CHENGE, TIBAIJUKA KIKAANGONI BARAZA LA MAADILI


Mbunge wa Bariadi Magharibi, Andrew Chenge Jumatano atasimama mbele ya Baraza la Maadili kujibu tuhuma za kukiuka maadili ya uongozi na kujipatia Sh bilioni 1.6 ambazo aligawiwa kutoka katika fedha za akaunti ya Tegeta Escrow.

Profesa Anna Tibaijuka ambaye alitimuliwa Uwaziri wa Ardhi, Nyumba na Makazi kutokana na kujipatia Sh bilioni 1.6 kutoka kwa mmiliki wa kampuni ya VIP Engineering, James Rugemalira atajibu tuhuma hizo Alhamisi.
Ratiba iliyotolewa na Baraza la Maadili, jijini Dar es Salaam inaonesha kuwa aliyekuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Katiba na Sheria, William Ngeleja ambaye pia ni Mbunge wa Sengerema, atasimama mbele ya Baraza hilo Jumatatu ijayo.
 Wengine watakaopanda kizimbani ni Mkurugenzi wa Sheria wa Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Rugonzibwa Mujunangoma atakayehojiwa Jumatatu ijayo.
Wengine ni  Mnikulu Shaban Gurumo atakayehojiwa  Machi 4, akifuatiwa na  Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Ufilisi na Udhamini (RITA), Philip  Saliboko na  Machi 6 atahojiwa Naibu Kamishna  Upelelezi na Kodi Mamlaka ya Mapato Tanzania  (TRA), Loicy Appollo.
Ratiba hiyo inaonesha kuwa Machi 9 atahojiwa Mkurugenzi  Mdhibiti  Uchumi Mamlaka ya Usafiri wa Anga, Dk Benedict Diu akifuatiwa na Meya wa Halmashauri ya  Manispaa ya Tabora, Gulam Remtullah.Akizungumza Dar es Salaam,  Mwenyekiti wa Baraza hilo, Jaji mstaafu Hamis Msumi alisema ratiba ya kuwahoji viongozi, ilitakiwa kuanza jana ikianza na aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya  Korogwe, Mrisho Gambo. Hata hivyo, Gambo aliwasilisha barua kwamba anaumwa na atashindwa kuhudhuria.Vievile,  Gambo aliwasilisha cheti cha daktari akitakiwa kupumzika kwa wiki mbili, jambo lililosababisha Baraza hilo kuahirisha kusikiliza shauri lake  hadi hapo litakapopanga kikao kingine.Kutokana na kuanza kuwapandisha kizimbani watuhumiwa  wa sakata la Escrow, Baraza litatoa uamuzi wa ama wahusika hao wafikishwe mahakamani, au la, kulingana na hatia watakazokutwa nazo. 
Kashfa ya Escrow iliyonguruma mwaka jana bungeni, imesababisha baadhi ya watuhumiwa kujiuzulu nyadhifa zao na wengine kuvuliwa madaraka, akiwamo Profesa Tibaijuka aliyewekwa pembeni na Rais Jakaya Kikwete Desemba mwaka jana.  
Chenge alikuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Bajeti na aliachia wadhifa huo hivi karibuni. Ngeleja aliyekuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Katiba, Sheria na Utawala na Mbunge wa Lupa na Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini , Victor Mwambalaswa, nao walijiuzulu hivi karibuni. 
Chenge na Profesa Tibaijuka kila mmoja alipata mgawo wa Sh bilioni 1.6 huku Ngeleja akipata Sh milioni 40.4 kutoka kwa James Rugemalira wa VIP Engineering and Marketing Limited, zikiwani mgawo wa Tegeta Escrow.
Akaunti ya Tegeta Escrow ilifunguliwa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) mwaka 2006 kwa ajili ya kuhifadhi fedha za malipo ya tozo ya uwekezaji (capacity charges), zilizokuwa zinalipwa na  Shirika la Umeme nchini (TANESCO) kabla hazijakabidhiwa kwa anayelipwa, ambaye ni Kampuni binafsi ya kufua umeme ya IPTL. Kabla ya hapo Tanesco ilikuwa inalipa moja kwa moja kwa IPTL.   Ilifunguliwa  ili kutoa nafasi kwa pande hizo mbili kumaliza tofauti zao kuhusu kiwango cha tozo hiyo.

No comments: