CUF YAZOA WANACHAMA WAPYA 891 LINDI



Chama cha Wananchi (CUF) mjini Lindi kimepata wanachama wapya kutoka CCM wapatao 891 kuanzia mwezi Desemba mwaka jana hadi Februari mwaka huu.

Katibu wa chama hicho mjini hapa, Rashidi Ndauka alisema hayo jana wakati alipokuwa akizungumza na gazeti hili ofiisni kwake mjini hapa.
Alisema wanachama hao wamegawanyika sehemu kuu mbili, ambako wanachama 775 ni wanachama wapya na  116 wanatokea CCM wakiwemo na viongozi wao.
Ndauka alisema viongozi waliojiunga na chama hicho na Mwenyekiti wa CCM kata ya Ngapa, Hamisi Nganga kutoka tawi la Mkwaya, ambako katibu wa tawi hilo, Abdallah Mchewa alijiunga na chama hicho.
Katibu huyo wa CUF alisema tatizo lililowafanya wanachama hao wa CCM wakihame chama chao na kujiunga na CUF ni kutokana na huduma ya maji waliyoipata ambayo imetokana na juhudi binafsi za mbunge wa jimbo la Lindi Mjini, Salumu Baruany.
Alisema kuwa hii ni mara ya kwanza kwa wananchi hao kupatiwa huduma ya maji licha ya kuwa miaka ya nyuma jimbo hilo lilikuwa linaongozwa na CCM.
Pia, alisema wananchi wa jimbo hilo walikuwa na matatizo mengi, ikiwemo ukosefu wa mbegu bora za mazao, hali inayofanya wakulima wanakuwa na wakati mgumu katika upatikanaji wa pembejeo hizo, kwa ajili ya kuzitumia mashambani, mwaka kipindi cha kilimo.
Mwenyekiti wa CUF na Mbunge wa Lindi Mjini kupitia CUF, Salumu Baruany aliwashauri wananchi wajiunge na chama hicho, kwani itakuwa rahisi kwao kupata maendeleo yao.
Alisema kwamba kipindi kifupi chama chake kimejitahidi kuibana Serikali kujenga barabara za mjini, mradi wa maji wa Ng’apa na kuboresha miundombinu mbalimbali.
Baruany alisema kama wananchi wataamua kujiunga na upinzani, basi watakuwa wanapata maendeleo, kwani mikoa ya Kaskazini ambako wapinzani wapo wengi na kuna maendeleo mazuri, miundombinu ya kielimu, nishati za umeme, majengo ya shule na zahanati ni bora. 

No comments: