Angelina Mabula anatoka  Butiama kwenda Iringa, Farida Mgomi kutoka Masasi kwenda Chamwino, William Ndile kutoka Mtwara kwenda Kalambo, Ponsian Nyami kutoka Tandahimba kwenda Bariadi, Mariam Lugaila kutoka Misungwi kwenda Mbongwe, Mary Onesmo kutoka Ukerewe kwenda Buhigwe, Karen Yunus kutoka Sengerema kwenda Magu, Josephine Matiro kutoka Makete kwenda Shinyanga, Joseph Mkirikiti kutoka Songea kwenda Ukerewe.
Wengine ni Abdula Lutavi kutoka Namtumbo kwenda Tanga, Ernest Kahindi kutoka Nyasa kwenda Longido, Anna Nyamubi kutoka Shinyanga kwenda Butiama, Rosemary Kirigini kutoka Meatu kwenda Maswa, Abdallah Kihato kutoka Maswa kwenda Mkuranga, Erasto Sima kutoka Bariadi kwenda Meatu, Queen Mulozi kutoka Singida kwenda Urambo, Yahya Nawanda kutoka Iramba kwenda Lindi, Manju Msambya kutoka Ikungi kwenda Ilemela, Saveli Maketta kutoka Kaliua kwenda Kigoma, Bituni Msangi kutoka Nzega kwenda Kongwa na Lucy Mayenga kutoka Uyui kwenda Iramba.
Wengine waliohamishwa ni Majid Mwanga kutoka Lushoto kwenda Bagamoyo, Muhingo Rweyemamu kutoka Handeni kwenda Makete, Hafsa Mtasiwa kutoka Pangani kwenda Korogwe, Dk Nassoro Hamid kutoka Lindi kwenda Mafia, Festo Kiswaga kutoka Nanyumbu kwenda Mvomero, Selemani Mzee kutoka Kwimba kwenda Kilolo, Esterina Kilasi kutoka Wanging’ombe kwenda Muheza, Subira Mgalu kutoka Muheza kwenda Kisarawe na Jacqueline Liana kutoka Magu kwenda Nzega.

Waliobaki Vituoni
Waziri Mkuu alitaja waliobaki kwenye vituo vyao ni Jokwika Kasunga (Monduli), Raymond Mushi (Ilala), Sophia Mjema (Temeke), Amani Mwenegoha (Bukombe), Ibrahim Marwa (Nyang'hwale), Rodrick Mpogolo (Chato), Manzie Mangochie (Geita), Darry Rwegasira (Karagwe) na Benedict Kitenga (Kyerwa).
Wengine ni Constantine Kanyasu(Ngara), Paza  Mwamulima(Mpanda), Peter Kiroya (Kakonko), Hadija Nyembo(Uvinza), Dk Charles Mlingwa(Siha), Shaibu
Ndemanga (Mwanga), Herman Kapufi (Same), Ephraim Mbaga (Liwale), Abdallah Ulega (Kilwa) na Joshua Mirumbe.
Aliwataja wengine ni Deodatus Kinawiro (Chunya), Rosemary Senyamule (Ileje), Gulamhusein Shaban (Mbarali), Christopher Magala (Newala), Baraka Konisaga(Nyamagana), Sarah Dumba (Njombe), Halima Kihemba (Kibaha), Nurdin Babu (Rufiji), Mathew Sedoyeka (Sumbawanga).
Iddi  Kimanta (Nkasi), Chande Nalicho (Tunduru), Senyi  Ngaga (Mbinga), Wilson Nkambaku (Kishapu), Benson Mpesya (Kahama), Paul Mzindakaya (Busega), Georgina Bundala (Itilima), Fatma Toufiq (Manyoni), Edward Ole Lenga (Mkalama), Hanifa Selengu (Sikonge), Suleiman Kumchaya (Tabora), Mboni Mgaza (Mkinga) na Selemani Liwowa (Kilindi).

No comments: