Licha
ya Mamlaka ya Chakula, Dawa na Vipodozi (TFDA) kufuta usajili na kupiga
marufuku uuzaji wa dawa duni, zenye madhara na zisizofaa kwa matumizi ya
binadamu, dawa hizo zimegundulika kuuzwa holela na baadhi ya wamiliki wa maduka
ya dawa katika kata ya Kisesa wilayani Magu mkoani Mwanza.
Hayo
yameelezwa na wakazi wa Kisesa wilayani hapa, wakati wa semina ya siku moja iliyojadili
visababishi vya ulemavu katika jamii, ambapo walisema madhara ya ulemavu yanatokana
na watu kutumia dawa zilizopita muda wake.
Semina
hiyo ilihudhuriwa na washiriki zaidi ya 50 kutoka katika makundi ya walemavu wa
kutoona, viungo, kutosikia, uono hafifu, ngozi na watendaji wa vijiji na
vitongoji, iliyoandaliwa na asasi ya watu wenye ulemavu ya SANJO na kufadhiliwa
na Shirika la the Foundation for Civil Society.
Wananchi
hao waliiomba Serikali kupitia TFDA, kuwachukulia hatua wamiliki hao wa maduka
wanaoendelea kuuza dawa hizo zilizofutiwa usajili kwa madai kuwa zinaweza
kuwasababishia madhara na pengine vifo.
Dawa
zilizofutiwa usajili na TFDA ni dawa ya kutibu fungus (ya vidonge na kapsuli)
aina ya Ketoconazole, dawa za kutibu mafua na kikohozi za maji, vidonge na
kapsuli zenye kiambato hai aina ya phenylpropanol amine na dawa ya kuua
bakteria ya sindano, aina ya Chloramphenicol Sodium Succinate.
Zingine
ni dawa ya kuua bakteria ya maji na kapsuli aina ya cloxacillin, malaria ya
vidonge yenye mchanganyiko wa Sulphadoxine na Pyrimethamine(SP) na dawa
aina ya Amikacin, Levofloxacin.
Watoa
huduma pia waliagizwa kusimamia mabadiliko ya matumizi ya dawa aina ya SP ili
ziweze kutumika kwa wajawazito tu na dawa aina ya kanamycin, amikacin na
Levofloxacin zitumike kwa wagonjwa wa kifua kikuu tu kwenye hospitali, vituo
vya afya na zahanati.
Akizungumza
katika semina hiyo, mkazi wa Kisesa, Romanus Kalista alisema licha ya Serikali
kupitia TFDA kubaini kuwepo kwa dawa duni kwa watumiaji na kufuta usajili wake
kwa matumizi ya binadamu, anaona hali hiyo imewachanganya wananchi kutokana na
ukweli wananchi wengi kabla ya kufutiwa usajili, walikuwa wakizitumia.
“Dawa
hizi hizi zimetumiwa na wananchi kwa muda mrefu, je wananchi waliokuwa
wakizitumia endapo watagundulika kupata madhara nani atawahudumia, na ukweli ni
kuwa kama zilikuwa na madhara wananchi nao watakuwa wameathirika”, alihoji.
Aliongeza,
“Hata hivyo dawa hizo zilizopigwa marufuku bado zinatumika hapa Kisesa na
TFDA bado haijatoa elimu ya kutosha kwa wananchi, na kibaya ni kwamba dawa hizi
bado zinauzwa kwenye maduka ya dawa.”
Alisema
yeye binafsi anashangaa kusikia serikali imetangaza kufuta usajili wa
baadhi
ya dawa zilizoharibika, ambazo vijijini zilikuwa zinatumiwa na wananchi na kuhoji
kuwa kama dawa hizo hazina ubora ni kwanini zisipigwe
marufuku
zinakotengenezwa hususan viwandani.
Kwa
upande wake, Agnes Mathias ambaye ni mkazi wa Kisesa na ambaye alikiri kuwa
aliwahi kufanya kazi ya kuuza dawa katika duka la dawa, aliitaka Serikali itoe
elimu zaidi kwa umma.
“Bado
dawa zilizopigwa marufuku zinauzwa huku kwetu, mimi nilikuwa muuzaji najua
mbinu zinazotumika kuuza dawa, wauzaji wanauza kwa kufungua mlango kidogo,
ningeomba serikali ingetuma wataalam waje kufanya ukaguzi vinginevyo madhara
yatakuwa makubwa”, alionya.
Kwa
upande wake, mkazi wa Kisesa John Alphonce licha ya kuitaka Serikali kupambana
na mila potofu juu ya watu wenye ulemavu, alisema kuwa baadhi ya dawa
wanazotumia akinamama wajawazito husababisha ulemavu kwa mtoto
anayezaliwa.
“Na
kwa sababu hiyo mimi sikubaliani na hoja kuwa ulemavu ni mpango wa Mungu,
inawezekana mama anaweza akawa amemeza dawa au kuchomwa sindano wakati wa
ujauzito na baadae mtoto anayezaliwa hupata ulemavu”, alisema.
Mwezeshaji
wa semina hiyo, Mwanasheria wa Chama cha Walemavu Mkoa wa Mwanza (CHAWATA),
Revocatus Almasi aliitaka jamii kushiriki kamilifu katika kukabiliana na
changamoto zinazowapata watu wenye ulemavu nchini na waachane na mila potofu.
“Kutokana
na mila zilizopitwa na wakati, jamii inaamini kuwa watu wenye ulemavu ni
tegemezi, wasio na uwezo,wanastahili kusaidiwa na watu wasio na ulemavu ili
waweze kumudu maisha yao”, alisema.
Mkurugenzi
wa SANJO, Joseph Msuka alisema lengo la semina hiyo ilikuwa ni kuelimisha jamii
kupitia kwa watu wenye ulemavu na watendaji wa vijiji na kata wajue
madhara yakuteketeza watoto wanaozaliwa na ulemavu kunakofanywa na baadhi ya
watu katika jamii, hasa wanaume na baadhi ya akinamama kutumia dawa zilizopita
muda wake wa matumizi.
Akizungumza
na mwandishi kwa njia ya simu kutoka mkoani Iringa, Kaimu Meneja wa TFDA Kanda
ya Ziwa, Moses Mbamba alisema wamiliki wa dawa wanaouza dawa hizo zilizofutiwa
usajili, wanajali zaidi kutafuta pesa kwa gharama ya maisha ya watu
kuliko
kujali uhai wa binadamu. Alisema ofisi yake itafanya ukaguzi wa haraka
katika
eneo hilo.
“Kesho
nitamuagiza msaidizi wangu aende huko mara moja kufanya
ukaguzi
na watakaobainika tutawafikisha mahakamani mara moja, hatutakubali wao kuendelea
kuuza dawa zilizofutiwa usajili,” aliahidi.
No comments:
Post a Comment