Wakati Wazanzibari wakisubiri mchakato wa
kupiga kura ya maoni ya Katiba
Inayopendekezwa kuruhusu kuanza uchimbaji mafuta na gesi, baadhi ya viongozi
wakuu serikalini wameshutumiwa kupinga na kuhamasisha wafuasi kususa mchakato.
Makamu wa Kwanza wa Rais, Seif Sharif Hamad
(pichani) ametajwa kuhusika na matamshi ambayo yanayoweza kukwamisha visiwa hivyo
kuchimba nishati hiyo.
Ametajwa kutotabirika kimisimamo kutokana na
kutoa kauli zinazokinzana anapokuwa chini ya wadhifa wake serikalini wa makamu wa kwanza wa Rais na pale anapokuwa
kwenye chama.
Imeelezwa kwamba, hivi karibuni akiwa nchini Qatar ambako alikutana na viongozi, wafanyabiashara na wawekezaji,
aliwataka waje kuwekeza akisema
mazingira yameimarika kutokana na amani na utulivu.
Aidha, alisema Zanzibar iko katika hatua za
mwisho za kukaribisha kampuni mbali mbali za nje kuwekeza katika mafuta na
gesi; hatua inayosubiri kukamilika kwa mchakato wa kura ya maoni ya katiba
itakayoruhusu Zanzibar kuchimba mafuta.
Seif alitoa kauli hizo katika nyakati tofauti
wakati alipokutana na Waziri wa Nishati na Viwanda wa Qatar, Dk Mohamed Saleh
Al-Sada. Asilimia 70 ya pato la taifa la nchi hiyo inatokana na gesi.
Hata hivyo, katika kile kilichoelezwa ni
kubadilika ndani ya chama, katika hotuba yake
mwishoni mwa wiki wakati akizindua kamati za uchaguzi wa chama
chake, aliwataka Wazanzibari kususa
mchakato wa kura ya maoni.
Alisema katika kuhakikisha kwamba huu ni mwaka
wa uamuzi na siyo wa uchaguzi, aliwataka wananchi kususa mchakato wa kura ya
maoni na kutaka wajipange kuhakikisha
CUF wanashinda katika uchaguzi mkuu na kushika dola.
“Wamepiga ngoma wenyewe, wamecheza wenyewe na
sasa tuwaache wenyewe waicheze katiba hiyo ni ya Dodoma na ibaki huko huko,”
alisema kwenye mkutano huo wa hadhara.
Kwa mujibu wa makamu huyo wa rais, Zanzibar
haiwezi kupata maendeleo ya kweli kwa mfumo wa serikali mbili uliopo sasa ambao ulipitishwa katika Katiba
Inayopendekezwa.
"Mimi napinga Muungano wa Serikali
mbili…kama tungekuwa na uwezo katika Muungano tuliokuwa nao sasa matukio ya
kukataliwa kwa huduma za mashirika ya ndege kama Qatar na Uturuki kamwe
yasingetokea,” alisema Seif.
Hata hivyo, kauli hizo alizotoa kwenye
mkutano, zimepokewa kwa hisia tofauti na
wananchi wengi wa Zanzibar hususani wanaotaka mabadiliko wakiitaja kuwa ni ya
kichochezi.
Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM)
Zanzibar, Vuai Ali Vuai akizungumza na waandishi wa habari, alisema chama
hakishangazwi na kauli alizoita za ‘ukigeugeu’ za kiongozi huyo wa CUF.
Vuai alisema mwaka 2010 wajumbe wa Baraza la
Wawakilishi kutoka CCM na CUF kwa pamoja walikubaliana na kufikia azimio la
kutaka kuona mafuta na gesi yanaondolewa katika orodha ya mambo ya muungano.
Alisema la kushangaza ni kuona kwamba, fursa waliyokuwa wanaitaka sasa imekuja
ambayo itatoa nafasi ya Zanzibar kuchimba mafuta na gesi lakini sasa wanapinga na kukataa moja kwa moja.
Alimtaja Seif kwamba, yupo kuona kwamba kwa njia yoyote anaingia
madarakani bila ya kujali maslahi ya Wazanzibari walio wengi.
"Mimi sishangazwi na kauli za Maalim Seif
kwani akiwa Qatar alisema jambo jingine huku akihamasisha wawekezaji, lakini
alipozungumza na wanachama wake ametoa kauli nyingine kabisa ya kutaka wafuasi
wake na Wazanzibari kwa ujumla kususa mchakato huo,” alisema Vuai.
Akifafanua zaidi, alisema Seif hataki kuona Muungano wa Tanganyika na
Zanzibar udumu na kwamba ndiyo sababu anatoa visingizio kwamba wananchi
wanauchukia.
Alitoa mfano kwamba, ajira nyingi za vijana
zinazotoka Tanzania Bara ambapo vijana kutoka Zanzibar wamenufaika na
ajira Idara ya Uhamiaji na pia walimu
wengi wamepata fursa kufanya kazi bara.
Kwa mujibu wa Vuai, Serikali ya Mapinduzi ya
Zanzibar haina uwezo wa kuwapatia vijana wengi kwa wakati mmoja ajira .
Alihimiza vijana kutokubali kurubuniwa na kusikiliza kauli alizoita za
upotoshaji zinazotolewa na Maalim Seif.
Wakati huo huo, baadhi ya wakazi visiwani hapa
wameshauri Serikali kuimarisha ulinzi katika kipindi cha kura ya maoni kuepuka
vurugu za wapinzani wanaoweza kuzuia wafuasi wa CCM kupiga kura.
“Tunaiomba Serikali kujitayarisha na kila aina
ya fujo zitakazojitokeza katika kipindi cha mchakato wa kura ya amani kwani
wapo wapinzani wameonesha nia ya kutishia kuharibu zoezi hilo,” alisema Ali
Juma, mkazi wa Mikunguni na kutaja hali
hiyo kuanza kujitokeza Pemba.
No comments:
Post a Comment